Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Saturday, February 13, 2016

MAISHA YA MATESO KIJIJINI KAPUNGA 1.

Na Joachim Nyambo

HATIMAYE mgogoro wa kimpaka uliodumu kwa zaidi ya miaka 10 kati ya mwekezaji katika shamba la Kapunga kampuni ya Expot Trading na wakazi wa kijiji cha Kapunga wilayani Mbarali umemalizika.Ukomo wa mgogoro huu umefikiwa kwa mwekezaji kuridhia kiasi cha hekta 1,870 za ardhi kurejeshwa kwa kijiji hicho.


Mapema mwezi Januari mwaka huu,Waziri wa Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi Willium Lukuvi alitangaza kurejeshwa kwa hekta hizo za ardhi kwa nyakati tofauti alipozungumza na wakazi wa kijiji cha Kapunga kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kijijini hapo na pia alipokuwa kwenye kikao na madiwani na watendaji wa halmashauri ya wilaya ya Mbarali.

Lakini nini kilikuwa kiini cha mgogoro huu na yapi yaliyojiri wakati wa msuguano baina ya wakazi wa kijiji cha Kapunga na mwekezaji.Maisha ya pande hizi mbili yamekuwaje katika kipindi chote cha mgogoro.Hapa ndipo ninapoamua kukupitisha katika maisha ya miaka hii kumi kupitia makala haya mfululizo niliyoamua kuyaiya Maisha ya mateso Kijijini Kapunga.

Mwaka 1985 wakazi wa kijiji cha Kapunga wilayani Mbarali waliombwa na serikali kutoa eneo chepe chepe lenye ukubwa wa hekta 5500.Ombi hilo lililenga serikali kupata eneo hilo kwaajili ya kilimo cha umwagiliaji.Ni hasa ilikuwa ni kuboresha kilimo nchini kutoka kile cha matumizi ya maji ya mvua ambacho ni cha msimu.

Inasemekana Mwalimu Julius Nyerere ndiye aliyeomba eneo hilo baada ya kupita katita vijiji vilivyopo pembezoni mwa barabara kuu na kukuta wakazi wakiuza mahindi mabichi na mbogamboga.Vijiji hivi ni pamoja na Chimala,Mswiswi na Igurusi.Kwakuwa ilikuwa msimu wa kiangazi ilimshangaza Mwalimu.

Baada ya kuuliza wenyeji na kuambiwa kulikuwa na bonde lililo na maji mengi aliomba apelekwe kulitembelea na ndipo akawaomba wakazi wa kijiji cha Kapunga watoe eneo hilo kwa serikali.

Mwaka 2012 nilizungumza na aliyekuwa Mwenyekiti wa kijiji cha Kapunga Ramadhan Nyoni aliyesema wanaKapunga walikubaliana na ombi hilo hasa baada ya kuelezwa manufaa ambayo wangenufaika kwa serikali kuliboresha eneo hilo kwaajili ya kilimo cha umwagiliaji.Zao lililopendekezwa kulimwa kwenye bonde hilo ni mpunga.

Jitihada za kujenga miundombinu ndani ya shamba hilo lenye hekta 5,500 zilianza kwa serikali kuomba mkopo Benki ya Dunia(WB).Lakini WB ilitoa sharti kwa serikali kuhakikisha pia inaboresha eneo la hekta 800 kwa wakulima wadogo waliotoa ardhi yao.

“Hapo ndipo ukafikiwa uamuzi wa hekta 5,500 za serikali ziwe mashariki na hekta 800 za wakulima wadogo ziwe magharibi na katikati eneo la kijiji cha Kapunga lenye hekta 1070.”alisema Nyoni na kuendelea

“Savei iliyofanyika ilihusisha maeneo yote matatu kwa maana ya eneo lililo na jumla ya hekta 7,370.Na katika mambo tuliyokuwa tumeahidiwa ni pamoja na serikali kukijenga kijiji chetu na kuwa cha mfano nchini”

“Serikali katika kujenga mradi kwenye eneo lake kupitia shirika la Nafco haikumaliza wote.Hekta 500 ndizo ziliandaliwa kwaajili ya kilimo.500 zilitumika kwa ujenzi wa makazi ya Nafco,kiwanda na karakana na 2000 zikaachwa”

Baadaye Nafco ilishindwa kuliendesha shamba hilo na hatimaye serikali ikaamua kuliuza kwa mwekezaji.Matangazo ya kuuza shamba hilo yalionesha hekta 5500.

Baadaye serikali ilimpata mwekezaji na kumkabidhi shamba hilo.Kinyume na matangazo ya kumtafuta mwekezaji mkataba uliongiwa kati ya serikali na kampuni ya Expot Trading Limited unaonesha jummla ya hekta 7,370.

Mkataba huo ulisainiwa agosti 17 mwaka 2006.Katika mkataba huo,inaonekana serikali iliwakilishwa na  mhandisi mkazi wa wizara ya Kilimo,Chakula na Ushirika Rosemary Tesha na kampuni ya Expot Trading Limited ikawakilishwa na Sunil Kumar kutia sahihi.

“Maswali tunayojiuliza wana Kapunga ni kwamba kama serikali ilituomba hekta 5,500 za ardhi,tukaipa hekta hizo na matangazo ya kutafuta mwekezaji yakamaanisha hekta hizo huo mkataba ulioingiwa kati ya serikali na mwekezaji unaoonesha hekta 7370 unatoka wapi?”

“Ina maana serikali iliamua kuuza mpaka ardhi ya wananchi walioikaribisha na kuipa eneo.Hili limekuwa mgogoro wa muda mrefu kati yetu na mwekezaji kwakuwa madai yake anasimamia mkataba hivyo uwepo wetu sisi na shamba letu la wakulima wadogo hautambui”

Mwenyekiti huyo wa kijiji cha Kapunga wakati huo alisema umefika wakati wakazi wa kijiji hicho wanajuta kwa kukubali ombi la mwalimu Nyerere la kumpa ardhi.Anasema badala ya matarajio waliyokuwa nayo wakati huo sasa wanavuna mateso na adhabu ambazo kama wasingetoa ardhi yao wangeendelea kuishi maisha ya furaha siku zote za maisha yao.

“Wakati tunaombwa shamba tuliahidiwa mambo mengi sana yaliyotuvutia.Tuliambiwa kijiji chetu kitakuwa cha mfano maana tungejengewa shule ya kisasa,kuletewa umeme na pia watoto wetu wangepata ajira kutoka katika shamba tulilotoa”

“Wakati wa Nafco tulianza kuona mwelekeo wa kutekelezwa kwa ahadi tulizopewa.Maana tuliletewa maji kijijini kwetu na tukawa tunayatumia kwa matumizi yote.Badaa ya kuingia mwekezaji alikata huduma hiyo na kutoa sababu nyingi”

“Ndoto ya kuwa na kijiji cha mfano iliondoka mara tu baada ya mwekezaji kuuziwa shamba.Hapo usemi wa baadhi ya viongozi akiwemo Juma Ngasongwa na mwenzake Joseph Mungai waliosema mkae mkao wa kula walipokuwa wanamkabidhi shamba mwekezaji tukaona ulimaanisha mkae mkao wa kufa.Maana badala ya kutujengewa shule ya kisasa alithubutu hata kuleta kijiko kikavunja tofali za tanuli mbili tulizokuwa tumechoma tukilenga kujenga shule yetu wenyewe.”  

Baada ya kuvunja tanuli hizo mwekezaji huyo alizigeukia baadhi ya nyumba za wakazi na kuzichoma kisha akajenga uwanja wa ndege kwenye eneo hilo.Anasema alianza kwa kuweka mabango kwenye makazi ya kaya 18 kabla ya kuzichoma moto na wakazi hao wakalazimika kuishi chini ya miti.Badaye aling’oa madaraja na kukataza wakijiji kukatisha ndani ya eneo laki wanapokwenda mashambani mwao.

Anasema badala ya ushirikiano kati ya watumishi wa Nafco na wakazi kijijini hapo ikaonekana sasa viendo vya unyanyasaji,udhalilishaji na kukomoana.Vitendo hivyo ni pamoja na mifugo kukamatwa na kutozwa faini ya shilingi 20,000 kila mmoja walipokutwa ndani ya eneo la mwekezaji.Na wafugaji walipoomba stakabadhi ya malipo hayo wakapewa ya Nafco na si kampuni ya sasa.

Nyoni anafafanua kuwa matukio ya mwekezaji huyo yapo mengi yanayowanyiam raha wakazi hao lakini tatizo ni kutofahamika kwa mpaka halisi.Lipo pia tukio la Julai 10,2011 ambapo mfanyakazi wa kampuni hiyo alimgonga kwa gari mfugaji Mwiguru Nguru na kumchana msamba kabla ya kumpiga ng’ombe mmoja risasi.

Mzee Willium Joram Kasekwa (72) ni miongoni mwa wakazi wa kijiji hicho walioshiriki mchakato wa kuikabidhi serikali eneo la shamba la Kapunga.Anaikumbuka sana siku alipokuja mwalimu Nyerere kuja kutia baraka katika shamba hilo.

“Akimaanisha ushirikiano kati ya serikali na wananchi alizindua shamba la wakulima wadogo kwa kupanda miche kadhaa ya mpunga katika shamba langu.Ulikuwa mwaka 1966 alipokuja na aliongozana na mkewe mama Maria pamoja na mwanamke mwingine aliitwa Bibi Titi”

Wazee wengine Zebrone Gaone Mbila na Elbaut Mwinuka pia nilipozungumza nao mwaka 2012 walionesha kukumbuka busara za Mwalimu Nyerere alizozionesha na kuwahakikisha maisha bora kwa kutoa kwao shamba kwa serikali.

Lakini wakasema wema wao umewasababishia sasa familia zao kuishi kama mkimbizini.Baada matukio ya mwekezaji katika shamba hilo hayaishi na kila kukicha anasisitiza kuwa kijiji cha Kapunga pamoja na mashamba ya wakulima wadogo ni eneo lake hivyo wakazi wanapaswa kuondoka.

Jitihada mbalimbali zilifanywa na wakazi wa kijiji hicho wakati huo lakini mara kadhaa ziligonga mwamba.Moja ya jitihada hizo ni pamoja na barua ya Februari 5 mwaka 2007 waliyomwandikia rais Jakaya Kikwete kuomba awasaidie kutatua mgogoro wa mpaka kati ya kijiji na mwekezaji lakini walise haikujibiwa.

Walisema maendeleo katika kijiji hicho yalikwama tangu mwaka 2006 kwakuwa walibakia kuishi mguu mmoja nje mguu mwingine ndani.Wanailalamikia sera ya ubinafsishaji wakisema imeleta mateso makubwa kwao na kutamani Mwalimu Nyerere kurudi duniani ili awarejeshee ardhi yao.

Kwa wakati huo,Uongozi wa wilaya ya Mbarali kupitia ofisi ya mkuu wa wilaya ulikiri kuwa mgogoro wa kimpaka kati ya kijiji cha Kapunga na mwekezaji ni pasua kichwa unakwamisha kwa kiasi kikubwa maendeleo ya kijiji hicho.

.........................ITAENDELEA KESHO ........................

No comments:

Post a Comment