Na Joachim Nyambo.
“Kaulimbiu ya Hapa Kazi Tu inatukumbusha kaulimbiu
za huko nyuma kama vile Uhuru na kazi,Uhuru ni kazi na Heshima ya mtu
kazi” Ni kauli ya Mwenyekiti wa wazee
wastaafu wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Mbeya,Isakwisa Mwambulukutu wakati wazee
hao walipotoa tamko la kupongeza utendaji kazi wa rais John Magufuli.
Tamko hilo liliungwa mkono na wazee wengine
wanachama wa umoja huo wakiwemo Edward Ndonde,Daniel Fussi,Kikeke A
Kikeke,Rogate Masuba,John Mushi,Bujo Mwakatumbula,Joji Nyirenda,Boniface
Kasyunguti,Philimon Mwansasu na mmoja wa waasisi wa TANU mkoani Mbeya,Helena
Mwaipasi.
“Sisi wazee tunaounda umoja wa Wazee wa CCM
tunaoishi jijini Mbeya kwa niaba ya wazee wenzetu tunapenda kutoa tamko rasmi
la kumpongeza rais John Magufuli kwa utekelezaji wake mzuri wa Ilani yetu ya
CCM ya uchaguzi ya mwaka 2015 na utendaji wake mzuri wa kazi katika awamu hii
ya tano ya serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania”alisema Mzee Mwambulukutu.
“Tunapotoa tamko la kumpongeza Dk.Magufuli
isieleweke kuwa tunaziona awamu nyingine zilizotangulia hazikufanya
mazuri,lahasha.Kama alivyosema aliyekuwa rais wa awamu ya pili Alhaji Ali
Hassan Mwinyi kuwa Kila zama na Kitabu chake,viongozi wa awamu zilizotangulia
kila mmoja alifanya mambo kwa kadiri ya karama aliyojaliwa na Mwenyezi Mungu
kulingana na hali halisi ya wakati wake huo.Hara Dk Magufuli ni moja ya matunda
ya awamu hizo zilizotangulia”anasema.
Mwenyekiti huyu anasema ni Ukweli usiopingika kuwa
maendeleo ya mtu au Taifa kwa ujumla hayawezi kupatikana kama watu hawataki
kufanya kazi.Ni jambo la kumpongeza rais kwa kuhimiza hilo na anapaswa
alisimamie kwa nguvu zote ili nchi iweze kujikwamua kutokana na lindi la
umasikini.
Wazee hawa wanasema sababu ya pili ya kumpongeza
rais ni Kuimarisha nidhamu na uwajibikaji wa watumishi wa umma.Watumishi wengi
wa umma walifikia mahali ambapo walifanya kazi kwa kadiri ya matakwa yao bila
kujali taratibu na kanuni za kazi.
“Walisahau ile kauli mbiu aliyotoa rais Ally Hassan
Mwinyi isemayo,Usipowajibuka,Ole Wako,Utakumbana na Fagio la Chuma.Sisi wazee
tunaamini Magufuli ni fagio la Chuma,kwani matokeo tumeanza kuyaona kwenye
sehemu ambazo huduma hutolewa kama vile hospitali,ofisi za serikali na sehemu
nyinginezo.”
Sababu ya Tatu ni Kupambana na rushwa,ukwepaji kodi
na ubadhirifu wa mali za Umma.Anasema Kwa kwa Kutumbua Majipu,Dk.Magufuli
anawakumbusha enzi za Hayati Edward Moringe Sokoine alipopambana na Wahujumu
Uchumi.
“Sisi wazee tunamwombea rais Magufuli Mungu
amlinde,ili atumbue majipu yote,vipele,chunusi na kukwangua kabisa ukurutu ili
Tanzania yetu ibaki safi na yenye afya njema kiuchumi na kiustawi wa jamii”
Kuboresha huduma za jamii ili kuleta hali nafuu ya
maisha ya watanzania ni sababu ya nne wanayoitaja wazee hawa kuwasukuma kutoa
pongezi zao.Hii ni pamoja na kuboresha huduma hospitalini,kutoa elimu bure toka
chekechea hadi kidato cha nne na kuhakikisha mikopo inapatikana kirahisi kwa
vijana wa elimu ya juu.
“Kwa kuendelea kuboresha miundombinu ya
barabara,reli,umeme,maji na mingine mingi hapa anatukumbusha usemi wa It can be
done play your part.Hivyo tunatoa wito kwa watanzania wenzetu kutimiza wajibu
wao pale walipo ili huduma za kijamii ziweze kuwa bora na kutufanya wote tuwe
na maisha nafuu”.
Kufufua na kuhimiza ujenzi wa viwanda ili kuongeza
ajira,kuongeza thamani ya mazao yatokanayo na Kilimo,uvuvi na Ufugaji na kuinua
uchumi wa Taifa pia limewakosha wazee hawa.Wanasema wameanza kuona matunda
kwani mkoni Mbeya tayari kiwanda cha Zana Za Kilimo(ZZK) kimeanza kufanya kazi
na baadhi ya vijana wamepata ajira.
“Hapa tukizingatia ile kaulimbiu ya Kupanga ni
Kuchagua hakuna kitakachoshindikana.Hivyo tunaomba juhudi ziendelee ili kufufua
viwanda vingine kama vile HISoap,kiwanda cha nguo na kiwanda cha kusindika
nyama”
Jambo jingine ni Kuboresha na maslahi ya wafanyakazi
kwa kuanza na kupunguza kodi itokanayo na mishahara yao kutoka asilimia 11 hadi
asilimia tisa.Wanasema wanaamini kutokana na Kutumbua Majipu,kudhibiti wafanyakazi
hewa na madeni hewa hali ya kiuchumi itakuwa bora na hivyo kuwezesha kuongezeka
kwa mishahara ya wafanyakazi na huduma bora kwa umma zitapatikana.
“Jambo ji ngine ni kuhimiza ujenzi wa Taifa
linalojitegemea.Ile kauli ya rais Magufuli ya Bora kushindia mihogo,kuliko
mkate wa Siagi wa masimango unatukumbusha kauli ya Baba wa Taifa Hayati Julius
Nyerere ya Heri kuwa masikini na Huru,Kuliko kuwa Tajiri na Mtumwa”
“Sisi wazee tunamwomba rais wetu akaze uzi wala
asijali vitisho vya wafadhili wanafiki na maneno ya Wanasiasa Uchwara.Tunaamini
pia kwa kubana matumizi ya serikali kwa kupunguza safari za nje ya nchi,posho
za vikao visivyo na tija kwa taifa letu na kupunguza sherehe zinazomaliza fedha
nyingi nchi yetu itaweza kujikwamua kiuchumi na hatimaye kuweza kujitegemea”
Wazee hawa wanasema unyenyekevu aliouonyesha
Dk.Magufuli wakati wa kuzindua Daraja la Kigamboni ni wa kipekee.Pamoja na
kwamba usimamizi wa ujenzi wa daraja hilo ulikuwa chini yake tangu alipokuwa
Waziri wa Ujenzi,alikataa daraja hilo kuitwa jina lake na badala yake aliamua
liitwe Daraja la Nyerere,kwa kumuenzi Baba wa Taifa kwa kuimarisha umoja wa
Kitaifa na kupigania Uhuru wa Bara la Africa.
Mzee Mwambulukutu anasema Kudhibiti uagizwaji holela
wa sukari toka nje ya nchi ili kuhakikisha watanzania wanapata sukari iliyo
salama na kwa bei nafuu na pia kukuza viwanda vya sukari vya hapa
nchini,inastahili pongezi.Pamoja na purukushani za hapa na pale zinazofanywa na
wafanyabiashara wasio na Uzalendo wanaamini juhudi za Rais zitashinda kwakuwa
Palipo na Mwanga,giza hujitenga.
“Jambo la mwisho ni kudhibiti hali ya ulinzi na
usalama visiwani Zanzibar na hivyo kufanikisha uchaguzi wa marudio bila
fujo.Akiwa Amirijeshi Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,aliweza
kuhakikisha ulinzi na usalamakatika visiwa vya Zanzibar unakuwepo na hivyo kuwezesha
uchaguzi wa marudio kufanyika hapo Machi 20 mwaka hu bila vurugu zozote.”
“Sisi wazee tunampongeza kwa hilo na tunapongeza
ushindi wa kishindo wa CCM katika uchaguzi huo,uliofanyika kwa amani na
utulivu”alisema Mzee Mwambulukutu.
Wazee wengine akiwemo Kikeke A Kikeke,wanasema
juhudi na ushirikiano wa pamoja baina ya watanzania wote pasipokujali nafasi
waliyonayo ndiyo utakaowezesha mikakati mbalimbali ya Dk.Magufuli
kufanikiwa.iwapo kutakuwepo na makundi ya watu wanayojitenga na kukwamisha itakuwa
vigumu kwake kuwezesha watanzania kupiga hatua kimaendeleo.
Kwa upande wa katibu wa umoja huo Philimon
Mwansasu,alisema watanzania wanapaswa kutambua kuwa maisha bora hayawezi
kupatikana kama taifa litabakia mikononi mwa matajiri wachache wenye kupenda
kulimbikiza mali kwaajili yao na familia zao na kuwaacha masikini wakiwa
watumwa ndani ya taifa lao.
“Tunachopaswa kufanya watanzania wote ni kushirikia
katika mipango ya rais kuhakikisha tunafichua maovu yote yanayofanywa na
watendaji wabovu.Kuchukuliwa kwao hatua ndiyo mwanzo wa walalahoi kupata unafuu
wa ugumu wa maisha.Tukisema tushirikiane na wahalifu kwa madai kuwa tunawaonea
huruma tutakuwa tunazidi kujikwamisha wenyewe”anasema Mwansasu.
Mwisho.
No comments:
Post a Comment