Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Wednesday, June 26, 2024

CHUNYA WAJIZATITI KEN GOLD KUCHEZA NYUMBANI LIGI KUU

 


Na Mwandishi Wetu, Chunya.

 

HALIMASHAURI ya Wilaya ya Chunya Mkoani Mbeya imewahakikishia wapenzi wa soka kuwa michezo ya Timu ya Ken Gold iliyopanda ligi kuu wataishuhudia kwenye uwanja uliopo  wilayani hapa kwakuwa mikakati imewekwa kuhakikisha ujenzi wa uwanja huo unakamilika kwa wakati.

 

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mtendaji wa Halimashauri ya Wilaya ya Chunya, Tamim Kambona tayari Shilingi milioni 200 imeytengwa na halimashauri hiyo kwaajili ya muendelezo wa ujenzi wa uwanja huo wa michezo uliopo katika Kata ya Mbugani.

 

Akizungumza na mwandishi wetu, Kambona alisema lengo la halimashauri ni kuona mradi wa ujenzi wa uwanja wa michezo uliopo Kata ya Mbugani unaomilikiwa na Halmashauri hiyo unakamilika kwa wakati kabla ya kuanza kwa ligi Kuu mwaka 2024/2025.

 

Alisema wanao uhakika Ken Gold itautumia uwanja huo kwa mechi zake za nyumbani kwakuwa mbali ya kutenga fedha hiyo kupitia mapato yake ya ndani pia imeunda Kamati maalumu ya wadau inayoongozwa na Ayoub Omary ili kusimamia kwa karibu mradi huo.

 

Kambona alisema sanjari na mipango ya Kamati Halmashauri inatarajia kutenga fedha nyingi zaidi mwaka ujao wa fedha ili kuuboresha zaidi uwanja huo na kuwa wa kisasa kwa kuwekwa nyasi bandia.

 

Mkurugenzi huyo pia aliwashukuru wadau wanaoendelea kutoa michango ya hali na mali akiwemo mwekezaji kwenye Sekta ya Madini aliyemtaja kwa jina la David Mathayo aliyesema ametoa tingatinga kwa ajili ya kushindilia uwanja.

 

Aliwataka wadau wengine kuunga juhudi zinazofanywa na halimashauri ili kuhakikisha uwanja unakamilika kabla ya mashindano ambapo wananchi wataongeza mapato yao kutokana na ujio wa wageni kutoka nje ya Wilaya na Mkoa kwa ujumla.

 

Mmoja wa wafanyabiashara na mkazi wa Kata ya Chokaa wilayani hapa, Boniphace Mwinuka alisema hatua ya kupanda daraja kwa timu ya Ken Gold inaleta hamasa kubwa ya michezo katika Wilaya ya Chunya kwani wengi wa wakazi walikuwa wakisafiri kwenda jijini Mbeya ili kushuhudia michezo ya ligi kuu.

 

Mwinuka alisema miongoni mwa faida zitakazopatikana kwa wakazi wilayani hapa iwapo ligi kuu itacheza kwenye uwanja huo ni pamoja na wafanyabiashara wa nyumba za kulala wageni kupokea wageni wengi pamoja na wajasiriamali na madereva wa Bodaboda kusafirisha abiria kutoka maeneo mbalimbali.

No comments:

Post a Comment