Friday, April 15, 2016
Wednesday, April 13, 2016
Tuesday, April 12, 2016
Msaada MCC sawa na Unga usio nyumbani mwako!
Na Joachim Nyambo.
UNGA usio nyumbani mwako ni sawa na Majivu!Ni
usemi wautumiao watu wa kabila la wafipa kutoka mkoani Rukwa ambao kwa lugha
yao husema “Usu usi ung’anda umwako Itwi!
Maana ya Usemi huu ni kuwa kitu chcochote
japo kiwe na uzuri wa namna gani,kama unakipata kutoka kwa jirani haupaswi
kukitegemea kwa asilimia 100.Ukiwekeza matumaini yote ya kukipata kila siku
basi utambue kuwa ipo siku utaadhirika.
Maana ya usemu huu hautofautiani na
kinachoonekana kati ya Tanzania na Shirika la Marekani la Changamoto za
Milenia(MCC).Ni kwa miaka kadhaa Shirika hili limekuwa likiisaidia Tanzania
fedha kwaajili ya kuendesha miradi mbalimbali ya kimaendeleo.Miongoni mwa
miradi iliyotekelezwa na fedha kutoka MCC ni pamoja na barabara ya
Tunduma-Sumbawanga na pia miradi ya Umeme vijijini.
Hivi karibuni
MCC imetangaza kusitisha msaada wa Dola za Marekani milioni 473 sawa na
shilingi Trilioni moja kwa serikali ya Tanzania.Shirika hilo limezuia fedha
hizo za maendeleo kutokana na Tanzania
kuitisha Uchaguzi wa marudio Zanzibar pamoja na kutumika kwa Sheria ya makosa
ya Mitandao.
Chini ya Mpango wa Uwekezaji wa MCC-2,fedha
hizo zilikuwa ziende katika kuboresha huduma za umeme,ikiwemo usambazaji wa
nishati hiyo katika vijiji vingine zaidi nchini.Kupitia MCC Tanzania imeweza
kupiga hatua katika matumizi ya umeme kutoka asilimia 10 ya wakazi mwaka 2005
hadi asilimia 46.Ongezeko hilo la matumizi ya umeme kwa watanzania sehemu kubwa
limetokana na MCC-1.
Katika awamu ya kwanza Tanzania ilipokea
kiasi cha Dola za Marekani milioni 698 ambazo zilitumika kwa ujenzi wa barabara
za Tunduma-Sumbawanga,Tanga- Horohoro,Namtumbo-Songea hadi Mbinga.
Fedha hizo pia zilitumika kujenga upya mfumo wa
huduma za maji kwaajili ya miji ya Dar es salaam na Morogoro na pia kusambaza
umeme katika vijiji vya mikoa 10 ya Tanzania bara.Zilitumika pia kutandaza njia
ya pili ya kusafirisha umeme chini ya Bahari ya Hindi kati ya Bara na Tanzania
visiwani na pia kujenga barabara zote kuu za Kisiwa cha Pemba na baadhi ya
barabara za Unguja kwa kiwango cha lami.
Ukweli ni kuwa msaada huu ulikuwa muhimu na
umeleta mabadiliko makubwa nchini.Kuboreshwa kwa barabara katika maeneo
yaliyokuwa yamesahaulika kamaa ile ya Tunduma-Sumbawanga kumefunguwa fursa
nyingi za kimaendeleo.Ni wazi kwa mwananchi kama mkazi wa Rukwa unapomweleza
suala la MCC kusitisha kuleta fedha nchini atasikitika kwakuwa ni mnufaika wa
moja kwa moja.
Lakini fedha hizi ukweli si za watanzania.Ni
sawa na unga wa kuomba kwa jirani.Hauwezi ukaupangia bajeti huku ukiwa na
uhakika wa asilimia zote.Hata kama una imani na jirani anayekupa unga huo ni
lazima pia ujue anakupa kutokana na kufurahi kwake,au kutosheka kwake.Siku
akiona haukumfurahisha au unga wake hautoshelezi ni wazi atabadili mawazo.
Uamuzi huo wa jirani MCC kujiondoa katika
miradi aliyokuwa akiifadhili Tanzania ni fundisho tosha kwa watanzania katika
vita yao ya kukabili umasikini na kujiletea maendeleo.Msaada wa unga wa jirani
sasa umekuwa majivu na yawapasa watanzania kutafuta unga wao ili wasijikute
wanakula majivu.
Kukatishwa kwa msaada huu kumeonekana kuwa
gumzo kubwa ndani na nje ya Tanzania.Wadau mbalimbali wameonekana kuwa na
michango tofauti ya kimawazo juu ya uamuzi huu.Mitandayo ya kijamii imejaa maoni
mbalimbali ya wachangiaji juu ya hoja hii.Wapo wanaoonesha woga wakisema sasa
Tanzania itakuwa kwenye wakati mgumu na wapo wale wanaosema ni wakati wa
kujipanga.
Lakini maamuzi haya ya MCC yanakuja wakati
serikali ya Tanzania chini ya rais Dk John Magufuli ikichukua hatua mbalimbali
katika kuimarisha uchumi ili kuweza kuondokana na kutembeza bakuli na kuitwa
ombaomba kwa mataifa wahisani.Tayari watanzani wameshuhudia jitihada kadhaa
zinazofanywa na serikali ya Dk Magufuli katika kuimarisha uchumi wa taifa lao.
Miongoni mwa ambao yaliyokwishafanyika ni
pamoja na udhibiti wa mapato katika bandari kuu ya Dar es salaam,Ufuatiliaji wa
malipo halali ya kodi sambamba na kuokoa fedha zilizokuwa zikipotea kwa kulipa
mishahara wafanyakazi hewa.
Katika gazeti la habarileo la Machi 30 mwaka
huu,Waziri wa Fedha na Mipango,Dk Phillip Mpango alikaririwa akisema serikali
haishaangazwi na uamuzi wa MCC kwakuwa dalili zilikwishaanza kuonekana tangu
Desemba mwaka jana.
“Tangu Desemba mwaka jana tulishasoma alama
za nyakati na ndiyo sababu hatukuzijumuisha fedha za MCC-2 katika maandalizi ya
Bajeti ya Serikali yanayoendelea kwa mwaka ujao wa fedha.”
“Tulisoma kwenye mitandao matamshi ya
viongozi wa mfuko huo ndiyo maana tukaamua kutozijumuisha fedha za MCC kwenye
bajeti ya mwaka ujao wa fedha,hivyo watanzania wasiwe na wasiwasi juu ya
kusitishwa kwa msaada huo”alikaririwa Dk Mpango.
Rais Dk Magufuli hata kabla ya kusitishwa kwa
fedha za MCC amekuwa akikaririwa mara kadhaa na vyombo vya habari akihimiza
matumizi sahihi ya rasilimali zilizopo Tanzania pamoja na kila mwananchi
kuwajibika katika kutoa kodi.
"Kila mmoja akifanya kazi, nchi
haitahitaji wala kubembeleza misaada ya masharti kutoka nje kwa kuwa ni yenye
neema, ina kila kitu na ikisimama imara na kila
mmoja akatimiza wajibu wake, itakuwa ni nchi inayotoa msaada kwa nchi nyingine
duniani". Anasema Dk Magufuli.
Dk Magufuli hatoi
kauli hii baada ya kuingia madarakani tu.Hta wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu
uliomuingiza madarakani wa mwaka 2015 alikuwa akiyasema hayo.Alisikika mara
nyingi akiwaambia wapiga kura kuwa kinachokosekana kwa Tanzania ni usimamizi
imara wa rasilimali zilizopo.
Lakini pia kwa
miaka kadhaa wanasiasa wakiwemo wa vyama vya upinzani wamekuwa wakilalamikia
mfumo wa usimamizi rasilimali wakisema ndiyo unaosababisha Tanzania kubakia
ombaomba.Miongoni mwa vyama ambavyo viongozi wake wamekuwa wakililia mfumo wa
usimamizi rasilimali ni Chama cha Demokrasia na Maendeleo(Chadema).
"Nchi hii tajiri sana lakini kutwa kucha
kulialia msaada MCC millenium, watanzania leo hawapati umeme hadi tukaombe MCC
wamekuwa wabunge kwetu? Ichaguenu Chadema hatutategemea wafadhili na masharti
yao tutajenga nchi ya kujitegemea" yalikuwa maneno katika hotuba ya
mwenyekiti wa Chadema Freeman Mbowe baliyoitoa kwenye mkutano wa kampeni za
uchaguzi mkuu Septemba 13,2015 katika Uwanja wa
Nzega mkoani Tabora.
Kusitishwa kwa msaada huu wa wamarekani
kunapaswa kuipa fundisho pia Tanzania kuwa taifa kubwa kama Marekani lina
malengo yake hata linapokupa msaada.Wakati mwingine malengo yake yanaweza
yasiendane na mipangilio ya Taifa linalopewa msaada na ndiyo sababu muasisi wa
taifa Mwalimu Julius Nyerere alionya kuwepo na umakini katika kupokea misaada
ya mataifa kama Marekani.
“Siku wamarekani wakinisifia nimefanya kazi
nzuri nitajiuliza kuwa nimekosea wapi!" aliwahi kutamka Mwalimu Nyerere
katika moja ya mikutano.
Kwa kauli ya mwalimu Nyerere kuna haja kwa
Mtaifa yanayoendelea kupanua wigo wa fursa ya wadau wa kimaendeleo badala ya
kusalia kwa taifa moja ambalo kila nchi change inaliangalia na kupiga magoti.Tanzania
inapaswa kupongezwa kutokana na kuonesha nia ya kuanza kushirikiana na nchi
kama Japani,China na Vietnam.
Mwisho.
Subscribe to:
Posts (Atom)