Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Tuesday, September 20, 2016

Ofisi ya Madini Chunya na mchango wake katika sekta ya Madini.

Na Joachim Nyambo.

OFISI ya Madini Chunya kwa sasa inahudumia eneo lote la wilaya za Chunya mkoa wa Mbeya na Songwe mkoani Songwe.Huduma ni pamoja na Utafiti,uchimbaji na biashara ya madini.

Kwa mujibu wa Kaimu Afisa Madini Mkazi wa wilaya ya Chunya Ndege Bilagi,Ofisi ina jumla ya watumishi 12 wanaogawanyika katika kada za mhandisi wa migodi mmoja,mjiolojia mmoja,Fundi sanifu mmoja,mhasibu mmoja,madereva watatu,walinzi watatu,mwangalizi wa ofisi mmoja na katibu mhitasi mmoja.Watumishi wane kati ya hao ni wa mkataba.

Ofisi hii inafanya kazi za Idara ya Madini iliyo chini ya wizara ya nishati na Madini,inatoa taarifa yake ofisi ya madini Kanda iliyopo jijini Mbeya.Pia inatoa taarifa katika taasisi nyingine za serikali ikiwa ni pamoja na ofisi ya mkuu wa wilaya juu ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za ofisi.

Ofisi inashirikiana na Halmashauri katika kutekeleza majukumu yake kwani shughuli nyingi za uchimbaji zinaingiliana na matumizi mengine ya rasilimali kama maji,misitu na ardhi.

“Baadhi ya shughuli zinazosimamiwa na ofisi ni pamoja na Kusimamia na kuratibu mfumo wa leseni wa Online Mining Cadastre Transaction Portal(OMCTP) kwa watumiaji wa leseni ikiwemo kuwasajiri,kuwafundisha wachimbaji au wateja namna ya kuomba na kuingiza maombi ya leseni kwa kutumia akaunti zao za barua pepe”anasema  Bilagi.

Shughuli nyingine ni Kusimamia uchimbaji wa awali(mdogo) wa madini ikiwa ni pamoja na kutoa huduma za ugani(Extension Service) kwa wachimbaji wadogo.Kukagua usalama wa maeneo ya wachimbaji wadogo na wakubwa na Kutoa elimua ya uhifadhi wa mazingira kwa wachimbaji wadogo,wa kati na wakubwa.

Nyingine ni kutoa elimu kuhusiana na matumizi ya baruti na kusimamia au kuhakikisha kuwa sheria na matumizi ya baruti vinatekelezwa kwa ufasaha.Kukusanya Maduhuli ya aina mbalimbali ya serikali yatokanayo na shughuli mbalimbali za madini.

“Ofisi pia ainawajibika kukagua shughuli za utafiti wa madini zinazofanywa na wenye leseni kubwa za utafiti wa madini(prospecting licenses),kupokea taarifa za robo mwaka kutoka kwa watafiti madini wenye leseni kubwa na kuzioanisha ili kubaini kama taarifa hizo zinaendana na kazi iliyofanyika katika leseni husika”

“Kuna kusimamia shughuli za uchimbaji mkubwa ili kubaini kama Sheria na kanuni zinafuatwa.Kufanya ukaguzi wa shughuli zote za uchimbaji kwa lengo la kubaini ukiukwaji wa sheria,Kutoa vibali vya kusafirisha madini na sampuli zenye madini nje na ndani ya nchi na pia Kutoa vibali vya kuagiza Baruti,kukagua maghala ya kutunzia baruti”

“Kwa kifupi tunasimamia Sheria ya Madini ya mwaka 2010,sheria ya Baruti ya mwaka 1963 pamoja na Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004” anasema Bilagi.

Uchimbaji mdogo wa madini

Bilagi anasema,Uchimbaji mdogo wa madini unafanywa na watanzania pekee ambao lazima wawe na leseni za awali za uchimbaji zijulikanazo kama Primary Mining Licenses(PMLs).Katika wilaya ya Chunya uchimbaji huu unafanyika katika maeneo yaliyogawanywa kwenye kanda.

Kanda ya Makongolosi kuna maeneo ya Mkola,Mapele,Gepu,Ujerumani,Chipoka na Kilombero wakati Kanda ya Matundani vipo vituo vya Kasisi,Kasakalawe,Itumbi Jeshini,Jobu Iti,Makatang’ombe,Idundu na Bwawani.

Kanda ya Chunya kuna maeneo ya Sinjili,Mlima Yasini,Mapogolo,Kiwanja,Mbugani,Itumba,Godima,Simba Reef,Simbachai,Safari Mine,Saitunduma,Simbadume,Majengo,Isenyela,Chalangwa,Nyatula,Mlimanjiwa,Kasanga Madini,Kasanga Market,Soweto na Mamusapu.

Maeneo mengine kwenye ukanda huu ni Mapapai,Ifumbo,Chikula,Kisu Mine,Magamba,Makoma,Mawelo,Mnyolima,Mwankonyonto,Shoga,Legezamwendo,Ilepuka,Chokaa,Mapunga,Majengo,Ihamba,Tukuyu,Sangambi,Izumbi na Kikavu.

Anasema wilaya za Chunya na Songwe zina wachimbaji wadogo wenye leseni za PMLs zipatazo 729.

Utafutaji wa Madini

Anasema Shughuli za Utafutaji wa madini zinafanyika kwenye leseni zinazojulikana kama Prospecting Licences(PL) katika  maeneo yote ya wilaya ya Chunya ili kubaini uwezekano wa kupata mashapo makubwa ya madini.

Ukanda huu wa madini unajulikana kwa jina la kijiolojia kama Lupa Gold Fields ambao una madini ya dhahabu na madini mengine ya Metali yaani Shaba,fedha,galena,chuma na mengineyo.Nje ya ukanda wa Lupa Goldfields kuna madini mengine kama rare earth elements(Metals),Magadi(Soda ash),madini ya vito na mengineyo.Wilaya hizi mbili zina jumla ya leseni za utafutaji madini 179.

“Kuna kituo cha Kufundishia wachimbaji wadogo cha Matundasi ASM kilichoanzishwa na serikali mwakaa 2005 ili kutoa elimu kwa vitendo kwa wachimbaji wadogo.Kituo hiki kipo eneo la Matundasi ambapo mwaka 2008 kilibinafsishwa kwa mwekezaji kwa makubaliano na serikali ili akiendeleze. Kwa sasa mradi huo unaendelea na shughuli za uchorongaji miamba ili kubaini mashapo yatakayoweza kuanzisha mgodi darasa”anasema.

Uchimbaji Mkubwa

Uchimbaji mkubwa unafanyika katika maeneo mbalimbali na kuna leseni zipatazo tano katika eneo linalisimamiwa na Ofisi hii ya Madini ya Chunya.Kwa eneo la wilaya ya Chunya pekee kuna uchimbaji mkubwa unafanyika eneo la kata ya Matundasi ambapo kampuni ya Sunshine Mining Co Limited yenye leseni ya ucjenjuaji(processing licence) namba 00067/2013 na imeomba Mining Licence kwa maeneo yake mawili.

“Kwa sasa kampuni hii  imesimamisha shughuli zake ili kutengeneza miundombinu ya bwawa la maji machafu(Tailing Storage Facility-TSF).Vilevile tuna wachimbaji wengi wadogo ambao sasa mitaji yao na uchimbaji wao umekuwa kutoka kwa wachimbaji wadogo hadi kufika kuwa wachimbaji wa kati.Mfano ni Aidani Msigwa,Isack Msowoya na Elias Mwembe.”

Uzalishaji Madini na Ulipaji wa Maduhuli ya Serikali

Kwa mujibu wa sheria ya madini,Wachimbaji wakubwa na wadogo wanapaswa kulipa kodi za serikali ambazo ni Ada ya mwaka ya leseni,mrabaha wa asilimia nne kutokana na uzalishaji waa madini,ada za kubeba baruti,ujenzi wa maghala ya kuhifadhia baruti.Hivyo serikali kupata mapato kutokana na tozo hizo ambapo utaratibu ni kuwa fedha zinapaswa kulipwa benki moja kwa moja.

Katika kipindi cha mwaka wa fedha 2010/2011 hadi 2015/2016 Jumla ya Shilingi 1,888,642,319.66 zilikusanywa na Ofisi ya Madini wilayani Chunya ikiwa ni Mrabaha wa asilimia 4 wa madini aina ya dhahabu yaliyochimbwa na wachimbaji wadogo wilayani hapa katika kipindi hicho.

Bilagi anasema katika kipindi hicho Jumla ya Gramu 821,113.16 za dhahabu zenye thamani ya jumla ya Shilingi 47,216,058,041.50 zilizalishwa katika migodi mbalimbali wilayani hapa hivyo kuwezesha serikali kujipatia shilingi 1,888,642,319.66 ikiwa ni mrabaha wa asilimia 4.

Akifafanua zaidi,anasema katika mwaka wa fedha 2010/2011 gramu 11,934.38 zenye thamani ya shilingi 668,325,550 zilizalishwa hivyo serikali ikajipatia mrabaha wa shilingi 26,733,020.

Mwaka wa fedha 2011/2012 gramu 14,693.80 zilizalishwa zikiwa na thamani ya jumla ya shilingi 822,852,600 hivyo serikali ikajipatia shilingi 32,914,104.

Mwaka 2012/2013 zilizalishwa gramu 11,957.93 zenye thamani ya shilingi 669,643,800 hivyo serikali ikapata shilingi 26,785,752 na mwaka wa fedha 2013/2014 zikazalishwa gramu 68,508.93 zenye thamani ya shilingi 3,836,499,900 na serikali ikajipatia shilingi 153,459,996.

Anasema mwaka wa fedha 2014/2015 zilizalishwa gramu 405,587.81 zilizokuwa na thamani ya jumla ya shilingi 22,712,917,481 na serikali ikajipatia shilingi 908,516,699.24 na mwaka 2015/2016 gramu 308,430.31 zilizalishwa zikiwa na thamani ya shilingi 18,505,818,710.50 na hivyo serikali ikajipatia shilingi 740,232,748.42.

Utengaji wa Maeneo kwaajili ya wachimbaji wadogo

Akizungumzia Utengaji wa Maeneo ya Uchimbaji mdogo,Bilagi anasema Wizara ya Nishati na Madini ilitoa eneo la Itumbi B lenye ukubwa wa Kilometa za mraba 12.78 ambapo baada ya kufanyiwa michoro zaidi ya viwanja 300 vilipatikana.

Anasema pia kwa sasa Wizara imetenga maeneo ya Mbugani na Chalangwa na mpango wa kuyagawa maeneo hayo utafanyika mara baada ya Wakala wa Jiolojia Tanzania(GST) atakapofanya kazi ya Utafutaji wa awali ili kubaini uwepo wa mashapo ya madini.

Changamoto zinazoikabili Ofisi
 Kwa mujibu wa Bilagi Ofisi ya Madini Chunya inakabiliwa na changamoto nyingi ambazo kimsingi zinakwamisha utendajikazi.Changamoto hizi ni pamoja na Ukosefu wa rasilimali fedha za kuendesha ofisi.Hii imesababisha kusimama kwa shughuli nyingi za nje ya ofisi(field activities) kama ukaguzi kwa wachimbaji,watafutaji madini,kutoa semina katika vijiji na pia kudhibiti wachimbaji haramu.

Umiliki na matumizi holela ya  Baruti ni changamoto nyingine inayohatarisha maisha ya wachimbaji wadogo wa madini,familia zao na majirani wilayani Chunya.Bilagi anasema baadhi ya wachimbaji wamekuwa wakitunza baruti majumbani mwao,madukani na baadhi husafiri nazo kwenye gari zao.

“Uhifadhi huu holela ni hatari kwa maisha ya wachimbaji hao,familia na majirani zao kwakuwa inaweza kusababisha mlipuko na kuwadhuru watu wanaokuwa jirani”.

Anasema changamoto nyingine iliyopo ni baadhi ya viongozi na watendaji wa serikali za vijiji kuingilia shughuli za ofisi ya madini hasa pale wanapotoa vibali kwa wachimbaji kinyume cha sheria.Baadhi yao wamekuwa wakaidi hata wanapoelimishwa na badala yake wamekuwa wakichochea migomo kwa wananchi ili wasikubali kutii sheria ya madini ya mwaka 2010.

“Tuna changamoto pia ya baadhi ya wanakijiji kujimilikisha maeneo ya kuchimb kwa kisingizio kuwa madini yapo katika mashamba yao.Vile vile hali hii imesababisha baadhi ya wachimbaji wanaomiliki leseni kisheria kushindwa kuchimba maeneo yao kwa kuhofia kufanyiwa vurugu na wenyeji”

 “Bado pia uchimbaji wa kuhama hama unaendelea.Hii inasababishwa na wachimbaji wengi kutokuwa na mitaji ya kutosha ya kufanya utafiti wa kugundua kama maeneo wanayoombea leseni yana mashapo ya madini ya kutosha ili wachimbe” alisema Bilagi.

Kuwepo kwa Utitiri wa kodi na tozo nyingi kwa wachimbaji wadogo nalo linatajwa kama changamoto kubwa.Baadhi ya taasisi zinatoza kodi kubwa zinazoleta manung’uniko kutoka kwa wadau wa shughuli za madini.Mfano watu wanaosaga mawe wanatakiwa kulipa TRA shilingi 700,000 kwa mwaka,wakilipe kijiji kuanzia kiasi cha shilingi 15,000 hadi 20,000 kwa mwezi na wanatakiwa walipe ushuru halmashauri ya wilaya.

Wachenjuaji wanalalamikia kodi ya zimamoto ambapo hadi baadhi yao waliwahi kuwekwa mahabusu wakiamriwa kulipa shilingi 5,000,000 kwa mwaka kama ada ya zimamoto huku wachimbaji wakiwa hawapati huduma yoyote kutoka jeshi hilo.Kero kubwa ni namna taasisi husika inavyoidai kwa njia ya shuruti kabla ya kuwaelimisha.

Bilagi anasema katika kutafuta ufumbuzi wa baadhi ya changamoto,serikali kupitia ofisi ya madini wilaya imeendelea kutoa Elimu kuhusu sheria ya Madini ya mwaka 2010 ili wananchi waweze kutambua kuwa unapomiliki ardhi hauna ruhusa ya kumiliki madini yaliyopo bila kufuata sheria.

Anasema pia Elimu inaendelea kutolewa kwa wananchi na wachimbaji juu ya namna bora ya kumiliki na kutumia baruti kwa mujibu wa Sheria ya Baruti ya mwaka 1963

Afisa huyo anasema Serikali ya awamu ya Tano imedhamiria kuinua hali ya wachimbaji wadogo ili wasiwe wa kuhama hama hivyo imeiwezesha wakala wa Jiolojia Tanzani(GST) ili wafanye utafutaji wa awali wa mashapo yenye madini katyika maeneo mbalimbali nchini na Chunya ikiwa ni miongoni mwa maeneo yaliyopewa kipaumbele.

“Serikali ina mpango wa kujenga kituo kingine cha kutoa elimu kwa wachimbaji wadogo katika kata ya Mbugani ili wawe na weledi wa uchimbaji wenye tija.Tunaendelea kutoa huduma ya kuandikisha wananchi katika mfumo wa leseni wa OMCTP ili kila mchimbaji aweze kuomba leseni bila ya kuwa na ulazima wa kufika ofisi ya madini”

Anasema kuhusu utitiri wa kodi Ofisi ya madini Chunya ilikwisha wasilisha kwa Kamishna wa Madini.

Mkuu wa mkoa wa Mbeya Amos Makalla alipotembelea shughuli za madini na kukutana na wadau wa Sekta hiyo aliahidi kuendelea kupigania haki za wachimbaji wa madini ili kupunguza adha zinazoikabili sekta hiyo wilayani hapa.

No comments:

Post a Comment