Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Monday, September 19, 2016

ELISABENE,SHULE ILIYOANZISHWA KUTOKANA NA MISUKOSUKO YA KIFAMILIA KIELIMU

Na Joachim Nyambo.

“Yapo mambo mengi yaliyonisukuma kuanzisha shule” Ni sentensi aliyoanza nayo Anivene Lusubilo nilipozungumza naye.Huyu ni mmoja wa wakurugenzi wa Shule ya Awali na Msingi ya mchepuo wa kingereza ya Elisabene iliyopo mjini Tunduma wilayani Momba mkoani Songwe.Mkurugenzi mwenza ni mumewe Frank Shitindi.

Ipo historia ndefu kwa familia ya wanandoa hawa hata kufikia hatua ya kuwa na taasisi ya kutoa elimu ambayo sasa imekuwa manufaa kwa jamii pia inayowazunguka na kwingineko nchini nchini.Ni familia yenye watoto wane wote wakiwa ni mabinti.

“Msukumo wa kwanza nilianza kuupata kutokana na mimi mwenyewe kupata elimu kwa kuungaunga sana.Hii ilitokana na wazazi wetu kutotambua sana umuhimu wa elimu”

“Suala la pili ninaye binti yangu ambaye mara baada ya kumaliza darasa la saba na kupata matokeo mabaya nilihangaika sana kupata shule ya sekondari ya kumpeleka.Nilimpeleka shule tano binafsi lakini kila alipofanya usaili alionekana kushindwa.Nilichokibaini ni kuwa alishindwa kutokana na kuwa na uwezo mdogo wa lugha ya kingereza.Iliniumiza sana,nikawaza halii kama hiyo ikoje kwa jamii inayonizunguka!” alisema Anivene ambaye ni mtaalamu wa Kilimo katika halmashauri ya mji wa Tunduma.

“Watoto wote waliofaulu kwenye usaili uliofanyika kwenye shule nilizompeleka mwanangu nilibainia walitokea katiak shule binafsi.Nikaona walimu katika shule hizi wanajituma kutokana na kutetea ajira zao hivyo mwanafunzi atapewa elimu inayostahili.Katika shule za serikali wapo walimu wanaobweteka na kuona hana cha kupoteza mtoto anapokuwa na maendeleo mabaya kitaaluma”

Anasema hapo alianza kufikiria kupeleka watoto wake wote kwenye shule za michepuo ya Kingereza ili wasikumbwe na adha iliyomkuta dada yao.Alimshawishi mumewe na walianza kuwekeza kidogo kidogo fedha kutoka katika sehemu ya mishahara yao ya kila mwezi.

 “Niligundua gharama haikuwa kubwa sana kumsomesha mtoto katika shule hizi.Nilimshawishi mume wangu kila mmoja wetu atenge shilingi elfu ishirini katika mshahara wake wa kila mwezi.Tukajikuta tunaweza.Yule aliyekuwa darasa la nne na mwezie wa darasa la kwanza tukawapeleka wote English Medium katika shule moja iliyopo hapa mkoani kwetu lakini wilayani Mbozi.”

Anasema kuwapeleka watoto katika shule hiyo ya mchepuo wa kingereza kukampa fundisho jingine ambalo lilizidi kumpanua mawazo na kuzidisha nia ya kutafuta ufumbuzi.Mazingira aliyokutana nayo yakaonekana kutomridhisha kama mzazi.

“Kwakweli pamoja na watoto kuendelea kusoma pale sikuweza kuwa na amani kwakuwa kila tulipokwenda kuwasalimia watoto hatukuridhishwa sana na mazingira tuliyokutana nayo.Masuala ya lishe,malazi na pia mazingiara ya shule kwa ujumla.Tukaona kuna kila dalili za watoto kuambukizana magonjwa kwa urahisi.Hapo tukaamua kuwahamishia katika shule moja iliyopo jijini Mbeya.”

Wakati haya yakifanyika suala la uchungu wa mzazi kuishi mbali na watoto wake nalo likajitokeza.Anivene akajikuta anakuwa mpweke kwa watoto wake kuishi mbali nae.Akahisi watoto pia hawana imani kutokana na kuishi kwao mbali na wapendwa wazazi wao.Akahisi kuna mambo muhimu wanayakosa.

“Hakuna siku niliyoumia kama nilipokuwa namwacha mtoto wangu wa mwisho anakwenda kuanza darasa la awali.Kilikuwa kitoto kidogo mno chenye miaka sita.Kilipoanza kulia nikajikuta na mimi nabubujikwa na machozi.Nilikosa raha hata baada ya kuwa nimemwacha shuleni.Nilijua uangalizi ni mzuri lakini nikawaza namba amekuwa akifurahi kila tuamkapo asubuhi.Nikaona furaha yake sasa itakuwa imepotea na huenda hata masomo ikawa shida kwake.nilibeba uchungu wa wanawake wote wa eneo hili”.

Wakati huo wote alikuwa akijaribu kutafakari ni kwanini watu wenye uwezo kwenye maeneo ya jirani hawajataka kuanzisha shule kama hizo wanazozifuata mbali ili watoto waweze kusoma jirani na makwao?Mji wa Tunduma una wakazi walio na vipato vizuri kutokana na wengi wao kuwa wafanyabiashara wakubwa.Lakini hawakutaka kuwekeza katika suala la elimu.Wote wakawa wanapeleka watoto mbali nao.

“Iliniuma sana lakini ikanibini kuja na wazo jipya.Ili uweze kuanzisha shule yakupasa uwe na vigezo gani.Hapo ndipo nilipoanza mchakato wa kufuatilia vigezo vinavyohitajika mpaka pale niliporuhusiwa na serikali”

Anasema hapo ndipo alipoanza kujenga majengo kwenye eneo lake lililopo katikati ya mji wa Tunduma ambako kwa sasa yapo madarasa ya shule ya awali pekee.Mwaka 2012 baada ya kukamilisha majengo hayo nikaanza kuwaza napataje walimu wa kuanza nao.Mtaji umeishia katika kujenga majengo na kuboresha mazingira.

“Nilihitaji muda wa kujipanga zaidi mpaka kufikia kuanza kuajiri na kupokea wanafunzi.Madhari niliyokuwa nimeweka yanayovutia watoto kwa kuwepo na bembea siku moja yakaniponza.Siku hiyo watoto wawili wa rafiki yangu waliokuwa wakisoma katika shule moja hapa mjini waligoma kwenda shuleni kwao.Walimlazimisha mama yake awalete kwenye majengo yetu na wakasema hawatokwenda shuleni kwao iwapo mama yao hatokubali ombi lao.”

“Mama yao alinipigia simu kuniomba awapeleke kwenye majengo yetu nikamwambia haiwezekani sisi hatujaanza kufanya kazi hivyo hatuwezi kuruhusu.Badaye alipoona wanamsumbua sana akanipigia tena simua akanambia kwakuwa pale kuna walinzi anawapeleka hivyo hivyo ili wakashinde huko wao wafurahi”

“Wakati akinambia hayo alikuwa tayari njiani kuelekea huko.Sikuwa na namna zaidi ya kumkubalia.Nilimpigia mlinzi akawafungulia geti na kuwaruhusu kuingia na mama yao akawaacha hapo.Mpaka nakwenda niliwakuta wanaendelea kucheza wala hata hawakujali kuwa walikuwa peke yao”anasema.

Anasema hapo akawa na mtihani mpya.Ili mlazimu atumie pesa yake ya mfukoni kuwanunulia chipsi kwenye kibanda kilichopo jirani kwaajili ya chakula cha mchana.Baadaye mama yao aliwapitia watoto hao na kurudi nao nyumbani.Kesho yake hali ilikuwa hivyo hivyo,watoto waligoma kwenda shuleni kwao ikabidi waletwe shuleni hapo.

“Nikawa na kibarua kigumu.Watoto wa watu wanasinda kwenye majengo yangu,hakuna mtu wa kuwasimamia,nikaona nina wakati mgumu.Ilibidi nikutane na mzazi wao ili tulijadili jambo hili kwa pamoja.Ajabu hakuwa na hofu kama yangu!Akanambia wewe unasubiri nini kutafuta walimu?akasema tafuta mwalimu aanze kuwafundisha watoto mimi nitakutafutia wanafunzi wengine kama unashindwa kuwatafuta”

“Nikaona mbona huyu simwelewi!Lakini nikaona huenda huu ndiyo mwanzo wenyewe.Akanitafutia mwalimu mmoja anaitwa Sarafina.Sikuwa na kwa kumweka ikabidi niishi nae nyumbani kwangu.Rafiki yangu akashawishi wafanyabiashara wakaniletea watoto wengine wawili.Hapo nikawa na wanafunzi wane.Kwakuwa usajiri  wa shule tulikuwa tumepata tayari hatukuwa na mashaka.”

Anasema baadaye waliopata mwalimu mwingine raia wa Kenya.Lakini hakuweza kudumu shuleni hapo kwakuwa baadaye ilibainika hakuwa ametimiza masharti ya kufanya kazi nchini hivyo aliondoka.Walilazimika kuendelea kudunduliza walimu.

“Unajua tatizo kubwa tulilonalo hapa nchini ni kupata walimu walio na uwezo.Si kwamba walimu hawapo!wapo wengi tu lakini uwezo ni tatizo.Na hii ndiyo inasababisha shule zetu kuwa na ushindani mkubwa wa kuwapata walimu wenye kuiwezesha taasisi yako kufanya vizuri”

Anasema kupenda kwake kujifunza kulimfanya azidi kupanua wigo wa uelewa kila mara aliposafiri.Alipenda kutembelea shule mbalimbali zinazotoa elimu sawa na ya shuleni kwake.Na kila jambo jipya alilojifunza aliangalia namna ya kuliongeza kwenye taasisi yake.

“Kutokana na ugumu wa kupata walimu kuna wakati ilinilazimu kwenda Dar es salaam na kukaa huko kwa majuma mawili nikiwatafuta wanaoweza kuja kunisaidia.Hapo ndipo nilipokutana na mwalimu David Buyogela ambaye sasa ndiye Mkuu wa shule.Nakumbuka ilikuwa mwaka 2013.Wakati huo pia mpaka nafanya mazungumzo na mwalimu huyu nilikuwa naumwa na kabla sijarudi ilibidi nifanyiwe upasuaji”

Kwakuwa mtazao wa familia hii ulikuwa ni kuwa na shule ya awali na Msingi zilizokamilika,waliamua kutumia eneo walilokuwa nalo nje ya mji kidogo litumike kwaajili ya kujenga shule ya msingi.Hapo ujenzi ulianza na baada ya kuziona taasisi za kifedha zikakubali kutukopesha fedha.

Anivene anasema kujua namna ya kutawala imekuwa chachu ya mafaniko kwenye taasisi yao kwani hadi sasa walimu na wanafunzi wamezidi kuongezeka.Wapo wanaohamia wakitokea katika shule nyingine na pia wale wanaoanza awali kila mwanzo wa mwaka wa masomo.

Mkuu wa shule mwalimu Buyogela anasema hivi sasa shule ina jumla ya wanafunzi 255 kwa maana ya kuanzia darasa la awali hadi darasa la tatu.Darasa la awali wapo 114  wasichana wakiwa 58 na wavulana 56,darasa la kwanza wako 71 wavulani 37 na wasichana 34.Darasa la pili waapo 54,wasichana 31 na wavulana 23 na darasa la tatu wako 16 wasichana 11 na wavulana watano.

“Wapo watoto wanaohamia kutoka shule nyingine.Hawa tunawasaili na kuona uwezo wao iwapo unaridhisha anaendelea na darasa alilokuwa huko alikotoka na iwapo tutaona kiwango chake hakiridhishi tunaongeza na mzazi au mlezi kumrejesha darasa moja.Lengo ni kumjengea uwezo kitaaluma aweze kwenda sambamba na wenzie darasani” anasema Buyogela.

“Kama watumishi tumekuwa na jambo la kujivunia kutokana na mahusiano mazuri baina yetu na mwajiri.Baadhi ya waajiri hawapedi kupokea maoni ya wafanyakazi wao.Kwa hapa hali ni tofauti,tunasikilizwa na tunajiona sehemu ya taasisi.”

Baadhi ya wanafunzi shuleni hapa Tecla Almasi,Moses Ndaga na Jesca Korogwe wote wa darasa la tatu,wanasema mazingira ya utoaji elimu yanayokwenda sambamba na kupata chakula yanawawezesha kupata fursa nzuri ya kuwaelewa walimu wao.

 Tecla na Moses wanasema walihamia shuleni hapa wakitokea shule tofauti lakini tofauti na walikotoka hapa wameongeza uwezo kitaaluma.Wanasema huenda mazingira ya walimu kuwajali na uwepo wa miundombinu rafiki ya kufundishiwa imekuwa chachu ya mafanikio yao tofauti na awali.

Uwepo wa uwekezaji shule ya Elisabene umekuwa chachu ya maendeleo kwa watu mbalimbali.Zipo ajira zilizozalishwa kama za walimu,madereva,wapishi,walinzi,watu wa usafi na utunzaji bustani,ujenzi wa majengo,ufyatuaji tofali na nyingine nyingi.

“Wananchi waishio jirani na shule pia tunawapa maji kutoka katika kisima kirefu tulichochimba hapa shuleni.Tunashiriki pia katika shughuli za kijamii kwa kuchangia michango mbalimbali.Tunaamini jamii inayotuzunguka ni sehemu yetu” anasema mkuu wa shule.

Pamoja na mafanikio yaliyofikiwa bado kuna changamoto zinazoikabili shule hii.Miongoni mwa changamoto hizo ni pamoja na mtoto kuletwa akiwa amechelewa kuanza shule,mzazi kutaka mtoto aingie darasa la juu japo hana uwezo akiona kumrudisha darasa atapata hasara.Pia kutokuwepo kwa hostel kunasababisha wanafunzi kukosa muda wa kutosha kupumzika akiwa katika mazingira ya shule.

“Kama watumishi tunataraji utawala unafanyia kazi suala la Usafiri wa watumishi,kujenga nyumba za wafanyakazi,Kujenga hosteli,kupata fursa ya kujiendeleza kielimu,kushiriki semina za mara kwa mara ili kujijengea uzoefu na pia kutuunganisha na taasisi za kifedha ili kupata mikopo na pia mifuko ya kijamii”anasema Buyogela.

Mkurugenzi wa shule anasema changamoto za kiutawala ni pamoja na wazazi kutolipa ada kwa wakati licha ya kuwa wazazi wengi wanao uwezo mzuri kiuchumi,upatikanaji wa walimu,kutofikiwa kwa miundombinu ya maji na maji katika eneo la shule ya msingi hivyo kulazimu kutumika kwa jenereta na kisima cha kuchimbwa.Taasisi za kifedha kutoza riba kubwa kwenye mikopo.

“Tuna changamoto kubwa ya mtazamo hasi wa serikali juu ya fedha binafsi,inaamini kuwa zinapata faida kubwa na hapo ndipo tunapolundikiwa mzigo wa kodi lukuki zikiwemo za majengo,TRA,fedha za ukaguzi,kulipia majengo.Hapa tunaona kama hakuna mahusiano mazuri baina ya serikali na shule binafsi”

“Lakini kuna suala la wazazi kutowajibika na watoto wao.Wapo ambao hawajawahi kufika hapa shuleni tangu watoto wao waanze kusoma hapa.Hawaulizii maendeleo ya watoto wao na wala hawawaandai watoto wanapokuja shule.Mtoto anakuja ukimuona tu utajua huyu anaumwa lakini unapompigia mzazi anakuwa hajui lolote na amemruhusu aje shule siku hiyo.Mtoto mwingine utakuta amekuja na nguo chafu ni kama hakutokea kwa mzazi.Hii yote ni kutokana na wazazi kutowajali watoto” anasema Anivene.

Mkurugenzi huyu anasema matarajio ya taasisi hii ni kujenga hosteli ili watoto waweze kukaa shuleni japo ni kwa wale watakaopenda.Japo hii ni changamoto kwake kwani awali alipenda mtoto aje kusoma na jioni aungane na familia yake.

Kuanzisha shule ya sekondari kutategemea mwenendo mzuri wa mafanikio ya shule ya msingi.Japo ni muhimu kwakuwa itasaidia watoto wanaomalisha shuleni hapo kuendelea na masomo ya sekondari wakiwa katika mazingira waliyoyazoea tofauti na kwenda shule nyingine.

Mtazamo wa Serikali ya mkoa wa Songwe ni kuona uwekezaji katika Nyanja mbalimbali ikiwemo sekta ya Elimu unaimarishwa.Hii itasaidia jamii ya wakazi mkoani hapa kujikwamua na kuondokana na maadui Ujinga,Maradhi na Umasikini pale watakapokuwa na elimu ya kutosha.

“Tunataka kuwaondoa wakazi wa mkoa wa Songwe kwenye Unyonge.Wana fursa nyingi za uzalishaji mali lakini bado ni wanyonge na ili kuwaondoa kwenye hali hii lazima tuwape elimu”alisema mkuu wa mkoa wa SongweLuteni mstaafu Chiku Galawa alipozungumza na wanachama wa Chama cha Waandishi wa Habari za Utalii na Uwekezaji Tanzania(TAJATI).

Kwa upande wake kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa,George Mbijima,alipokimbiza mwenge shuleni hapa alipongeza waasisi wa shule ya Elisabene akisema jamii inapaswa kujikita katika uwekezaji wa kujikomboa kutoka kwenye adui Ujinga.

No comments:

Post a Comment