Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Thursday, January 29, 2015

TAARIFA YA JESHI LA POLISI MKOA WA MBEYA KWA VYOMBO VYA HABARI



MTU MMOJA ASIYEFAHAMIKA JINA WALA MAKAZI YAKE AUAWA KWA KUPIGWA NA WANANCHI WALIOAMUA KUJICHUKULIA SHERIA MKONONI KWA TUHUMA ZA WIZI.


MTU MMOJA ASIYEFAHAMIKA JINA WALA MAKAZI YAKE, JINSI YA KIUME, UMRI KATI YA MIAKA 30-35, ALISHAMBULIWA KWA KUPIGWA SEHEMU MBALIMBALI ZA MWILI WAKE NA KUNDI LA WANANCHI WALIOAMUA KUJICHUKULIA SHERIA MKONONI KUTOKANA NA TUHUMA ZA WIZI.

TUKIO HILO LIMETOKEA MNAMO TAREHE 28.01.2015 MAJIRA YA SAA 16:17 JIONI HUKO ENEO LA MWANJELWA, KATA YA MANGA, TARAFA YA IYUNGA, JIJI NA MKOA WA MBEYA. INADAIWA KUWA CHANZO CHA TUKIO HILO NI TUHUMA ZA WIZI BAADA YA MAREHEMU KUTUHUMIWA KUHUSIKA KATIKA TUKIO LA UVUNJAJI LA TAREHE 26.01.2015. MWILI WA MAREHEMU UMEHIFADHIWA HOSPITALI YA RUFAA MBEYA.

KAIMU KAMANDA WA POLISI MKOA WA MBEYA KAMISHNA MSAIDIZI WA POLISI BARAKAEL N. MASAKI ANATOA WITO KWA WANANCHI KUACHA TABIA YA KUJICHUKULIA SHERIA MKONONI KWANI NI KINYUME CHA SHERIA NA BADALA YAKE WAJENGE TABIA YA KUWAFIKISHA WATUHUMIWA WANAOWAKAMATA KWA TUHUMA MBALIMBALI KWA HATUA ZAIDI ZA KISHERIA.

Imetolewa na:

[BARAKAEL N. MASAKI – ACP]
KAIMU KAMANDA WA POLISI MKOA WA MBEYA.

Tuesday, January 27, 2015

AUAWA KWA SHOKA,ANYOFOLEWA ULIMI,MENO NA JICHO LA KUSHOTO

WATU watatu wamefariki dunia mkoani Mbeya katika matukio tofauti yakiwemo mawili ya mauaji ya kinyama.

Miongoni mwa matukio ya mauaji hayo ni pamoja na la mkazi wa kijiji cha Mkutano wilayani Momba,Hamis Simwawa(25) aliyekutwa shambani akiwa ameuawa kwa kukatwa shoka shingoni na kisha kunyofolewa viungo vya mwili ikiwemo ulimi,meno ya chini na jicho la kushoto.

Kaimu kamanda wa polisi mkoani Mbeya Barakael Masaki mwili wa Hamis ulikutwa Januari 26 mwaka huu majira ya saa 2:00 asubuhi katika kijiji cha  Mkutano kilichopo katika kata ya Nzoka wilayani Momba.

Kaimu kamanda Masaki alisema kabla ya mauaji kijana huyo aliitwa kwenda kusaidia shughuli za shamba na alipofika shambani ndipo walimuua kwa kumkata na shoka shingoni kabla ya kumnyofoa ulimi,meno ya chini na jicho la kushoto na kupeleka viungo hivyo kusikojulikana.

Alisema tukio hilo linahusishwa na imani za kishirikina na kufuatia mauaji hayo watu wawili wanashikiliwa aliowataja kuwa ni Kawawa Sinkala(31) na Emmanuel Sinkala(15) wote wakazi wa kijiji cha Mkutano.

Katika tukio la pili Kaimu kamanda Masaki alisema Mwinzala Sekele mwenye umri wa kati ya miaka 40 na 45 mkazi wa kitongoji cha Chang’ombe kilichopo kijijini Mshewe wilayani Mbeya aliuawa kwa kupigwa sehemu mbalimbali za mwili wake na kundi la wananchi walioamu kujichukulia sheria mkononi.

Alisema mwili wa marehemu ulikutwa saa Januari 26 mwaka huu majira ya saa 5:00 asubuhi ukiwa umetelekezwa kijijini mshewe kata ya Bonde la Usongwe wilayani Mbeya.

Kwa mujibu wa kaimu kamanda Masaki inadaiwa kuwa chanzo cha mauaji hayo ni kulipiza kisasi kufuatia marehemu kutuhumiwa kuhusika na mauaji yaliyotokea awali Januari 24 mwaka huu majira ya saa tisa alasiri ambapo mkazi wa mkazi wa kijiji cha Mshewe Sekela Kaini alikutwa ameuawa na mwili wake kutupwa kwenye shamba la mahindi kijijini hapo.

Wakati huo huo mkazi wa Ilomba jijini Mbeya Joshua Mwaisanila(35) alifariki dunia baada ya kugongwa na lori lenye namba T 189 BLKs Semi Trailler lililokuwa na tela lenye namba  T 193 BLK lililokuwa likiendeshwa na Ahazi Cheyo(24) mkazi wa Iyunga jijini Mbeya.

Kaimu kamanda Masaki alisema ajali hiyo ilitokea Januari 26 mwaka huu saa tatu asubuhi maeneo ya Forest barabara kuu ya Mbeya/Tunduma na dereva wa lori hilo anashikiliwa na polisi wakati chanzo cha ajali kinachunguzwa.

CHADEMA MBEYA WAANZA KUJIPUNGUZA KASI,WAONESHA KUTOUTAKA UKAWA

KATIKA kile kinachoonekana Chama cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA) Mbeya mjini kuzidi kupoteza mwelekeo na pia kudhihirisha kutoheshimu Umoja wa Katiba ya Wananchi(UKAWA),chama hicho kimewatimua makada wake watatu kwa kile kilichoelezwa kuwa walikuwa waasi ndani ya chama.

Miongoni mwa waliovuliwa madaraka na kisha kutimuliwa ni pamoja na mjumbe wa Kamati tendaji ya wilaya Meshack Kapange ambaye pia ni mwenyekiti wa Chadema kata ya Uyole.

Wengine ni katibu wa baraza la wanawake la wilaya(Bawacha) Agatha John na Mtunza hazina wa Chama hicho katika kata ya Igawilo Stanley Tweve.

Taarifa zilizolifikia gazeti hili kutoka chanzo cha ndani ya chama hicho zinaeleza kuwa uamuzi huo ulifikiwa juzi katika kikao kilichofanywa na Kamati tendaji ya wilaya na kuamuru kuwasimamisha uanachama wafuasi wake hao watatu.

“Taarifa hizi ni za kweli kabisa na ni maamuzi yaliyofikiwa kwenye kikao cha jana.Vipo vikao vingi vilivyofanyika kabla ya hiki kilichotoa maamuzi ya kuwavua uanachama” alisema mmoja wa makada wa Chadema aliyeomba kutoandikwa jina lake gazetini.

Alipohojiwa juu ya taarifa za kuvuliwa uanachama Kapange alikiri kupokea barua kutoka wilayani ya kusitishiwa uanachama kabisa.

Kapange alisema alipokea barua hiyo juzi akisimamishwa uanachama kwa tuhuma za kuandaa na kuratibu mkutano wa Umoja wa Katiba ya Wananchi(Ukawa) uliofanyika Januari 5, mwaka huu katika viwanja vya Shule ya msingi Hasanga Uyole jijini Mbeya na kuhutubiwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini David Kafulila.

Kwa mujibu wa Kapange,tuhuma nyingine anazotuhumiwa na viongozi wa Chama hicho ni kutoa nafasi fupi ya kusalimia wafuasi walioshiriki mkutano huo kwa Mwenyekiti wa Wilaya ya Mbeya mjini John Mwambigija kwani alimpa dakika mbili tu kwenye mkutano huo.

Viongozi walipenda Mwambigija apewe muda mrefu kama ambavyo imekuwa ikifanyika kwenye mikutano yote ya Chadema mjini hapa tofauti na viongozi wengine kutoka vyama mbalimbali vinavyounda Ukawa ambao pia walikuwa wakipewa dakika mbili mbili kila mmoja kusalimia wananchi.

Aliongeza kuwa sababu nyingine ni yeye kama mratibu wa mkutano huo kukaa meza kuu sambamba na mgeni rasmi ambaye ni Mbunge David Kafulila na kushindwa kumpisha Mwenyekiti wake John Mwambingija kwa kuwa ndiye mwenye cheo kikubwa kuliko Mratibu wa Mkutano huo wa Ukawa.

Kapange pia hakusita kuwataja wanachama wengine waliovuliwa uanachama na kikao cha Kamati tendaji ya Wilaya kuwa ni Agatha John katibu wa Baraza la Wanawake wa Chadema(BAWACHA) Wilaya ya Mbeya mjini na Mtunza hazina wa Chadema kata ya Igawilo, Stanley Tweve.

Kwa upande wake Katibu wa Baraza la Vijana wa Chadema(Bavicha) Mbeya mjini Gidion Siame, ambaye ndiye aliyesaini barua za kuwasimamisha uanachama viongozi hao alipoulizwa kuhusiana na taarifa hizo alikiri na kufafanua kuwa uamuzi huo umetokana na kikao halali cha chama ngazi ya wilaya.

Kwa mujibu wa Siame,awali kabla ya maamuzi ya mwisho wanachama hao waliitwa katika vikao vya Chama kwa ajili ya kuhojiwa kuhusu tuhuma zinazowakabili lakini hawakutoa ushirikiano badala yake walikuwa wakijibu kama wanavyotaka wao na hicho ndicho kilichopelekea maamuzi hayo ya kamati.

Alifafanua kuwa hatua ya kuwatimua uanachama makada hao imefikiwa kwa mujibu wa katiba ya Chama Ibara ya 5(3&4) inayohusu kukoma kwa uanachama na kwamba wanayo nafasi ya kukata rufaa katika vikao vingine ngazi za juu ili kupinga adhabu waliyopewa katika ngazi ya wilaya.

ULEVI NOMAAAAAAAAAA!!!!!!!!

 Jamaa ambaye hakufahamika jina wala makazi yake akiwa amelewa chakari kama alivyokutwa na kamera ya Lyamba Lya Mfipa katika mitaa ya Kabwe jijini Mbeya jirani na Blue House Pub.
PICHA NA ERASTO KIKWALA WA Lyamba Lya Mfipa

Friday, January 23, 2015

ZIARA YA WAJUMBE WA KAMATI YA BUNGE YA KUDUMU YA MIUNDOMBINU BANDARI ZA KIWIRA NA ITUNGI ZIWA NYASA

 Wajumbe wa kamati ya kudumu ya Bunge ya Miundombinu wakikagua eneo la Bandari ya Itungi lililokuwa limejaa mchanga awali na mchanga huo kuondolewa na maji ya mafuriko ya Aprili mwaka jana











Mkuu wa Bandari ya Kyela Parcival Salama akitoa maelezo ya Bandari ya Itungi kwa waziri wa Miundombinu Dk Harison Mwakyembe na wajumbe wa kamati ya kudumu ya bunge ya Miundombinu.
 Mhariri mkuu wa Lyamba Lya Mfipa Ndugu Joachim Nyambo akiwa katika boti na baadhi ya wajumbe wa kamati ya bunge ya miundombinu kukagua bandari ya Itungi.



Monday, January 19, 2015

CBE YAKABIDHI MSAADA HOSPITALI YA WAZAZI META


                             HABARI KAMILI

MSAADA wa shuka wenye thamani  ya takribani shilingi milioni tano umetolewa na Chuo cha Biashara(CBE) kwa hospitali ya Rufaa Mbeya kitengo cha wazazi na watoto cha Meta.

CBE imetoa msaada huo ikiwa ni sehemu ya maadhimisho yake ya kutimiza jumilei ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwa chuo hicho nchini ikiwa ni wakati pia ambapo inajivunia mafanikio yake yakiwemo kusambaza matawi yake mikoani likiwemo la Mbeya.

Akikabidhi msaada huo leo,mkuu wa chuo cha CBE Prof Emmanuel Mjema amesema chuo kinathamini huduma za afya hudusani kitengo cha uzazi kutokana na kuwa kati ya maeneo muhimu yanayowezesha afya ya binadamu kuimarika.

Amesema kutolewa kwa shuka hizo kunadhihirisha wazi kuwa CBE inakijali kizazazi kilichopo na kijacho hivyo kuna kila sababu ya kuweka mazingira bora kwa mtoto anayezaliwa ili akue akiwa na afya bora na hatimaye maishani mwake kuja kuwa mtaalamu wa biashara akiwa miongoni mwa wadau wa chuo hicho.


Kwa upande wake Mkuu wa hospitali ya wazazi Meta Dk.John Francis amesema msaada huo umekuja kwa wakati muafaka kwani licha ya hospitali ya rufaa katika kitengo hicho kutokuwa na uhaba mkubwa wa vitendea kazi,bado vifaa vilivyopo havitoshelezi mahitaji.

Dk.Francis amesema kumekuwepo na ongezeko kubwa la akina mama na watoto wanaofika hospitalini hapo kuhitaji huduma za afya hivyo wadau wanapaswa kuendelea kutoa michango yao ya hali na mali ili huduma bora inayotolewa izidi kuwa endelevu.

Tuesday, January 6, 2015

UAPISHAJI WENYEVITI WA MITAA NA WAJUMBE ULIVYOINGIA DOSARI JIJINI MBEYA

 Kaimu mwanasheria wa halmashauri ya jiji la Mbeya Chrispin Kaijage akigawa fomu za kiapo kama njugu nje ya ukumbi hali iliyosababisha hata wasiopaswa kuapishwa kuchukua fomu hizo.

 Afisa mwingine wa halmashauri ambaye hakufahamika jina lake mara moja naye akiendelea kugawa fomu za kiapo.

 Baadhi ya watu ambao hawakujulikana iwapo walikuwa wajumbe halali wa shughuli ya kuapishwa au la wakizisoma fomu za kiapo mara baada ya kugawiwa.



 Wajumbe wakiwa wametawanyika mara baada ya kutoka nje ya ukumbi

 Baadhi ya wajumbe wakimshangaa mwanasheria wa jiji kwa kitendo chake cha kugawa fomu za kiapo kama njugu nje ya ukumbi.
 Haikujulikana mara moja maboksi haya yalikuwa na nini ndani.Yaliondolewa ukumbini mara baada ya wajumbe kukasirika na kuamua kutoka nje ya ukumbi.



                           HABARI KAMILI
KATIKA kile kinachodhihirisha uwepo wa baadhi ya watendaji ambao wamekuwa wakisababisha serikali kuchukiwa na wananchi kwa kuvurunda kwenye maeneo yao,kaimu mwanasheria wa halmashauri ya jiji la Mbeya Chrispin Kaijage jana(Januari 5) alivuruga shughuli ya kuwaapisha wenyeviti na wajumbe wa serikali za mitaa.

Shughuli hiyo iliyokuwa ianze majira ya saa tano asubuhi katika ukumbi wa shule ya sekondari ya Mbeya Day jijini hapa,shughuli hiyo ilionekana kuanza kuingia dosari tangu mapema na hali hiyo kuendelea hadi tunakwenda mitamboni.

Dosari ya kwanza ilianza pale Kaijage aliporuhusu shughuli hiyo kugeuzwa na kuwa mkutano wa kisiasa ukiongoza na mmoja wa viongozi wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi(Ukawa) Baraka Mwakyabula ambaye ni katibu mwenezi wa Chadema Mbeya mjini.

Chini ya mwanasheria huyo,Mwakyabula alikabidhiwa ukumbi na kuendesha mkutano atakavyo kwani ndiye aliyeweza kuchagua wajumbe aliotaka wasimame na kuuliza maswali yaliyoikuwa yakijibiwa na mwanasheria wakati wajumbe wakisubiri viongozi wa halmashauri wafike kuwaapisha.

Ni wakati huop ambapo baadhi ya wajumbe walionekana kukerwa na kile kilichoendelea ukumbini hapo kiasi cha kumtaka mwanasheria aharakishe kuwaleta viongozi wa halmashauri ili waapishwe na kuondoka ili wakaendelee na shughuli zao nyingine.

Wajumbe walionekana kusononeshwa zaidi kwa mwanasheria kuendelea kuruhusu shughuli ya kuapishwa ambayo ilikuwa ikiendelea kuchelewa na kugeuzwa kuwa mkutano wa kisiasa kwani hata katika kuteua wajumbe wa kuuliza mwongozaji alikuwa akionekana kutoa nafasi zaidi kwa wajumbe kutoka vyama vya upinzani na kuwanyima fursa wanaotoka CCM.


Siasa hizo zilizokwenda sambamba na kuchelewa kwa mkurugenzi wa halmashauri ya jiji Musa Zungiza kulizidi kuingiza dosari shughuli nzima kwani ilipofika majira ya saa nane kasoro wajumbe walichukua uamuzi wa kuanza kutoka nje ya ukumbi na hapo kila mmoja akawa anaongea kwa jazba maneno aliyoona yanafaa.

Wakizungumza kwa jazba nje ya ukumbi wajumbe hao walisema Mkurugenzi wa Jiji na uongozi wa Halmashauri kwa ujumla umewadharau na kuwanyanyasa kutokana na kutofuata muda waliokuwa wamewaandikia awali.

Mwakyabula ambaye pia ni mwenyekiti wa Mtaa wa Mwanjelwa alimgeuka mwanasheria na kuungana na wajumbe wenzake kulalamika akisema katika barua ya Halmashauri ya Jiji ya kuwaita kuapishwa ilidai wanapaswa kufika eneo la tukio kuanzia majira ya saa tano asubuhi jambo ambalo lilitekelezwa kwa wakati lakini wahusika hawakufika katika muda ulioandikwa.

“Kitendo hiki ni kuonesha dharau kwa wenyeviti na wajumbe.Haiwezekani wakatuita saa tano asubuhi lakini hadi hivi sasa ni saa nane mchana hawajafika, hii ni fedheha kubwa hivyo tumekubaliana zoezi hili liahirishwe kwa leo hadi siku nyingine watakapojipanga” alisisitiza Mwenyekiti huyo.

Hata hivyo alisema licha ya kuahirisha kwa shughuli hiyo ya kuapishwa lakini uongozi wa halmashauri ya Jiji la Mbeya unapaswa kuwaomba msamaha wajumbe kwa kuwadharirisha pamoja na kuwalipa posho ya siku hata kama zoezi halikufanyika.


Wakati hayo yote yakiendelea wajumbe walikuwa wamegawanyika ambapo kundi kubwa walikuwa nje na wachache walisalia ndani ya ukumbi wakiendelea kusubiri na hapo ndipo ilikuja dhana ya kuwa waliobakia ukumbini ni wanaccm na baadhi ya wajumbe waliokuwa nje wakaanza kusuka mpngo wa kuingia wawapige ili kuwalazimisha kutoka nje.

Wakati hayo yakiendelea,punde kaimu mwanasheria alionekana akiwa katika lango kuu(Getini) na akaanza kugawa fomu kiholela kwa wajumbe waliokuwa jirani hali iliyosababisha wajumbe wote waliokuwa nje kukimbilia eneo la getini na kuanza kugawana fomu za kiapo kama njugu.

Wapo wajumbe walioonekana kuchukua fomu zaidi ya kumi na kuanza kuwagawia wenzao lakini wapo pia ambao walichukua fomu kwa kiasi hicho na wakaonekana kutoka nje ya geti na kuelekea makwao pasipo kueleza fomu hizo walikuwa wakizipeleka wapi.

Hali hiyo ilisababisha baadhi ya wajumbe kuhoji ni kwa namna gani udhibiti wa fomu hizo umewekwa kwakuwa kulikuwa na uwezekano mkubwa wa fomu kujazwa na mtu asiyestahili.


Kwa upande wake Kaijage, ambaye alikuwa akiwasihi wajumbe kutulia lakini alishindwa kutoa ufafanuzi juu ya sababu ya kuchelewa kwa viongozi waliopaswa kuwaapishwa Wenyeviti hao pamoja na wajumbe wao.


Aidha alipoulizwa na waandishi wa habari sababu za yeye kuanza kugawa fomu za kiapo kiholela pasipo kufuata utaratibu huku akianzia barabarani alijibu kuwa yeye sie msemaji bali alifika kituoni hapo kushuhudia zoezi la kuwaapisha viongozi hao.


Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Mbeya, Musa Zungiza, alipofuatwa ofisini kwake,wanahabari walijibiwa kuwa alikuwa nje ya ofisi katika shughuli za kuapisha wajumbe na wenyeviti kwenye kanda nyingine na alipotafutwa kwenye simu yake ya kiganjani kujibu changamoto iliyojitokeza hakuweza kupokea.

Friday, January 2, 2015

VITUKO VYA KUVUKA MWAKA

 Mmoja wa wakazi wa jijini Mbeya ambaye hakufahamika jina lake mara moja akiwa amelewa kiasi cha kushindwa kutembea kama alivyokutwa na Lyamba Lya Mfipa maeneo ya Ilemi Darajani jijini Mbeya.
Baadhi ya wakazi wakiendelea kumshangaa alipokuwa akishindwa kunyenyuka ili aendelee na safari.Ilikuwa Januari Mosi 2015 majira ya saa Kumi jioni.

PICHA NA ERASTO KIKWARA WA Lyamba Lya Mfipa

KIKUNDI CHA SAVE ORPHANS CHATOA MSAADA WA MWAKA MPYA KWA YATIMA

 Vitu mbalimbali vilivyokabidhiwa kwa kituo hicho

 Mwenyekiti wa kikundi cha Save Orphans Redson Kaisi akizungumza jambo kabla ya kukabidhi msaada
 Mkuu wa kituo Malezi ya Huruma Anna Kasile akibainisha namna watoto waishio kituoni hapo wanavyopokelewa na kulelewa.




                             HABARI KAMILI
KIKUNDI cha Save Orphans cha jijini Mbeya kimetoa msaada wa vitu mbalimbali vikiwemo vyakula kwa kituo cha kulelea watoto yatima cha Malezi ya Huruma kilichopo Simike jijini hapo.

Baadhi ya vitu vilivyokabidhiwa ni mchele,sukari,nyama,mafuta ya kupikia na ya kupakaa,sabuni za unga na za mche,madaftari na kalamu za wino na risasi.

Mwenyekiti wa kikundi cha Save Orphans Redson Kaisi amesema lengo la kutoa msaada huo ni kuwawezesha watoto kituoni hapo kusherehekea sikukuu ya mwaka mpya kwa furaha kama ilivyo kwa watoto wengine.

Kaisi alisema kikundi hicho chenye wanachama wanne kimekuwa kikitoa misada kwa vituo mbalimbali vya kulelea watoto yatima kutokana na kutambua mahitaji ya watoto hao ambao baadhi ya wanajamii wamekuwa wakiwatenga.

Ameitaka jamii kwa namna inavyoguswa kujitolea kuwasaidia watoto yatima ili kuwawezesha kuishi maisha mazuri na kutimiza ndoto zao kwa kuwajengea mazingira bora ya kuishi.

“Asilimia kubwa ya jamii tumekuwa tukijisahau kwa kuwapa huduma za msingi watoto tunaoishi nao majumbani pekee.Tunasahau kuwa wapo ambao hawana wazazi wala walezi ambao nao wana uhitaji kama wale tunaoishi nao.Tukiendelea kuwasahau tujue tunajenga tabaka la kiubaguzi ndani ya jamii zetu” alisema Kaisi.

Akipokea msaada huyo,mkuu wa kituo Malezi ya Huruma Anna Kasile amesema amekuwa akiwalea watoto kituoni hapo katika mazingira magumu kutokana na kutokuwa na chanzo cha mapato zaidi ya misaada ya wadau mbalimbali.

Kasile pia amelalamikia uwepo wa watu ambao wamekuwa wakimbeza kwa kumuita mtu aliyepungukiwa na akili na ndiyo sababu anaendelea kupokea na kuishi na watoto waio wake.

Hata hivyo amesema changamoto hizo haziwezi kumkatisha tama,badala yake anazichukulia kama chanhu ya kuongeza upendo wake kwa jamii ya watoto yatima na kuomba wadau zaidi kuendelea kushirikiana naye katika kutimiza malengo na ndoto za watoto kituoni hapo.