Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Tuesday, January 27, 2015

CHADEMA MBEYA WAANZA KUJIPUNGUZA KASI,WAONESHA KUTOUTAKA UKAWA

KATIKA kile kinachoonekana Chama cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA) Mbeya mjini kuzidi kupoteza mwelekeo na pia kudhihirisha kutoheshimu Umoja wa Katiba ya Wananchi(UKAWA),chama hicho kimewatimua makada wake watatu kwa kile kilichoelezwa kuwa walikuwa waasi ndani ya chama.

Miongoni mwa waliovuliwa madaraka na kisha kutimuliwa ni pamoja na mjumbe wa Kamati tendaji ya wilaya Meshack Kapange ambaye pia ni mwenyekiti wa Chadema kata ya Uyole.

Wengine ni katibu wa baraza la wanawake la wilaya(Bawacha) Agatha John na Mtunza hazina wa Chama hicho katika kata ya Igawilo Stanley Tweve.

Taarifa zilizolifikia gazeti hili kutoka chanzo cha ndani ya chama hicho zinaeleza kuwa uamuzi huo ulifikiwa juzi katika kikao kilichofanywa na Kamati tendaji ya wilaya na kuamuru kuwasimamisha uanachama wafuasi wake hao watatu.

“Taarifa hizi ni za kweli kabisa na ni maamuzi yaliyofikiwa kwenye kikao cha jana.Vipo vikao vingi vilivyofanyika kabla ya hiki kilichotoa maamuzi ya kuwavua uanachama” alisema mmoja wa makada wa Chadema aliyeomba kutoandikwa jina lake gazetini.

Alipohojiwa juu ya taarifa za kuvuliwa uanachama Kapange alikiri kupokea barua kutoka wilayani ya kusitishiwa uanachama kabisa.

Kapange alisema alipokea barua hiyo juzi akisimamishwa uanachama kwa tuhuma za kuandaa na kuratibu mkutano wa Umoja wa Katiba ya Wananchi(Ukawa) uliofanyika Januari 5, mwaka huu katika viwanja vya Shule ya msingi Hasanga Uyole jijini Mbeya na kuhutubiwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini David Kafulila.

Kwa mujibu wa Kapange,tuhuma nyingine anazotuhumiwa na viongozi wa Chama hicho ni kutoa nafasi fupi ya kusalimia wafuasi walioshiriki mkutano huo kwa Mwenyekiti wa Wilaya ya Mbeya mjini John Mwambigija kwani alimpa dakika mbili tu kwenye mkutano huo.

Viongozi walipenda Mwambigija apewe muda mrefu kama ambavyo imekuwa ikifanyika kwenye mikutano yote ya Chadema mjini hapa tofauti na viongozi wengine kutoka vyama mbalimbali vinavyounda Ukawa ambao pia walikuwa wakipewa dakika mbili mbili kila mmoja kusalimia wananchi.

Aliongeza kuwa sababu nyingine ni yeye kama mratibu wa mkutano huo kukaa meza kuu sambamba na mgeni rasmi ambaye ni Mbunge David Kafulila na kushindwa kumpisha Mwenyekiti wake John Mwambingija kwa kuwa ndiye mwenye cheo kikubwa kuliko Mratibu wa Mkutano huo wa Ukawa.

Kapange pia hakusita kuwataja wanachama wengine waliovuliwa uanachama na kikao cha Kamati tendaji ya Wilaya kuwa ni Agatha John katibu wa Baraza la Wanawake wa Chadema(BAWACHA) Wilaya ya Mbeya mjini na Mtunza hazina wa Chadema kata ya Igawilo, Stanley Tweve.

Kwa upande wake Katibu wa Baraza la Vijana wa Chadema(Bavicha) Mbeya mjini Gidion Siame, ambaye ndiye aliyesaini barua za kuwasimamisha uanachama viongozi hao alipoulizwa kuhusiana na taarifa hizo alikiri na kufafanua kuwa uamuzi huo umetokana na kikao halali cha chama ngazi ya wilaya.

Kwa mujibu wa Siame,awali kabla ya maamuzi ya mwisho wanachama hao waliitwa katika vikao vya Chama kwa ajili ya kuhojiwa kuhusu tuhuma zinazowakabili lakini hawakutoa ushirikiano badala yake walikuwa wakijibu kama wanavyotaka wao na hicho ndicho kilichopelekea maamuzi hayo ya kamati.

Alifafanua kuwa hatua ya kuwatimua uanachama makada hao imefikiwa kwa mujibu wa katiba ya Chama Ibara ya 5(3&4) inayohusu kukoma kwa uanachama na kwamba wanayo nafasi ya kukata rufaa katika vikao vingine ngazi za juu ili kupinga adhabu waliyopewa katika ngazi ya wilaya.

No comments:

Post a Comment