Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Sunday, November 26, 2017

MATUKIO YA USAJIRI WATEJA BARAZANI ENTERTAINMENT DAR

MAKAO MAKUU KINONDONI STUDIO DAR ES SALAAM
 KAZI YA KUSAJIRI WATEJA IKIENDELEA KATIKA MITAA MBALIMBALI
 MTEJA AKIELEKEZWA MFUMO MPYA WA UNUNUZI WA KAZI ZA SANAA KUPITIA BARAZANI ENTERTAINMENT AMBAPO MTEJA ATANUNUA KWA KUTUMIA SIMU YAKE YA KIGANJANI NA KISHA WAKALA KUMFIKISHIA BIDHAA NYUMBANI KWAKE
 UTOAJI ELIMU KWA WATEJA UKIENDELEA KUPITIA PROMOSHENI KABAMBE INAYOENDE;LEA KUTIKISA JIJINI DAR ES SALAAM.





UNASUBIRI NINI! JISAJIRI LEO UPATE NAMBA YAKO YA BARAZANI

Wednesday, November 15, 2017

Niliyoshuhudia Kipindupindu cha Mbarali.

 Na Joachim Nyambo.

KAMA kuna msukosuko Wakazi wa wilaya ya Mbarali mkoani Mbeya hawatokuja kuusahau kwenye historia ya mwaka 2017 ni Ugonjwa wa kipindupindu.Kwa hakika ugonjwa huu umeacha historia kubwa wilayani hapa.Na hakika wakazi wa wilaya hii wamepata shida.

Agosti  2 mwaka huu ndipo Ugonjwa wa Kipindupindu uliripotiwa kulipuka katika baadhi ya maeneo ya wilaya ya Mbarali.Kibaya zaidi ni kuwa maeneo ya awali hakukuwa na wataalamu wa kubaini kuwa wagonjwa waliopatikana walikuwa na dalili za ugonjwa huo hivyo waliendelea kuachwa majumbani wakipata tiba za kubahatisha.Hawakuamini kipindupindu kinaweza kutokea kiangazi cha jua kali.
Baada ya Agost 2,ugonjwa ulipobainika ndipo heka heka zilikolea.Jambo la kwanza ilikuwa ni maamuzi ya Kamati ya ulinzi na usalama kupiga marufuku utoaji holela wa huduma za vyakula na vinywaji.Hapo ililazimu Hoteli,Migahawa na Mamalishe zote kufungwa.Vivyo hivyo kwa vilabu hususani vya pombe za kienyeji.

Kufungwa kwa maeneo haya muhimu kukaleta adha si tu kwa wafanyabiashara wa vyakula na vinywaji kushindwa kujiingizia kipato.Walaji nao walipata wakati mgumu.Wageni ndiyo walikuwa katika wakati mgumu zaidi kwani wakati wenyeji walipokwenda majumbani mwao kula chakula,wao walilazimika kushinda njaa au kuponea biskuti na soda.

Kwakuwa katazo hili lilidumu kwa siku kadhaa,wauzaji na wateja wa vyakula na pombe walibuni mbinu.Mbinu hizi zilikuwa za hatari zaidi na huenda ndizo zilisababisha ugonjwa kusambaa kwa kasi.Ilikuwa ni kupika na kuuza vyakula majumbani kwa uficho.Huku usafi haukuzingatiwa kwakuwa kila kitu kilifanyia kwa siri.Hata vyombo vilivyotumika havikukaushwa juani kwani vingeonekana machoni pa watawala waliopiga marufuku.

Uuzaji pombe za kienyeji ulikuwa wa hatari zaidi.Wauzaji waliozinunua kutoka kwa waliozitengeneza kwa kificho walikwenda kuziuzia kwenya maeneo yaliyojificha na wanywaji kuyatumia maeneo hayo pasipo kujali hali ya usafi.Wapo inaosemekana walinywea pombe chooni.Hivyo walikaa nje ya nyumba ya mtu kama wanajamii wanaojadiliana mambo ya msingi lakini walipeana muda wa kuingia msalani kunywa pombe kwani vilabuni hazikuwekwa.

Naikumbuka Agost 4 niliposhuhudia mama mmoja anaeuza Supu ya Ng’ombe katika vibanda vilivyopo jirani na ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Mbarali alipokimbia na Sufuria ya Supu baada ya kuona kundi la wanahabari tukielekea nyumbani kwake.Tukiwa wanne tulikuwa wilayani hapa kikazi na tulipowauliza wenyeji walituonesha sehemu tunayoweza kupata kifungua kinywa kwakuwa tulitoka jijini Mbeya alfajiri.

Pasipo kujua kama mama huyo alikuwa anauza kificho kwani hatukuwa tumefika mjini Rujewa wala kukutana na uongozi ili kujua kilichokuwa kinaendelea juu ya masuala ya chakula tulikwenda moja kwa mwa mama huyo,lakini tukashangazw3a baada ya kuona anatoka mbio na sufuria lake na kulificha nyuma ya nyumba yake.Tulipoulizia supu wakati amerudi tulijibiwa hawakupika siku hiyo.

Tulilazimika kurudi katika jengo la Ofisi ya mkuu wa wilaya lakini kabla hatujafika tukaitwa na mwenyeji ambaye kimsingi alikuwa ametutambua.Ndipo tulisimama na alipotufikia kwa sauti ya chini akasema…

“Sikilizeni Yule mama alijua ninyi ni askari.Unajua huku kwetu wamepiga marufuku kuuza vyakula kutokana na kipindupindu.Sasa huyu anauza kwa kificho na kwakuwa huku hakuna ni mbali na majumbani sisi tunalazimika kula hapa japo tunamsimamia.Hivyo ninyi nendeni kwani nimekwisha mwelekeza ni nyi ni akina nani.”alituambia mwenyeji yule.

Hatukuwa na namna zaidi ya kurudi na kupata kifungua kinywa.Japo ilikuwa kwa mashaka makubwa lakini hatukuwa na chaguo kwakuwa njaa nayo ilikuwa inauma na hatukujua kazi tuliyoendea itaanza saa ngapi na itatuchukua muda gani.Tulipokwenda mjini Rujewa ndipo tukashuhudia vibanda vyote vya vyakula kufungwa.

Agost hiyo 4 katika Kikao cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya wilaya ya Mbarali,Serikali ya wilaya  ikawataka wananchi  wa maeneo yote wilayani hapa kuchukua Tahadhari.Hadi tarehe hiyo watu wanne walikuwa wamekufa na 55 kulazwa katika kambi maalumu kutokana na ugonjwa huo.

Hadi wakati huo maeneo yaliyokuwa yamekumbwa na Kipindupindu ni ugonjwa huo ni Kata tatu za Ubaruku,Rujewa na Lugelele huku chanzo cha mlipuko kikitajwa kuwa ni kuchafuliwa kwa maji ya Mto Mbarali maarufu kwa jina la Mfereji wa Wachina ambao huriririsha maji yake katika kata hizo.

Akitoa salamu za Serikali kwenye kikao cha Baraza la Madiwani wa Halmashau ya wilaya ya Mbarali,Mkuu wa wilaya hiyo Reuben Mfune aliwataka madiwani kuhamasisha wananchi kwenye kata zao kuchukua tahadhari badala ya kubaki wakiamini kipindupindi kitaishia tu kwenye maeneo kiliporipotiwa kwa sasa.

“Tuwaambie wananchi tuwahimize usafi,wasio na vyoo tuhakikishe wanakuwa navyo.Tusijione took salama kwakuwa maeneo yetu hajagundulika mgonjwa.Ni muhimu tukachukua tahadhari mapema kabla hakijasambaa zaidi”alisisitiza Mfune.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo,Kivuma Msangi aliwataka wakazi wilayani hapa kuchukua hatua za haraka kuwafikisha kwenye kambi maalumu iliyopo katika uwanja wa Barafu mjini Rujewa wagonjwa wanaoonekana kuwa na dalili za ugonjwa huo badala ya kubaki nao majumbani au kuwapeleka kwenye zahanati na Hospitali ya wilaya.

Msangi aliwahakikishia madiwani kuwa kwa idadi ya wagonjwa waliopo kwa wakati huo dawa zilizokuwepo zilikuwa zintosheleza lakini uhaba ungeweza kujitokeza iwapo ugonjwa huo utasambaa zaidi na kusababisha ongezeko kubwa la wagonjwa.
Hadi kufikia Agosti 30 zaidi ya watu 700 walikuwa wameripotiwa kuugua Kipindupindi tangu ugonjwa huo ulipobainika Agosti 2.Idadi ya waliokuwa wamekufa ilifikia nane.Watatu wa awali wakiwa walikufa kabla ya ugonjwa kutambulika,wanne walifia majumbani baada ya ugonjwa kutambulika na mmoja alikufa wakati akielekea Hospitali kupata matibabu.

Kwa mujibu wa Msangi hadi Agosti 30 idadi kubwa iliyokuwa imewahi kufikiwa ni ya wagonjwa 77 kwa siku.Lakini siku hiyo wagonjwa waliokuwepo ni saba hatua iliyoanza kuonyesha kuwa kulikuwa na kila dalili za kutokomeza ugonjwa huo.

Msangi alisema ugonjwa huo ulisambaa zaidi kutokana na maji ya mito iliyopo wilayani hapa kuwa na vimelea vya kipindupindu hatua iliyoilazimu halmashauri kushirikiana na wataalamu kutoka Idara ya maji kuyatibu maji kwa kutumia dawa mbalimbali kila wakati.

“Lakini pia kulikuwa na changamoto ya wananchi wenyewe kuwa na imani kuwa huenda kitu wanachokiita wao Kidudu mtu ndicho kinasababisha watu kuugua.Hawakutaka kuamini kuwa ni kipindupindu.Wapo waliothubutu hata kuhoji ni kipindupindu gani hiki hata hakiui baada ya kuona idadi ya watu wanaokufa ni ndogo ikilinganishwa na wakati mwingine wakati ugonjwa huu ulipowahi kulipuka”.alisema Msangi

Jioni ya siku hii nilipata wasaa wa kukutana na wakazi katika maeneo mbalimbali ya mji wa Rujewa na nikasikia mengi.Upo uvumi uliosambaa ya kuwepo kwa mkazi mmoja waliyeadi amekuwa akimwaga kinyesi katika Mfereji wa maji yanayokwenda Shambani kwa mwekezaji wa Mbarali Estate.Mfereji ambao maji yake hutumiwa majumbani mwa wakazi wa miji ya Rujewa na ubaruku.Ikasemekana huyu ndiye aliyeueneza.Lakini ukweli wapo pia wakazi waliokuwa wakifua nguo zao kwenye mito iliyopo.

Jioni hii pia nilishuhudi mtu mmoja aliyejitambulisha kama mtaalamu wa afya.Huyu alikuwa akipita katika Baa na maduka ya vinywaji vya viwandani baridi na moto akigawa dawa alizoziita za kuzuia Kipindupindu yeye aliziita Anti Cholela.

Nikiwa na baadhi ya wakazi katika Baa moja iitwayo Igurusi Pazuri jirani na Stendi ya Mabasi ya Rujewa,mtu huyu ambaye wanaonekana kufahamiana naye japo walikuwa wagumu kutaja jina lake alipita na kutugawia vidonge vitatu kila mmoja wetu akisema ndiyo dozi kamili ya kuzuia.Viwili vikiwa vya kijini na kimoja cheupe.Nilipouliza mtaalamu mmoja akanambia vidonge hivyo ni Cypro na docsyren.

Kilichonishangaza mimi ni kuona dawa zikigawiwa hata kwa watu waliokuwa wakinywa pombe kama Bia,Konyagi na Value.Nikajiuliza dawa hii itanywewa wakati gani na watu hawa.Lakini mtoaji ambaye dhahiri naye alionekana kuwa aalikuwa ametumia kilevi kw asana tu hakuwa akitoa maaelekezo ya kutosha.Akaniacha hoi zaidi alipokuwa akiulizaa kama una mtu au watu nyumbani kwako pia unaweza kuwaachukulia.Nikajiuliza dozi hii ni sawa kwa watu wazima na watoto?Sikupata jibu.

Kwa wakati huo Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Mbarali,Francis Mtega alikiri kuwa makatazo ya awali ya upikaji holela vyakula na uuzaji pombe za kienyeji ulisababisha pia ugonjwa huo kuenea zaidi kwakuwa watu walilazimika kwenda kula na kunywa kiuficho katika maeneo yaliyo machafu wakihofia kukamatwa.

Mtega alisema kufuatia hali hiyo baadae,iliilazimu Halmashauri kuja na mpango mbadala wa kuhakikisha watoa huduma za vyakula na vinywaji wanazingatia kanuni za usafi ili waendelea kutoa huduma hizo kwenye maeneo yao kama kawaida.

“Halmashauri bado inaendelea na mikakati ya kuhakikisha ugonjwa huo unatokomezwa kwa kusimamia kanuni za usafi ambapo sasa watoa huduma za vyakula na vinywaji wasiozingatia maelekezo wanawajibishwa kupitia kikosi kazi maalumu kilichoundwa”alisema Mtega. 

Hali ilizidi kuwa mbaya,ugonjwa ukazidi kusambaa maeneo mengine hadi nje ya wilaya ya Mbarali.Septemba Mosi Serikali ya mkoa wa Mbeya ikalazimika kutangaza hali ya hatari.Mkuu wa mkoa Amos Makalla  alisema tayari Kipindupidu kimeripotiwa katika wilaya mbili.Akawataka wananchi kuchukua tahadhari kuzingatia kanuni za usafi kwakuwa baada ya kuripotiwa Mbarali mgonjwa mmoja  pia alibainika wilayani Mbeya.

Katika maeneo na nyakati tofauti,Makalla alisitiza wataalamu wa afya kuwajibika ipasavyo kutoa maelekezo kwa wananchi huku pia akiwataka wananchi watakaoona mgonjwa yeyote kuwa na dalili za kipindupindu kutoa taarifa haraka kwa mamlaka zinazohusika ili ufanyike uchunguzi mara moja.

Aliwataka wananchi kutopuuza suala la uwepo wa ugonjwa huo kwakuwa kutokana na muingiliano wa watu uliopo ni rahisi mno ugonjwa huo kusambaa maeneo mengine zaidi ya ulikobainika hivi sasa.Akasema Serikali inaendelea kuchukua jitihada za dhati kuhakikisha ugonjwa huo unadhibitiwa ili kutoleta madhara zaidi kwa jamii ikiwemo kukwamisha shughuli za uzalishaji mali.

Naikumbuka pia Siku nilipokutana na mkazi wa Nonde jijini Mbeya aliyekuwa akiendelea kupata kinywaji katika moja ya vibanda vilivyopo eneo la Pamodz Uhindini.Japo hakutaka kutaja jina lake lakini alionesha kusikitishwa na hatua ya nyumba yake kuwekewa Karantini siku moja baada ya kubainika kuwepo na mgonjwa wa kipindu pindu.Huyu ni mtoto wa dada yake aliyekuja kumsabahi akitokea Chimala wilayani Mbarali.

“Kwa mara ya kwanza nyumba yangu iliwekewa Karantini,tukazuiwa watu kutoka wala watu wan je ya familia kuja.Binti yule aliyetokea Usangu Chimala huko alikuwa anatapika na kuharisha mpaka baadaye walipomhamishiwa kwenye kambi maalumu.Ilitisha sana majirani na rafiki zangu waliopata taarifa”alisikika mkazi huyo akisimulia watu aliokaa nao.

Ugonjwa huu ukazidi kuitikisa Mbarali.Jitihada za kupambana nao nazo zikaongezeka siku hadi siku.Silaha ya mwisho ikawa ni kuwashirikisha wazee maarufu hasa wa kimila.Kila hali ilipoonekana kuwa mbaya zaidi Serikali ililazimika kupiga marufuku uuzaji vyakula na vinywaji.Ilipoonekana nafuu ikaruhusu.

Oktoba 10 katika maadhimisho ya Siku ya wazee Duniani,ambapo kiwilaya waliadhimisha tarehe hiyo badala ya Oktoba Mosi,Halmashauri ya wilaya ikakiri kushindwa kudhibiti Ugonjwa wa kipindupindu hadi pale walipowashirikisha wazee wakiwemo viongozi wa Kimila.

Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri alisema kwa takribani miezi mitatu ugonjwa huo uliwasumbua na kuwafanya wataalamu kutolala usiku na mchana wakitumia utaalamu wao lakini hawakuweza kufua dafu.Msangi alisema baada ya kuwashirikisha wazee akiwemo kiongozi wa Kabila la Wasangu Chifu Melele wa sasa,kukawa na kila dalili za kukomeshwa kwa kipindupindu wilayani hapa.

“Wataalamu tumehangaika wee ,tumetumia utaalamu wetu lakini wapi!Tumewashirikisha hawa wazee hasa Chifu wetu Melele leo ninapozungumza tuna siku mbili hatuna hata mgonjwa mmoja wa kipindupindu wilayani kwetu”

“Tutazidi kuwashirikisha wazee kwakuwa tunatambua umuhimu wao.Wao wanayajua mambo mengi hivyo tukiwatenga tunaweza kuipoteza jamii yetu” alisisitiza Msangi.

Hatimaye hali imeonekana kuwa shwari,kwani hadi mwishoni mwa Oktoba hakuna mgonjwa mpya aliyebainika kuwa na ugonjwa huu.Hakika Mbarali hawatakisahau kipindupindu cha mwaka huu.

TARURA na matarajio ya ukombozi barabara Mbeya

Mkuu wa mkoa wa Mbeya,Amos Makala akizungumza na wadau mbalimbali wa barabara siku ya uzinduzi wa Tarula mkoa(Picha na Joachim Nyambo)


Na Joachim Nyambo.

MKOA wa Mbeya ni moja kati ya mikoa nchini ambayo tayari imezindua rasmi kimkoa Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini(TARURA).Uzinduzi huu ulifanyika Septemba 9 mwaka huu ikiwa ni baada ya uzinduzi wa wakala huo uliofanyika kitaifa mjini Dodoma.

Kwa mkoani Mbeya ujio wa Tarura unaonekana kuwa sawa na wa mkombozi aliyesubiriwa kwa miaka mingi na sasa amewasili.Shujaa huyu alisubiriwa kwa muda mrefu na wadau mbalimbali mkoani hapa kutokana na changamoto zilizokuwa zikiwakabili katika miundombinu ya usafiri wa barabara.

Changamoto za Uhaba wa miundombinu ya barabara na pia ubovu wa barabara hususani za vijijini zimekuwa zikilalamikiwa kwa miaka mingi kukwamisha maendeleo.Mambo mengi yalikwa si ya kijamii,kisiasa na hata kiuchumi.

Miongoni mwa wadau waliokuwa wamechoshwa na kilio cha barabara hizi ni wakulima.Hawa walishindwa kusafirisha kwa wakati mazao yao kutoka mashambani kuyapeleka mijiji kuliko na masoko.Hapo walijituma kuzalisha kwa wingi mazao lakini uhakika wa kuyafikia masoko haukuwepo.

Mfano mzuri ni uzalishaji wa Mazao ya mifugo hasa maziwa katika wilaya ya Rungwe,Uzalishaji mpunga katika Bonde la Usangu wilayani Mbarali na uzalishaji wa viazi mviringo Mbeya vijijini.Kutokana na kukosekana kwa barabara za uhakika usafirishaji wa mazao haya umekuwa mgumu na kusababisha wakulima au wafanyabiashara wanaoyafuata shambani kupata hasara.
 Kuna wakati mkulima aliyevuna viazi katika vijiji vya Kikondo Mbeya vijijini,Mkulima wa Ndizi vijiji vya Lufilyo Busokelo na Mkulima wa alizeti na ufuta wilayani Chunya alishindwa kusafirisha mazao yake kuyafikisha jijini Mbeya au hata yalipo makao makuu ya wilaya yake kwa kukosa usafiri.Alibaki kusubiri mfanyabiashara mwenye roho ngumu amfikie alipo na hapo ndipo alipokubali pia kunyonywa kwakuwa aliyemfikia ndiye alipanga bei.


Sasa mkombozi wa kweli ameingia.Ni Tarura anayekuja kusimamia barabara na madaraja yaliyopo mijini na vijijini.Huyu ni pacha mwenza wa Wakala wa Barabara nchini(Tanroads) anayeshughulikia barabara za kuunganisha mikoa na wilaya.

Katika Uzinduzi wa Tarura,mkuu wa mkoa wa Mbeya,Amos Makalla alisema ana uhakika kama vile Tanroads wanavyofanya vizuri katika kusimamia ujenzi na ukarabati wa barabara kuu ndivyo Tarura nao watafanya kazi.Kwa matawi haya mawili kufanya shughuli zao  kiuweledi ni dhahiri huduma ya usafiri wa barabara mkoani hapa na Tanzania kwa ujumla utakuwa wenye ubora na kuleta tija kwa kila mdau wa maendeleo katika kipindi cha miaka michache tu ijayo. 
“Sote ni mashahidi,tunaona kila kukicha namna Tanroads wanavyofanya vizuri,wanavyoisaidia Serikali kuunganisha mikoa kwa barabara zinazojengwa kwa kiwango cha lami.Hawa nao watafanya hivyo ninaamini”

“Tunaamini kuwa sasa zile changamoto za fedha kuja lakini tija isionekane kwa barabara zilizojengwa au kukarabatiwa sasa itaondoka.Fedha zinakuja mpaka zinavuka mwaka wa fedha hazijatumika kwakuwa vikao vya madiwani havikukaa nayo hatutoisikia”alisema Makalla.

Kwa kuanzia Makalla aliitaka Tarura kuanza na fedha kiasi cha Shilingi Bilioni 13.2 za miradi ya barabara zinatumika kabla ya kupokea fedha za mwaka wa fedha 2017/2018.Kiasi hiki cha fedha kiliendelea kuwepo katika Halmashauri mbalimbali za mkoani hapa kufuatia kusitishwa kwa miradi yake baada ya kuundwa kwaTarura hivyo kwa sasa fedha hizo zinatakiwa kuiingizwa kwa wakala hiyo ili kazi ziendelee.

Katika uzinduzi huo uliohudhuriwa na Mameneja wa wakala hiyo wa Halmashauri za wilaya zote,wakuu wa wilaya,wenyeviti wa Halmashauri na Wakurugenzi watendaji,Makalla aliitaja Halmashauri ya Wilaya ya Kyela kuongoza kwa kuwa na fedha nyingi zaidi kiasi cha Shilingi Bilioni 5.2 ikifuatiwa na Busokelo yenye shilingi Bilioni 3.8 na Mbeya jiji ina shilingi Bilioni 1.9.

Halmashauri ya wilaya ya Rungwe ina shilingi bilioni 1.6,Mbeya vijijini shilingi milioni 640,Chunya milioni 15.8 na Halmashauri iliyokuwa imetumia fedha zote kabla ya kubadilishwa kwa utaratibu ni ya wilaya ya Mbarali.

Alitaka Tarura kuanza kutumia fedha hizo mara moja kuendeleza miradi iliyokuwa imeanza ili kuharakisha maendeleo ya wananchi kupitia uimarishaji wa miundombinu ya barabara na madaraja.Iwapo wakandarasi walikuwa hawajalipwa sasa walipwe waendelee na kazi ili wazikamilishe haraka.

“Kusiwe tena na sababu ya wakandarasi kutoendelea na kazi.Walipeni kwa kazi walizokuwa wamekamilisha na pia hakikisheni wanaanza kazi au kuendelea na zile zilizokuwa zimesalia.Lengo hapa ni kuharakisha maendeleo ya wananchi”

Aliwataka Watendaji wa Wakala hiyo kuhakikisha wanayapa kipaumbele maeneo yaliyo na changamoto kubwa ya barabara hususani yaliyo na uzalishaji mkubwa wa mazao lakini waananchi wamekuwa wakipata usumbufu kuyasafirisha hadi barabara kuu na kwenye masoko.
 “Huko nyuma mnajua fedha zilizokuwa zikiletwa mpaka zigawanywe gawanywee kwenye kata zinabakia kidogo.Na kuna baadhi ya maeneo fedha hazikuonesha kabisa kuleta matokeo.Hilii ilikuwa kwa sababu kila mmoja alitaka aridhishwe”

Hata hivyo Makalla alisisitiza ushirikiano baina ya Maafisa wa Tarura,Ofisi za wakuu wa wilaya na Halmashauri akisema pande zote bado zinategemeana katika kutekeleza majukumu hivyo ni muhimu kushirikiana lakini kwa kila upande kuheshimu mwingine.

“Msije mkajiona Tarura mmekuwa ninyi ndiyo ninyi mkapandisha mabega juu.Lazima uwepo ushirikiano,mkuu wa wilaya lazima atakuja kukagua miradi kwakuwa ndiye msimamizi wa shughuli zote za Serikali katika wilaya.Madiwani nao lazima watakuwa na ziara za kukagua miradi yenu ili wawaeleze wananchi.Lakini na ninyi mtakuwa na kazi ya kushauri kitaalamu siyo kwakuwa fedha zimekuja basi kila diwani atake baraba inayokwenda kwake ndiyo itengenezwe”

“Wala hapa Halmashauri msilalamike mkasema wamenyang’anya kazi zenu.Na madiwani msione kuanzishwaTarura basi changamoto za barabara kwenye halmashauri zenu hazitofanyiwa kazi.Ainisheni kupitia vikao vyenu wapeni ili waoa waratibu kitaalamu.Hakuna anayefanya la kwake hapa sote tunamlenga mwananchi.Na ndiyo sababu tunawataka Halmashauri mkabidhiane mali na Tarura bila malumbano”

Makalla anasema matokeo makubwa ya Tarura yanatakiwa yalenge kuleta unafuu kwenye maeneo yenye changamoto ya kusafirisha mazao hasa yale yaliyo na uzalishaji mkubwa

“Uzuri Tarura bado watawajibika katika kikao cha bodi ya barabara ambacho ninyi ni wajumbe.Mtawahoji huko na mtawapima.Kikubwa tunataka Tarura ilete mabadiliko ili kuonesha umuhimu na maana ya kuanzishwa kwake.”

Katibu Tawala mkoa wa Mbeya,Marium Mtunguja alizitaka Halmashauri na Watendaji wa Tarura kuzitendea haki Fedha wanazo pelekewa kwaajili ya miradi badala ya kuona ni sifa kubaki nazo mpaka mwaka wa fedha unamalizika.

“Siyo sifa kubaki na fedha nyingi za miradi wakati wananchi wanapata shida.Ni bora ubakiwe na sifuri lakini kazi ziwe zilifanyika.Jitahidini kutumia fedha kwa kazi zilizokusudiwa.Msione fahari kuziona fedha kwenye akaunti zenu.”anasema Mtunguja.

Mratibu wa Tarura mkoa wa Mbeya,mhandisi Danstan Kishaka,aliwataka mameneja wa wilaya wa wakala hiyo kutambua kuwa kuondolewa kwao katika Halmashauri kunalenga kuboresha kazi hivyo mahitaji ya Serikali ni kuona Utekelezaji wa miradi ya barabara sasa unakuwa wa kiwango kinachohitajika.

“Tunatakiwa tuwe Tai wapya wenye kuona mbali katika kuwatumikia wananchi.Hatupaswi kujenga kiburi na sote tunajua huku hakuna kuazimiwa huku ukiharibu ni barua moja kwa moja hivyo lazima tutambue kuwa tupo kuhakikisha Ilani ya Chama Cha Mapinduzi inatekelezwa kupitia Barabara.Na lazima kwakuwa tutaendelea kutumia ofisi za Halmashauri kwa muda unapotoka nje ya kituo lazima mkuu wa wilaya yako na Mkurugenzi wajue”alisema Kishaka.

Wenyeviti wa Halmashauri za wilaya mkoani hapa wanasema Tarura imekuja kwa wakati muafaka kwani itapunguza mivutano iliyokuwepo baina ya madiwani na kusababisha pesa iliyotengwa kutoonesha tija.

“Madiwani walikuwa wanabeba mzigo mzito.Ilikuwa hata zikija shilingi laki tano inabidi wazigawane,ili kila mmoja aonekane alifanya kitu kwa watu wake.Muhimu hapa msianze na fedha,anzeni na kuzijua barabara ninyi ni wataalamu lakini wanaozijua barabara ni wananchi,hakikisheni mnawafikia huko waliko.”alisema Mwenyekiti wa wenyeviti wa Halmashauri za mkoani hapa Anyosisye Njobelo ambaye pia ni mwenyekiti wa Halmashauri ya Busokelo.

“Lakini imefika pia wakati tuachane na wimbo wa kupata taarifa kwenye makaratasi,tunataka kuona barabara.Kilio cha wananchi ni kupunguziwa mzigo wa gharama kubwa ya kusafirisha mazao toka mashambani”aliongeza.

Chalya Julius ni mwenyekiti wa wakuu wa wilaya mkoani hapa,anasema “Sote tunaamini Tarura ni chombo kilichopewa jukumu kwa niaba ya serikali hivyo yote yaliyoamriwa yatatekelezwa”

“Wakuu wa wilaya tutatoa ushirikiano wa kutosha na pia kusimamia mashirikiano baina ya Tarura na Halmashauri.Zaidi tutasimamia viwango vya kazi za barabara”alisema Julius ambaye pia ni mkuu wa wilaya ya Rungwe.

Baadhi ya wananchi kutoka maeneo ya pembezoni,wanasema wanachosubiri ni matokeo chanya na si ubabaishaji.Wanasema kujengwa na kukarabatiwa kwa barabara maeneo ya pembezoni kutainua kipato chao na pia kutarahisisha upatikanaji wa huduma muhimu za kijamii zikiwemo za Afya.

“Watu wanajituma kuzalisha mazao ya chakula na biashara kwa wingi lakini wanakatishwa tama na uhaba wa masoko.Tunaamini hata wawekezaji wanaogopa kuja kuwekeza viwanda maeneo ya pembezoni kutokana na miundombinu duni ya barabara”alisema Mkazi wa Lwangwa Busokelo,Neva Matinya. 

KATIBU WA CHADEMA KANDA YA NYASA ATIMKIA CCM

ALIYEKUWA katibu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) wa chama hicho wa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini (Nyasa), Frank Mwaisumbe ametangaza kujiondoa katika chama hicho na amepanga kujiunga na Chama cha Mapinduzi (CCM) wakati wowote kuanzia sasa.

Mwaisumbe aliyeshika wadhifa huo kwa miaka sita kabla hajauachia kwa hiari yake mwenyewe Januari mwaka huu amesema atajiunga na CCM kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Rais Dk John Magufuli za kufufua uchumi wa nchi.

“Safari yangu ya kisiasa ndani ya Chadema kwa kipindi chote nilichokuwa huko imekoma leo, sasa naona nahitaji kuungana na watanzania wenzangu kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya tano na kazi zake zote zinazolenga kuleta maendeleo ya Taifa,” alisema.

Akizungumzia tafsiri potofu ya baadhi ya watu wanaoamini kila anayetoka upinzani na kwenda CCM amenunuliwa, Mwaisumbe alisema; “Kwanini CCM waninunue, sina hakika kama CCM wananihitaji kwa kiwango cha kuninunua lakini nisema mimi binafsi ndiyo ninayeihitaji CCM kwahiyo nakwenda kwa hiari yangu mwenyewe.”

Mwaisumbe ambaye kitaaluma ni mchumi alisema ameisoma vizuri Katiba ya CCM na atakapokuwa mwanachama wake, atatimiza wajibu wake kama inavyotakiwa kufanywa na mwananchama mwingine yoyote.

Mwaisumbe ametangaza uamuzi huo leo katika hoteli ya Ambassador mjini Iringa ikiwa ni siku moja tu baada ya aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Lawrance Masha kutangaza kurejea CCM baada ya kujiondoa Chadema aliyoitumikia kwa miaka miwili.

Na wakati chama hicho mjini Iringa kikiwa katika maandalizi ya kumpokea Mwenyekiti wa Taifa, Freeman Mbowe anayekuja kuongeza nguvu katika kampeni za uchaguzi mdogo wa udiwani kata ya Kitwiru.

Wakati Chadema wamemsimamisha Bahati Chengula katika uchaguzi huo, CCM wamemsimamisha Baraka Kimata, diwani wa zamani wa kata hiyo aliyechaguliwa mwaka 2015 kupitia Chadema kabla hajajitoa na kujiunga na CCM hivikaribuni.

Pamoja na pigo hilo Chadema jimbo la Iringa Mjini imepoteza madiwani wengine watatu kwa nyakati tofauti hivikaribuni, wawili wakiwa ni wa viti maalumu na mmoja wa kata ya Kihesa ambao kwa pamoja walijiunga na CCM wakati chama hicho kikizindua kampeni zake udiwani katika kata hiyo, shughuli iliyohudhuriwa na Katibu wa Itikadi na Uenezi Taifa, Humphrey Polepole.