Na Joachim Nyambo.
WAHENGA walinena hakuna lililo na mwanzo likakosa kuwa na
mwisho!Mateso yaliyowasibu wakazi wa kijiji cha Kapunga sasa yamefikia
ukomo.Miaka 10 ya misukosuko baina yao na mwekezaji kampuni ya Kapunga Rice
inayoendesha shughuli zake chini ya kampuni mama ya Expot Trading ilikuwa mwiba
kwa wakazi hawa.
Mgogoro baina ya pande hizo mbili umemalizika baada ya
serikali kusikia kilio cha wananchi.Sasa mgogoro wa kimpaka uliodumu kwa zaidi
ya miaka 10 umemalizika kwa mwekezaji kuridhia kiasi cha hekta 1,870 za ardhi kurejeshwa kwa kijiji hicho.
Waziri wa Ardhi,Nyumba
na Maendeleo ya Makazi Willium Lukuvi mapema mwezi jana alitangaza kurejeshwa
kwa hekta hizo za ardhi kwa nyakati tofauti alipozungumza na wakazi wa kijiji
cha Kapunga kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kijijini.Alizungumzia pia
jambo hilo alipokuwa kwenye kikao na madiwani na watendaji wa halmashauri ya
wilaya ya Mbarali.
“Rais John Pombe Magufuli ameamua
kuwapa zawadi ya mwaka mpya wakazi wa Mbarali.Zawadi yenyewe ni kutekeleza
kabla ya kutimiza siku mia moja za utawala wake ahadi aliyowaahidi wakazi wa
Kapunga ya kutatua mgogoro wa kimpaka kati yenu na mwekezaji wa shamba la
Kapunga aliyoitoa wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu” alisema Lukuvi.
Alisema serikali imekubaliana na
mwekezaji kurejesha kipande cha ardhi cha hekta 1,870 kwa wakazi wa kijiji
cha Kapunga walichokidai kwa zaidi ya miaka kumi huku viongozi wengi wakiika
kijijini hapo na kushindwa kufikia suluhisho la mgogoro.
Lukuvi alisema tatizo lilianzia
mwaka 2005 wakati mwekezaji alipobinafsishiwa shamba kwani vipimo alivyopewa
vilikuwa tofauti na uhalisia wa eneo lililokuwa likimilikiwa na serikali kama
shamba la Kapunga.
Alisema tayari wamezungumza na kampuni
husika iliyobinafsishiwa shamba hilo kwa mkataba wa umiliki wa miaka 99 ambayo
tayari ilikwisha chukua mkopo benki kwa kutumia hati miliki ya ardhi
hiyo.
“Tumekaa na kukubaliana,kiasi hiki
cha ardhi kirejeshwe kwenu na mwekezaji amekubali.Ili kuwasaidia pia
wawekezaji tumezungumza na watu wa benki waliyochukua mkopo na tumekubaliana
kiasi cha mkopo kinachotokana na kiasi cha ardhi tunachokiondoa irejeshewe ili
wasiendelee kumtoza mwekezaji” alisema Lukuvi hali iliyosababisha wakazi wa kijiji
hicho kupiga mayowe na vigelegele kwa furaha.
“Awali hakukuwa makosa kwa serikali
kulitumia shamba la Kapunga kwakuwa ardhi yote ni mali ya serikali.Nafco
alikuwa mtoto wa serikali kwahiyo hakukuwa na tatizo kutumia ardhi hii.Makosa yalikuja
kufanyika wakati shamba linabinafsishwa kwa kwekezaji.Hilo tumeliona na ndiyo
sababu leo tumeridhia kurejesha ardhi yenu”
Lukuvi aliwaambia wakazi hao ambao
muda wote akihutubia waliridhia kusimama wakinyeshewa mvua kuwa hekta hizo sasa
ni mali ya kijiji chao na tayari wataalamu wa wizara yake wapo kijijini hapo
na wanaendelea na utaratibu wa kutengeneza upya mipaka kati ya eneo la kijini
na lile la mwekezaji ambalo sasa linabakiwa na hekta zisizopungua 5000.
Aliwataka wakazi wa kijiji
hicho kutoa ushirikiano wa kina kwa wataalamu wanaofanya shughuli hiyo sambamba
na kupendekeza umiliki wa ardhi iliyorejeshwa kwao ili watakao miliki wapewe hati miliki.
“Hakikisheni mnashiriki kuweka
mipaka hii.Mshirikiane pia kuona namna gani inafaa kwa umiliki wa eneo hilo ili
muweze kuwa na hati miliki.Hii itawezesha pia serikali kunufaika kwakuwa
mtatakiwa kulipia kodi.Maana pasipo kuwa na hati ni wazi kuwa na serikali nayo
inakosa haki yake”
Alipendekeza vijana kupewa
kipaumbele wakati wa mgawanyo wa ardhi hiyo akisema kundi hilo ndilo
linalokabiliwa na changamoto kubwa ya ukosefu wa ardhi
kutokana na ongezeko la wakazi.
“Siwezi kulazimisha kuwa wapewe
vijana,lakini nashauri kipaumbele kikubwa kiwe kwao kwakuwa ni kundi lisilo na ardhi
ya kumiliki.Wakati mkifanya mchakato wa kugawa au kutengeneza namna ya umiliki
wa ardhi hii basi jaribuni na kulitafakari hili kwa kina”
Waziri huyo alionya kutokuwepo kwa
upendeleo katika ugawaji na umiliki wa ardhi hiyo akisema yawezekana wajanja
wachache wakataka kujinufaisha kupitiaa nyadhifa zao jambo alilosema
likibainika litafuatiliwa kisheria.
“Tusije kusikia kuna mtu kapewa
ardhi kutokanan na kitambi chake au nafasi yake.Mkasababisha wakubwa wachache
wakaneemeka na walalahoi wakabaki wakiona kwa macho tu ardhi yao ikiwanenepesha
wachache.Na ninyi maafisa tukisikia mna mgawo wenu hapa lazima tutachukua hatu.”alisisitiza
Lukuvi.
Hatua hii ya kurejeshea kipande cha
ardhi yao ni faraja kubwa kwa wakazi wa kijiji cha kapunga.Wanajua sasa ukomo
wa mateso na manyanyaso umefika.Furaha yao inaongezeka mara dufu pale
wanapowaza kuwa sasa kijiji chao kiko salama kwakuwa ilikuwa kiondolewe kwani
kilikuwa kikitajwa kuwa sehemu ya eneo la mwekezaji.
Mafanikio haya yenye kuonesha uwepo
wa serikali sikivu na yenye kuwajali watu wake hayaishii kuwafurahisha wakazi
wa Kapunga pekee.Wadau mbalimbali wakiwemo wanahabari wanafurahia hatua hii.Hii
ni kwakuwa walishiriki katika kutetea ardhi hiyo.Waliujulisha umma mateso
waliyokuwa wakiyapata wakazi wa kijiji hiki kutoka kwa mwekezaji
Hata hivyo unapozungumzia mafanikio
haya kamwe huwezi kuwasahau wada mbalimbali waliowezesha kuyafikia.Hawa ni
pamoja na viongozi mbalimbali akiwemo aliyekuwa mkuu wa mkoa wa Mbeya John
Mwakipesile,aliyekuwa mkuu wa wilaya ya Mbarali,Luteni Cosmas Kayombo na
wengine wengi.Mara kadhaa viongozi hawa walijaribu kutafuta suluhu ya mgogoro
huu wakiwa wao wenyewe au kushirikiana na viongozi wa ngazi za juu.
Viongozi waliopo madarakani kama
Mkuu wa mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro na mkuu wa wilaya ya Mbarali Gullamhussein
Kifu hawatosahaulika katika historia ya kijiji cha Kapunga.Wamekuwa mstari wa
mbele na kuwezesha mgogoro huu kupatiwa ufumbuzi.
Uwepo wa rais Dk John Magufuli
madarakani utabaki kukumbukwa na wakazi wa kijiji hiki.Aliwaahidi kutatua mzozo
wao akiwa kwenye kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.Amewatekelezea ahadi
hiyo akiwa hata hajatimiza siku 100 madarakani.Yeye anaiita zawadi ya mwaka
mpya kwa wakazi wa Kapunga.
Wapo wakazi wengi waliokuwa
wamekwishaanza kukata tama.Wakiamini mgogoro huo hautakuja pata ufumbuzi.Hii ni
kutokana na kudumu kwa muda mrefu huku wakijionea danadana zilizokuwa zikipigwa
na viongozi wengi waliofika kijijini hapo.
Wakazi wa kijiji hiki wanasema
kurejeshea ardhi ni hatua ya kwanza.Wanahoji kwakuwa serikali imekiri makosa
yalifanyika wakati wa kubinafsisha shamba la Kapunga ni nini hatma ya wananchi
waliopata hasara kutokana na hasira za mwekezaji.
Katika mkutano wao na waziri Lukuvi
wakazi hao walihoji ni nani anayepaswa kuwajibika kwa hasara walizopata.Wapo
waliobomolewa nyumba zao na viwanja vyao vikatumika kujenga uwanja wa ndege wa
mwekezaji,wapo waliobomolewa tofali walizokuwa wamefyatua na kuzichoma
wakisubiri kujenga.Zipo familia zilizopoteza wapendwa wao kwa kusombwa na maji
baada ya mwekezaji kubomoa madaraja.
Hili bado ni swali lisilopatiwa
majibu.Kwa kuwa makosa yalifanyika wakati wa kuuza shamba wanakijiji wanaona ni
wazi yupo mtu anayepaswa kuwajibika katika kulipa fidia ya hasara
waliyoipata.Hii itaongeza ushirikiano baina yao na mwekezaji ambaye sasa
anabakiwa na kipande cha ardhi kilicho halali.
Nawatakia kila la kheri
wakazi wa Kapunga katika maisha yao mapya kwenye ardhi yao halali.Muhimu kwao
ni kukumbuka ardhi waliyorudishiwa isije ikawaingiza kwenye migogoro mingine ya
wao kwa wao.Umakini katika kupanga matumizi sahihi ya ardhi hiyo unahitajika.Ni
wakati pia kwao kukaa na mwekezaji na kumaliza tofauti zao.Hii itadumisha udugu
baina yao na kuishi maisha ya furaha wakiwa majirani wenye kupendana.
MWISHOOOO