Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Monday, February 15, 2016

MAISHA YA MATESO KIJIJINI KAPUNGA-3

Na Joachim Nyambo.

JANUARI 12 hadi 14 mwaka 2012 zilikuwa tarehe nyingine za majonzi kwa wakazi wa Kapunga.Kwa kutumia ndege ya kunyunyizia dawa mwekezaji wa katika shamba la Kapunga ambapo alimwaga sumu katika mashamba ya wakulima wadogo yaliopo jirani na eneo lake.Zaidi ya wakazi 150 wa Kijiji cha Kapunga waliathirika na tukio hilo.


Meneja wa shamba hilo Walder Vermaak, Afisa ugani Serger Bekker na Rubani wa ndege Andries Daffe walitajwa kushiriki ukatili huo kwa kuharibu mazao ya wakulima hekari 489.5.Hii iliongeza kilio na masikitiko makubwa kwa wakazi wa kijiji hiki.Wengi wakajiuliza hivi kweli nia ya Baba wa taifa hili ilikuwa ni kuona wananchi tunatokwa machozi katika ardhi yetu kila kukicha.

Licha ya kuharibiwa kwa mazao pia wapo wananchi waliodhurika na sumu iliyonyunyiziwa kwenye mashaamba. Baadhi ya wananchi walioathiriwa na sumu hiyo wakati ndege ikimwaga mashambani na kushuhudiwa ni pamoja na Michael Shija, Severina Mbwilo, Elikana Nsemwa, Edward Simkoko, Gaidon Peter Ngogo (54), Jailo Esau (22), Jackson Mwandemange  (52), Catherina Shipela (50), Edda Ngosha (35), Julius Isega(50), Ramadhan Nyoni (52).Wengi kati yao walidhurika kwa kuharibika ngozi za miili yao hususani miguuni na mikononi.Wengi pia walikumbwa na hili walipokuwa wakishuhudia unyunyiziaji wa sumu hiyo.Hawakuwa na la kufanya ili kuzuia hili.


Shukrani kwa vyombo vya dola,vikaweza kusikia kilio cha wananchi na kuchukua stahiki dhidi ya watuhumiwa. Meneja wa shamba Walder Vermaak, Afisa ugani Serger Bekker na Rubani wa ndege Andries Daffe wakafikishwa mahakamani.

Hatua ya kufikishwa mahakamani kwa Mwekezaji wa shamba la la Kapunga Rice Project yaani Kampuni ya Export Trading Group ikachukuliwa na wakazi wilayani hapa kama mwanzo wa kufikiwa muafaka wa matukio yanayokiuka haki za binadamu ambayo walikuwa wakitendewa na mwekezaji huyo.

Baadhi ya wakazi katika kijiji cha Kapunga kilicho na jumla ya vitongoji saba wakanambia hatimaye serikali imeanza kujionea mahusiano yasiyoridhisha baina ya mwekezaji na wakazi wa maeneo jirani.Hata hivyo wakazi hao wakaiomba serikali kuyaangalia kwa kina malalamiko mengine ambayo walikuwa wakiyawasilisha katika ngazi mbalimbali za serikali wakimtupia lawama mwekezaji huyo lakini yalikuwa yakipuuzwa.

Mmmoja wa wakazi hao Elia Sanga alisema kuwa kufikishwa mahakamani kwa mwekezaji huyo kunadhihirisha uongozi wa serikali katika ngazi za Wilaya na Mkoa kuanza kuyafanyia kazi malalamiko ya wakazi hao.
Februari 14 mwaka 2012 ndipo Mwekezaji huyo apofikishwa katika mahakama ya wilaya ya Mbeya akishitakiwa kwa makosa mawili tofauti.Kosa la kwanza ni kula njama ya kutenda kosa la kuharibu mali na la pili kuharibu mali za wananchi kwa hila.


Ilielezwa mahakamani hapo kuwa makosa hayo yaliyafanywa  Januari 12 hadi 14, mwaka huu kwa kutumia ndege ya kunyunyizia dawa ambapo alimwaga sumu katika mashamba ya wakulima zaidi ya 154 wa Kijiji cha Kapunga wilayani humo.

Akisoma mashitaka hayo mbele ya Hakimu wa mahakama hiyo Seif Kulita, Mwendesha mashitaka wa Serikali Griffin Mwakapeje alisema kuwa washitakiwa hao akiwemo Meneja wa shamba hilo Walder Vermaak, Afisa ugani Serger Bekker na Rubani wa ndege Andries Daffe walitenda kosa hilo wilayani humo na kuharibu mazao ya wakulima hekari 489.5.

Mwakapeje alisema kuwa wawekezaji hao wote kwa pamoja walitenda kosa hilo kinyume na sheria namba 226 (i) cha marekebisho ya sheria ya mwaka 2002 la kuharibu mazao hayo ya Mpunga wa wakulima wanaolima eneo linalojulikana kwa jina la Mpunga moja.

Baada ya mashitaka hayo, Hakimu Kulita alpowauliza washitakiwa hao wote kwa pamoja walikana shitaka hilo ambapo wakili aliyekuwa akiwatetea washitakiwa hao Ladislaus Rwekaza aliomba dhamana kwa wateja wake na hatimaye mahakama ikaridhia kwa Masharti ya kila mtuhumiwa kuwa na mdhamini mmoja mweye mali isiyohamishika isiyopungua Shilingi Milioni kumi.

Aidha Hakimu huyo alitoa sharti kwa washitakiwa hao kuwa mbali na sharti la kuwa na mdhamini mmoja na mali isiyohamishika pia watuhumiwa waliytakiwa kukabidhi hati za kusafiria na kwamba hawapaswi kusafiri nje ya mkoa wa Mbeya na kama watahitaji kusafiri nje ya mkoa wa Mbeya ni lazma wapate kibali cha mahakama hiyo ambapo washitakiwa walitimiza masharti hayo.

Hapo ndipo washitakiwa hao walidhaminiwa na Uwesu Msumi mkazi wa Jijini Dar Es Salaam ambaye aliikabidhi mahakama hiyo hati ya nyumba yenye namba 229 Block J iliyopo Mbezi Jijini Dar es Salaam, Christian Basil Mmas aliyekabidhi hati ya nyumba yenye namba 109 iliyopo Geza Ulole Jijini Dar es Salaam na Sunnil aliyetoa hati namba 254 iliyopo Kigamboni Jijini Dar es Salaam pia na kesi ikaahirishwa hadi Machi 6, mwaka huo ilipotarajiwa kutajwa tena.

Hata hivyo wakazi wa Kapunga wanasema shitaka hilo limedumu kwa muda mrefu mahakamani pasipo kumalizika.Waliwahi  kushauriana na uongozi wa kampuni husika kuona uwezekano wa kuliondoa shauri hilo mahakamani ili wakae na kukubaliana nje ya mahakama.Hii ilitokana na nia iliyooneshwa na mwekerzaji ya kukiri makosa ya kuharibu mazao.

Mbele ya waziri wa Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya makazi Willium Lukuvi Mapema Januari mwaka huu wakazi hao walisema iwapo mwekezaji yuko tayari wanaweza kuliondoa shauri hilo mahakamani ili walizungumzie nje.Wazo hilo lilinaonekana kukubalika pia na mwekezaji.

Akizungumza kwenye mkutano aliowajulisha wakazi hao kurejeshwa kwa kijiji hekta 1,870 zilizoporwa awali na kuingizwa kwa mwekezaji,waziri Lukuvi alisema ni jambo jema iwapo wataondoa shitaka mahakamani na kulizungumzia nje ya mahakama ili kuweka wigo mpana wa kulijadili.Alimtaka mbunge wa jimbo la Mbarali Haroun Pirimohamed kushiriki katika kutafuta ufumbuzi wa suala hilo.

Kwa upande wake Pirimohamed aliahidi kushirikiana na pande zote mbili sambamba na mahakama kuondoa shitaka hilo mahakamani.Aliahidi kuhakikisha mgogoro baina ya pande hizo mbili kumalizika nje ya mahakama akijigamba kuwa pande hizo zote anazimudu.

“Babu yangu aliwahi kunambia kuwa shitaka linapokuwa mahakamani ni sawa na watu wawili wanagombania Ng’ombe mmoja ambapo mmoja kati yao anavuta pembe huku mwenzie akivuta mkia lakini wote wawili wanajisahau kuwa wamemsahau mtu katikati ambaye anamkamua ng’ombe huo pasipo kubughudhiwa” alisema Pirimohamed kwenye mkutano uliowakutanisha waziri Lukuvi,Mkuu wa mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro,Mkuu wa wilaya ya Mbarali Gulamhussein Kifu na watendaji wengine wa mkoa na wilaya.

........................ITAENDELEA KESHO...................

No comments:

Post a Comment