Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Wednesday, December 30, 2015

MWILI WA MCHIMBAJI MWINGINE MGODI WA DHAHABU WAPATIKANA



HATIMAYE shughuli ya kutafuta miili ya wachimbaji wadogo waliofukiwa na kifusi kwenye mgodi wa dhahabu wa Mnadani kata ya Sangambi wilayani Chunya imemalizika jioni hii baada ya mwili wa mchimbaji wa pili kupatikana.

Mwili uliokuwa umesalia kwenye kifusi hicho ni wa mchimbaji Riziki Kalengo mkazi wa wilayani Mbozi mkoani Mbeya ambapo hadi unaopolewa leo majira ya saa 11 kasoro za jioni ulikuwa na siku ya nne tangu wachimbaji hao wafukiwe na kifusi Disemba 27 mwaka huu wakiwa wawili.

Akizungumza na Lyamba Lya Mfipa kwa njia ya simu kutoka eneo la tukio mara baada ya kupatikana kwa mwili huo mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Chunya,Bosco Mwanginde amesema mwili wa marehemu Riziki umepatikana kufuatia juhudi kubwa zilizofanywa na wadau mbalimbali wakiwemo wachimbaji na wakazi wa vijiji jirani.

Mwanginde amesema kutokana na miamba iliyokuwa imefunika shimo la mgodi huo katika kina kirefu,ilikuwa vigumu shughuli ya ufukuaji kifusi kuendelea kufanywa na mashine na hapo ndipo ikawalazimu wananchi kutumia zana za  kawaida zikiwemo chepe,majembe na sururu.

Amesema tayari miili yote ya marehemu wawili ukiwemo ule wa Wambura Makulu mkazi wa Musoma Mkoani Mara ulioopolewa siku ya jumanne imekabidhiwa kwa ndugu na jamaa tayari kwa kuanza safari ya kuelekea makwao kwaajili ya maziko.

Bwana alitoa na Bwana ametwaa,jina la Bwana na Libarikiwe!

WATATU MBARONI KWA KUMUOZESHA BINTI KWA KIKONGWE



DAWATI la jinsia na watoto la jeshi la polisi wilayani Nkasi mkoani Rukwa linawashikiliwa watu watatu wakazi wa kijiji cha mkole kwa kosa la kumlazimisha mtoto wao wa kike wa miaka 18 kuolewa na Mwanaume wa miaka 72 baada ya kutoa mahali ya ng’ombe 8 na shilingi 100,000.

Akizungumza binti huyo( Jina linahifadhiwa) mbele ya dawati hilo alisema kuwa wazazi wake walichukua mali kwa mzee Edward Muscat (72) Ng’ombe 8 Tshs,100,000 bila kumshirikisha na kuamua kumlazimisha kwenda kuolewa na mzee huyo ambaye kiuhalisia ni Babu yake.

Alisema kuwa yeye baada ya kuambiwa na wazazi wake ya kuwa akaolewe na mzee huyo alikataa na ndipo walipomlazimisha kwenda kwa nguvu kwa mzee huyo ambapo aliishi naye kindoa kwa muda wa siku Nne na ndipo alipotoroka na kukimbilia polisi.

Alisema yeye kila akirudi nyumbani wazazi wake hao umfukuza na kumalazimisha mtoto huyo kwenda kwa mmewe huyo kwa madai kuwa walishapokea mali hivyo ni lazima aolewe na mzee huyo.

Baba wa mtoto huyo Mboje Saguda baada ya kumhoji juu ya tukio hilo akiwa mikononi mwa polisi sambamba na mkewe alikiri kupokea mali hiyo kutoka kwa mzee huyo na kuwa wao hiyo kwao ni mila wala siyo tatizo.

Na alidai kuwa mtoto wao huyo licha ya kukataa kuolewa na mwanaume huyo ilikua ni lazima aolewe ili kukidhi matakwa ya mila yao ya kabila la Wasukuma.

Mwenyekiti wa dawati la jinsia na watoto wa wilaya Nkasi Anna Kisimba alisema wazee hao wamekwenda kinyume na haki za binadamu na kuwa hivyo ni vitendo vya kikatili dhidi ya mtoto wa kike na kuwa hivi sasa wanaandaa mashitaka ya kuwafikisha mahakamani watuhumiwa wote watatu ya kumdhalilisha mtoto wa kike.

Alisema wazee hao mume na mke ikiwa ni pamoja na muoaji wametenda kosa la jinai kumlazimisha binti mdogo kuolewa na Babu kwa lazima,na kuwa licha ya kwamba binti huyo kwa umri aliofikia ni halai kuolewa lakini si katika mazingira ya kulazimishwa kwa tamaa ya mali na kuwa suala la kuoa ama kuolewa ni la hiari hivyo ni lazima kila mmoja akubali kwa dhati kutoka moyoni mwake.

Mkuu wa polisi ( OCD) wilayani Nkasi Cyprian Mushi alikiri jeshi lake kuwashikilia watu hao kwa maana wazazi wa binti na muoaji kwa kwenda kinyume na haki za binadamu na kuwa ni kitu ambacho hakikuballiki kuoana kwa kutofautiana umri kwa mbali kiasi hicho hata kama wamekubaliana.

Amesema kuwa kosa kubwa kwa watuhumiwa hao ni kitendo cha kumlazimisha binti ambaye kimsingi ana maamuzi yake na hilo lote ni shinikizo litokanalo na tamaa ya mali iliyopelekea kumdhalilisha binti huyo kijinsia,na kuwa upelelezi umekamilika kuanzia sasa watafikishwa mahakamani kujibu yuhuma hizo.

Na Israel Mwaisaka,Nkasi

KILIMO CHA KISASA KISICHOHITAJI ARDHI KUBWA



Mgomba una uwezo mkubwa wa kuhifadhi maji.Hii inaweza kuwa faida kubwa kwa wakulima wa mboga mboga.Toboa matundu katika shina la mgomba uliokatwa kama inavyoonekana katika picha hapo juu,weka udongo wenye mchanganyiko na mbolea kwenye matundu hayo na kasha na kisha pandikiza miche yako.

MWILI WA MCHIMBAJI MMOJA WAFUKULIWA KWENYE KIFUSI CHUNYA

JITIHADA za kuokoa wachimbaji wawili waliofukiwa na kifusi katika machimbo bubu ya dhahabu yaliyopo eneo la mnadani kata ya Sangambi, wilayani Chunya zimeendelea tena jana jumanne(Disemba 29) na hatimaye kuzaa matunda kwa mmoja wa wakichamji hao kuopolewa akiwa amefariki dunia. 

Wachimbaji madini hao walifukiwa na kifusi tangu Disemba 27 mwaka huu majira ya asubuhi na shughuli ya kufukua kifusi ili kuwaokoa ikaanza Disemba 28 majira ya asubuhi baada ya mashine ya  kufukua kifusi kupatikana. 

Hata hivyo kutokana na gari lenye mashine hiyo kutokuwa na taa ililazimu shughuli hiyo kusitishwa ilipofika juzi jioni na kiza kuanza kutanda hivyo shughuli hiyo ikaendelea tena jana Disemba 29. 

Akizungumza na Lyamba Lya Mfipa kutoka eneo la tukio,mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Chunya Bosco Mwanginde amesema jitihada za ufukuaji kifusi zilianza kuzaa matunda majira ya saa nane mchana baada ya wananchi waliokuwepo kufanikiwa kuopoa mwili wa mmoja wa wachimbaji hao. 

Mwanginde amemtaja marehemu ambaye mwili wake uliopolewa jana kuwa ni Wambula Makulu mwenyeji wa Musoma mkoani Mara aliyesema alihamia maeneo hayo miaka kadhaa iliyopita.

Mwanginde amesema pamoja na kuukuta mwili huo shughuli ya kufukua kifusi iliendelea kwa lengo la kumtafuta mchimbaji mwingine aliyemtaja kwa jina la Riziki Kalengo mkazi wa wilayani Mbozi japo pia jioni shughuli hiyo ilisimama na imeendelea leo asubuhi.

Monday, December 28, 2015

WACHIMBAJI WADOGO WAHOFIWA KUFA BAADA YA KUFUKIWA NA KIFUSI

WACHIMBAJI wadogo wawili ambao majina yao hayajafahamika mara moja wanahofiwa kufa baada ya kufukiwa na kifusi kwenye machimbo bubu ya dhahabu yaliyopo eneo la mnadani kata ya Sangambi, wilayani Chunya.

Wakazi wa kata hiyo wanasema wachimbaji hao walifukiwa na fikusi wakiwa kazini Desemba 27, mwaka huu majira ya asubuhi.

Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Chunya,Bosco Mwanginde alisema wachimbaji hao walikuwa sita na wakati wakiendelea na shughuli ya uchimbaji ndipo kifusi kiliwafukia wawili kati yao.

Mwanginde alisema awali kulikuwa na madai kwamba watu watatu ndio waliofukiwa na kifusi hicho, lakini baadaye ikathibitika kwamba waliofukiwa ni wawili kati ya hao sita.

Alisema mara baada ya kutokea kwa tukio hilo, alimfikishia taarifa Mkuu wa mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro, ambaye alifika jana(Desemba 8) eneo la tukio na kuongoza kazi ya kuokoa watu hao, akiwa pamoja na Mkuu wa wilaya ya Chunya, Elias Tarimo.

“Nilitoa taarifa kwa Mkuu wa mkoa, na nikaanza kufanya jitihada za kutafuta magari yenye mtambo wa kufukua (Tingatinga ).Ilikuwa vigumu kwakuwa gari za aina hiyo zilikuwa mbali.Nilifanikiwa kupata moja kutoka kwa Mehrab, ambalo ilikuwa mbali hivyo nayo imekuja leo (Jana) saa 12:00 asubuhi kazi ya kufukua kifusi ikaanza” alisema Mwanginde.

Mwenyekiti huyo wa halmashauri, alisema hadi saa 11:00 jioni ya desemba 28 wakati akizungumza na Lyamba Lya Mfipa kwa njia ya simu,shughuli ya kufukua kifusi ilikuwa ikiendelea.

Hata hivyo Mwanginde aliwataka wachimbaji wilayani humo kuchukua tahadhari, wanapoingia kwenye mashimo ya migodi machimboni hapo hasa katika kipindi hiki cha mvua zinazoendelea kunyesha.

Kwa upande wake Diwani wa kata ya Sangambi, Junjulu Mhewa, alisema alipata taarifa za vijana hao wawili kufukiwa na kifusi, ambapo alitoa taarifa kwenye uongozi wa wilaya, ambapo walifika eneo la tukio asubuhi lakini jitihada za kuwaokoa zilishindikana.

Naye Kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya,Ahmed Msangi, alisema taarifa za kufukiwa kwa wachimbaji hao, zilifahamika baada ya mmoja wa wachimbaji kuingia mgodini na kusikia sauti za watu wakiomba msaada wa kuokolewa na kubainisha kuwa shughuli ya kufukua kifusi inaendelea.

YANGA YAMTIMUA NIYONZIMA RASMI

Uongozi wa Yanga, umetangaza kuvunja mkataba wake na kiungo wake Haruna Niyonzima.
Yanga imechukua uamuzi huo ikiwa ni miezi isiyozidi mitano tokea isaidi mkataba mpya wa miaka miwili na Niyonzima.

Msemaji wa Yanga, Jerry Muro amesema Niyonzima atalazimika kulipa kiasi cha dola 71,175 (zaidi ya Sh milioni 149) kutokana na kukiuka mkataba uliosababisha kuvunjika kwa mkataba huo.

Mzozo wa Yanga na Niyonzima ulianza baada ya kiungo huyo kuchelewa kurejea kazini alipokwenda kuitumikia timu yake katika michuano ya Chalenji nchini Ethiopia.

Uongozi wa Yanga ulimsimamisha kwa madai amekuwa na tabia hiyo ya kuchelewa kila mara na kumtaka atoe maelezo.

Tuesday, December 22, 2015

UZINDUZI WA AUTUMN HARVEST ULIVYONOGA JIJINI MBEYA



 Wadau mbalimbali wa Autumn Harvest wakiendelea kufurahia kinywaji hicho huku wakijiselfie kwenye uzinduzi uliofanyika katika Hoteli ya Paradise jijini Mbeya.Kinywaji hicho hivi sasa kitakuwa kinaingizwa nchini kwa njia halali na kampuni ya Tanzania Distillers Limited(TDL) kikitokea Afrika Kusini kinakotengenezwa.
 Wasanii wa Kundi la Makhirikhiri la Mbeya wakitumbuiza kwenye hafla hiyo fupi ya uzinduzi.
 Mmoja wa wadau hau Francis Mwasamwene akichangia mwazo wakati wa hafla.
 Wasanii moja wa kundi la Makhirikiri la Mbeya wakiwa katika picha ya pamoja na Mhariri mkuu wa Lyamba Lya Mfipa Bw.Joachim Nyambo(wa pili kulia)

Meneja Autumn Harvest nchini Diana Balyagatiakizungumza jambo.