Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Thursday, December 3, 2015

CST YAADHIMISHA SIKU YA WALEMAVU DUNIANI KWA KUITAKA JAMII KUSHIRIKIANA NA WALEMAVU

JAMII nchini imehimizwa kuongeza ushirikiano dhidi makundi ya watu walio na mahitaji maalumu hususani walemavu kwakuwa kufanya hivyo kutawezesha uwepo wa jamii iliyo na ustawi na yenye kujali maslahi ya kila mmoja.

Afisa ustawi wa jamii mkoa wa Mbeya Bibi Stella Kategile amesisitiza hayo alipomwakilisha mkuu wa mkoa huo Abbas Kandoro kwenye sherehe za maadhimisho ya Siku ya walemavu duniani,yaliyofanyika kimkoa katika viwanja vya kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya yakiwa yameeandaliwa na Kituo cha Kulelea watoto wenye ulemavu cha Chird Surport Tanzania(CST).

Katika maadhimisho hayo yaliyokwenda sambamba na uzinduzi wa mpango wa Peleka rafiki zangu wote shuleni unaoendeshwa na CST,Bi.Kategile amesema bado jamii ya walemavu imekuwa ikitengwa katika masuala mbalimbali hatua inayosababisha jamii hiyo kujiona wanyonge na wasio na haki.

Kupitia hadhara hiyo,Bi Kategile amesema kuna kila sababu ya jamii ya walemavu kushirikiana na makundi mengine kwakuwa hakuna ajuae ulemavu utamfika lini.

Akizungumzia suala la elimu kwa walemavu,Bi Kategile amesema kuna kila sababu ya kuendeleza mpango wa elimu shirikishi kwenye shule zote ili kuwezesha watoto walio na ulemavu kubadilishana uzoefu wa kivipaji na wenzao kwakuwa kila upande unajambo la kipekee kwa kundi jingine

Kwa upande wake mkurugenzi mtendaji wa CST Bibi Noela Shawa amesema Mradi wa Peleka rafiki zangu wote shuleni hauwalengi watoto walio na ulemavu pekee bali pia wale waishio katika mazingira magumu ambao wanaikosa haki ya kupata elimu kutokana na mazingira wanayoishi.

Aidha Bi.Shawa amesema miundombinu isiyo rafiki kwa wanafunzi walio na ulemavu mashuleni,imekuwa ikisababisha watoto wengi kushindwa kujiunga kwenye shule zilizopo jirani na familia zao huku shule maalumu kwaajili ya watoto wa jamii hiyo zikionekana kuwa mbali hivyo kusababisha baadhi ya wazazi kukata tamaa ya kuwapeleka shuleni.

Desemba 3 ya kila mwaka,dunia huadhimisha siku ya Walemavu,lengo likiwa ni kuongeza mapambano dhidi ya vizingiti vinavyokwamisha ustawi wa jamii hiyo pasipo kujali aina ya ulemavu.

No comments:

Post a Comment