Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Tuesday, July 31, 2012

POLISI YAWASHIKILIA WATU 13 WAKIWEMO VIONGOZI WA CHAMA CHA WALIMU MKOANI MBEYA

Kamanda wa polisi wa Mkoa wa Mbeya Diwani Athumani , akiongea na waandishi wa habari
Waandishi wa habari wakimsikiliza kamanda wa polisi mkoa Mbeya

POLISI Mkoani Mbeya, inawashikilia watu 13  wakiwemo viongozi wa Chama cha walimu na walimu wenyewe kwa tuhuma za kuhusika na vurugu zilizosababisha hasara zaidi ya shilingi milioni 100 wakati wa mgomo wa walimu ulioanza juzi.
Kitendo cha walimu hao kugoma kuingia darasani kilisababisha baadhi ya maeneo, wanafunzi  kufanya maandamano ya amani ya kudai haki ya kufundishwa  jambo ambalo linadaiwa kutumiwa vibaya na wahalifu kwani walitumia nafasi hiyo kufanya uhalifu kwa kuiba mali za watu.
Wahalifu hao walichoma ofisi za Halmashauri ya Mbozi ndani ya Mji mdogo wa Tunduma  na kuiba mali zilizokuwemo kama  kompyuta 5 za ofisi, pikipiki yenye namba STK 6264, kumbukumbu na nyaraka mbalimbali.
Wahalifu hao  walivunja milango ya ofisi zote, kuvunja vioo vya magari ya kubebea taka aina FAW  SM 8726, na kuiba betri mbili za gari hilo  na gari dogo aina ya Nissan lenye namba SM 2858 mali ya mamlaka hiyo.

Kamanda wa polisi wa Mkoa wa Mbeya Diwani Athumani , aliwataja watuhumiwa hao wanaodaiwa kuhusika na uhalifu  na kusababisha hasara ya shilingi  milioni 117, 515,000  kuwa ni Mexon Mbilinyi, Akida Kondo, Chalres Rupia, Athumani Mgala, Stela Garbert, Atiliyo Benard, Nikodemus Exavely, Mashaka Amoni na James Kabuje.
Diwani, alisema kuwa watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaiwa kuhusika na uhalibifu wa ofisi ya halmashauri ya mji mdogo wa tunduma ikiwa na kuiba mali yenye thamani zaidi ya milioni 100 na kwamba wote kwa pamoja wamefikishwa mahakamani leo.
Akizungumzia suala la kukamatwa kwa viongozi wa Chama cha walimu pamoja na walimu  alisema watuhumiwa hao wamekamatwa kutokana na tuhuma za kuhamasisha wezao kugoma jambo ambalo ni kinyume cha sheria.
Aliwataja wahusika hao kuwa ni Mwalimu wa Patro Mangula na ni Katibu wa chama cha walimu wilaya ya Kyela ambapo inadaiwa kuwa kiongozi huyo alikuwa akishirikiana na watu wengine kupita mashuleni kuhamasisha walimu waliokuwa wanaendelea na kazi ya kufundisha wajiunge na mgomo.
Wengine ni Mwalimu Emanuel Kyejo wa shule ya msingi Mbebe Wilaya ya Ileje na mjumbe wa chama cha walimu wilaya ya Ileje, Anyakingwe Lwinga na mjumbe wa chama cha walimu ambapo wote kwa pamoja wanatuhumiwa kuhamasisha walimu kugoma.
Aidha, katika uhalifu wa Tunduma, Kamanada Diwani alisema kuwa polisi Mkoani Mbeya kwa kushirikiana na wananchi walifanikiwa kuokoa Mabati 168, Printa moja na mita mbili za maji, Bendera moja ya Taifa na photocopy mashine.
Pia, Kamanda Diwani alitumia nafasi hiyo kutoa ufafanuzi kwa nini askari wake walitumia  Bomu  na risasi katika vurugu hizo ambapo alisema kuwa Bomu hilo lilitumiwa kulitawanyisha kundi kubwa la watu lililokuwa linazidi kuelekea kwenye ofisi za serikali pamoja na Taasisi za kibenki  na kwamba hakuna madhara yaliyojitokeza.
“Baadhi ya watu wamekuwa wakiipotosha jamii kuwa askari walitumia bomu kuwatawanya wanafunzi na ndio sababu za wananchi kuanzisha vurugu jambo hilo si kweli kwani bomu lilitumiwa baada ya kundi la wahuni lililokuwa likivamia ofisi na kuiba mali zilizomo ndani,”alisema.
Alisema,  wakati kundi hilo linafanya vurugu tayari wanafunzi walikuwa wamerejea kwenye makao yao lakini kundi hilo la wahuni ndio lilikuwa likizidi kujikusanya na kuendelea kufanya uhalifu huo huku baadhi wakiwa wanaelekea kwenye eneo la Benki.
“Baada ya walinzi wa Benki kuona kundi hilo linaikaribia benki askari walipiga risasi mbili juu ili kuwatawanya na kwamba zoezi hilo lilisaidia kuwarudisha watu hao waliokuwa na lengo la kufanya uhalifu katika benki hiyo ,”alisema
Aidha,  Diwani aliitaka jamii kuondoa mawazo potofu kwamba huenda vurugu hizo zimechangiwa na baadhi ya wanasiasa jambo ambalo si kweli kwani jeshi la polisi linaamini kuwa kundi hilo la uhalifu halina itikadi yoyote ya siasa.
“Polisi inawashikilia watu hao kwa tuhuma za uhalifu na ninaamini watu hawa ni wahalifu hivyo watafikishwa mahakani kwa makosa ya uhalifu tu na wala hakuna siasa,”alisema
 
 Hata hivyo aliwataka walimu pamoja na viongozi wa chama cha walimu kuacha kuwahamasisha wezao kufanya mgomo kwani wao tayari walitangaza kugoma na wamegoma hivyo kupita mashuleni na kuwakuta wezao wanafundisha na kuwalazimisha kugoma ni uvunjifu wa amani hivyo hatua za kisheria zitachukuliwa zidi yao.
 
HABARI NA PICHA KWA HISANI YA MBEYAYETU BLOGU

Monday, July 30, 2012

JOGOO MWENYE SHANGA, HIRIZI AZUA KIZAZAA


Na Salum Maige, Sengerema

WAKAZI wa Mtaa wa Nyanchenche Road mjini Sengerema juzi walifurika kushuhudia tukio la kuonekana jogoo asiye na manyoya akitembea huku akiwa amefungwa shanga na hirizi mbili shingoni na mabawa yake yakiwa yamechanjwa chale na kupakwa dawa nyeusi.
 
Tukio hilo lililovuta umati wa watu lilitokea juzi  saa 7:00 mchana kwenye moja ya familia ya mtaa huo[jina limehifadhiwa]ambaye alidai kwamba kuku huyo alijitokeza nyumbani kwake bila kufahamu alikotokea.
 
Kuku huyo wa ajabu alikutwa na wananchi katika mji huo ulioko kando kando ya barabara,jambo lililowashtua wakazi wa Sengerema waliofika kulishuhudia huku wakilihusisha na imani za kishirikina.
 
Katika tukio hilo hakuna mwananchi aliyejitokeza kumshika kuku huyo, huku wenyeji wa mji husika wakiendelea na shughuli zao licha ya kuonyesha mshituko.
 
Akizungumza na waandishi wa habari,Mwenyekiti  wa kitongoji hicho Leah James alieleza kushangazwa na tukio hilo aliloliita la ajabu, na kwamba halijawahi kutokea  katika kitongoji hicho kwani limeibua hisia tofauti miongoni mwa wanajamii.
 
“Nimepata taarifa za tukio hili ilikuwa mchana muda wa saa saba na tumefika mpaka eneo la tukio, kwa kweli inashangaza na kusikitisha, huyo kuku wa ajabu hana nyoya hata moja wala alama ya kidonda na amechanjwa chale kwenye mbawa zake,kavishwa hirizi mbili shingoni na amefungwa shanga kwenye mbawa zake” alisema mwenyekiti.
 
Baada ya tukio hilo uongozi wa eneo hilo na sungusungu uliamua kuitisha mkutano siku iliyofuata leo(jana) ambapo walifuatilia na kumbaini mmiliki wa kuku huyo kuwa ni  Leticia Makoye ambaye alidai kuku huyo ni wake na  humtumia katika shughuli za uganga wa kienyeji .
 
Kikao hicho kiliamua kumrudishia kuku huyo ingawa alikuwa tayari amekufa kutokana na kupigwa baridi usiku kucha, maamuzi yaliyopingwa na wananchi na hivyo kulazimika kumshambulia kwa mawe hadi nyumbani kwake huku viongozi wa mtaa huo wakimpatia ulinzi hadi alipoingia ndani ya nyumba.
 
Baadhi ya wananchi waliozungumza na Gazeti hili eneo la tukio wamekuwa na hisia tofauti huku baadhi yao wakilihusisha na imani za kishirikina kutokana na vitu alivyokutwa navyo kuku huyo ikiwa ni pamoja na shanga,hirizi,na chale alizochanjwa kwenye mbawa zake.
 
Grece Michael (32), Fadhili Alfani (45), na Daniel Marco walisema  matukio ya ajabu kama hilo ni dalili za mwisho wa dunia kutokana na vitendo vya kishirikina kuongezeka na kwamba njia pekee ya kuepukana navyo ni kudumu katika sala na imani.

Chanzo: Mtanzania

Taarifa ya serikali ya kuifungia MWANAHALISI


NI VURUGU,MGOMO,MAANDAMANO TUNDUMA

KUFUATIA Mgomo wa walimu ulioanza leo, wanafunzi wa shule mbalimbali za msingi waliamua kuandamana ili kudai haki ya kufundishwa katika maandamano ambayo yaliingiliwa na vibaka ambao baadaye walivunja ofisi za Halmashauri ya mji wa Tunduma na kuiba mali kadhaa kisha kuchoma nyaraka zilizokuwemo.

Hatua hiyo ilijitokeza mapema saa 2asubuhi wakati wanafunzi wa shule 14 za msingi zilizopo katika halmashauri wa Tunduma,walipojikusanya na kufanya maandamano hadi nyumbani kwa diwani ambapo baada ya kumkosa walielekea kituo cha polisi cha mjini hapa kabla ya kufika ofisi za halmadhauri ya mji.

kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo walidai kuwa, awali wanafunzi hao walikwenda nyumbani kwa diwani wa kata ya Tunduma Frank Mwakajoka (CHADEMA) na baada ya kufanya mazungumzo na mke wa diwani huyo ambaye inadaiwa hakuwepo waliandamana hadi kituo cha polisi na kuelekea katika ofisi za halmashauri ya mji ambapo msafara huo uliingiliwa na baadhi ya watu walioendesha uporaji huo.


Mmoja wa Shuhuda hao ambaye alijitambulisha kuwa ni Julius Edward, alidai kuwa baada ya wanafunzi hao kufika katika ofisi  za polisi walipokelewa na kufanya mazungumzo ambayo  maamuzi yake hayakuafikiwa na wanafunzi hao.


Alisema baada ya kutoafiki majibu yaliyotolewa na Polisi
  wanafunzi hao waelekea kwenye mzunguko wa barabara uliopo karibu na eneo la ofisi za Uhamiaji na Mamlaka ya Mapato nchini (TRA) katika mpaka wa Tanzania na Zambia ambako walizuia barabara ili magari yasipite.

Usumbufu huo ulidaiwa kujitokeza kwa muda wa nusu saa, hatua ambayo ilisababisha   polisi wa kituo hicho kufika eneo hilo na kulazimika
 kuwatawanya wanafunzi hao kwa kutumia mabomu mawili ya machozi hali ambayo ilisababisha vibaka kujiingiza na kuaanza uporaji kwa kukimbilia ziliko ofisi za halmashauri ya mji.

Watu hao ambao wameonekana wakivamia ofisi hizo na kuchoma moto baadhi ya mali za halmashauri hiyo huku wakipora  kompyuta 5 za ofisi, pikipiki yenye namba STK 6264, kumbukumbu na nyaraka mbalimbali sambamba na kuvunja milango ya ofisi zote, kuvunja vioo vya magari ya kubebea taka aina FAW  SM 8726, na kuiba betri mbili za gari hilo  na gari dogo aina ya Nissan lenye namba SM 2858 mali ya mamlaka hiyo.


Kulingana na tukio hilo vibaka wameweza kuonekana wakipora mali katika ofisi hizo huku wengine wakivunja chumba cha kuhifadhia mizigo mbalimbali na kufanikiwa kuiba mabati na viti na mali nyingi zilizokuwa zikibebwa,huku baadhi yao walionekana wamebeba madumu ya mafuta ya petroli wakitishia kuchoma jengo hilo.


Aidha Wanacnhi wa mjini hapa wanakumbuka matukio mbalimbali yanayojitokeza katika mji huu kuwa huwa yana leta adhari, kama ilivyo tokea katika matukio machache ya Februari 18, 2005 kufuatia wamachinga watano waliokamatwa Nakonde Zambia na mnao Septemba mosi hadi 3 mtu mmoja aliyefia  katika mahabusu ya Nakonde nchini Zambia.


Mji wa Tunduma umekuwa kinala cha  matukio ya vurugu  na uvunjifu wa amani linapotokea jambo lolote hali ambayo huchangiwa na
  watu wanaojiita wana harakati kuongoza vikundi vya watu ambao huaribu na kupora mali za watu.

Mkurugenzi wa mji huu Aidan Mwanshiga alipotakiwa kuelezea uharibifu hu alisema kuwa
  tadhimini ya uharibifu uliotokea inafanywa na taarifa rasmi itatolewa.

Kamanda wa polisi wa mkoa wa Mbeya Diwani Athumani akizungumzia tukio hilo alisema kuwa tukio hilo haliwezi kuvumiliwa kutokana na kuwa maandamano ya wanafunzi hayawezi kupelekea kuvunjwa kwa ofisi za serikali bali kuna watu ambao wametumia mwanya huo ili kupora mali.

Aidha Kamanda Diwani alisema mbali ya uharibifu wa mali za Mamlika ya mji wa Tunduma hakuna madhala mengine yaliyotokea ikiwa ni pamoja na majeruhi au vifo vilivyojitokeza.


Wakati huo huo katika Kata ya Vwawa wanafunzi wa shule za Ichenjezya na Haloli waliandamana hadi ofisi za halmashauri ya wilaya ya Mbozi na baada ya maandamano hayo walirejea shuleni kwao kwa amani huku wakisindikizwa na Polisi.

aidha wanafunzi hao walidai kuwa walimu wao walifika shuleni lakini hawakuwa tayari kufundisha wakiwaambia kuwa hawatafundisha kwa vile wapo kwenye mgomo hivyo waliwashauri waandamane hadi ofisi za halmashauri kudai haki yao hiyo.


Vilevile habari kutoaka Jijini Mbeya zimeeleza Mbeya zimeeleza kuwa mgomo ulianza mapema leo asubuhi, ambapo walimu walifika shuleni na kusaini kitabu cha mahudhurio kisha kukaa kimya huku wakiawaacha wanafunzi wakilandalanda bila cha kufanya.

Saturday, July 28, 2012

ALBINO WAHIMIZWA KUSHIRIKI SENSA


WALEMAVU wa ngozi (Albino) wamesisitizwa kushiriki zoezi la sensa ya watu na makazi inayotarajiwa kufanyika agosti 26 mwaka huu na kudumu kwa muda wa siku saba.
Mmoja wa washiriki wa mafunzo ya wakufunzi watakaokwenda kufundisha makarani wa Sensa katika ngazi za tarafa za wilaya mkoani Mbeya Mwalimu Sydney Mwamlima ambaye pia ni mlemavu wa ngozi ameyasema hayo alipozungumza na waandishi wa habari muda mfupi baada ya mafunzo yao ya siku 12 kufungwa.

Mwalimu Mwamlima amesema kama ilivyo kwa shughuli nyingine takwimu zitakazopatikana kupitia sense ya watu na makazi zitasaidia serikali na wadau wengine katika kupanga mikakati ya kupambana na changamoto zinazowakabili walemavu hao.

Amesema kumekuwepo na changamoto nyingi zinazowakabili albino ikiwemo mauaji ya kinyama na kukatwa viungo kunakofanywa na baadhi ya watu kutokana na imani za kishirikina hivyo jamii hiyo inaishi kwa hofu kubwa.

Hata hivyo amesema ulinzi kwa jamii hiyo ni mdogo hali aliyosema huenda pia inasababishwa na kutowepo kwa takwimu zinazoonesha idadi yao ambazo zingeweza kusaidia katika kuweka mpango madhubuti ya kuwapa huduma muhimu ikiwemo ulinzi dhidi ya maadui.

Amewataka albino wenzakekutojificha wakati wa kuhesabiwa badala yake watoe ushirikiano wa kutosha kwa makarani watakaohusika na sense ya watu na makazi kwenye maeneo wanayoishi.

“Ni vema tukajitokeza kuhesabiwa kwakuwa sisi kama jamii yenye mahitaji maalumu pia takwimu zetu zinahitajika ili zisaidie wadau mbalimbali kupanga mikakati itakayosaidia kutatua changamoto zinazotukabili.Lakini pia sisi hatutengani na jamii nyingine hivyo ni vema hesabu yetu pia ikaungana na watu wengine ili kuiwezesha serikali kutambua idadi ya watu iliyo nao.” Alisisitiza mwalimu Mwamlima.

Naye afisa tawala wa wilaya ya Mbarali Moses Mashala ambaye pia ni muhitimu wa mafunzo hayo amesema hamasa zaidi inahitajika kwa wananchi hasa maeneo ya pembezoni ili watambue umuhimu wa kuhesabiwa.

Aliitaja wilaya ya Mbarali kuwa miongoni mwa maeneo yanayohitaji uhamasishaji wa hali ya juu kutokana na jamii inayoishi katika wilaya hiyo ambao wengi ni wafugaji wa makabila ya wasangu,wamasai na wasukuma ambao ni mara chache kuhudhuria vikao na mikutano ya kuhamasisha masuala ya msingi.

Kwa upande wake mshiriki mwingine Mary Swila mkazi wilayani Momba amependekeza vyombo vya habari kuwezeshwa zaidi ili visaidie katika kutoa elimu hususani katika maeneo ya pembezoni kama wilayani kwake ambako watu wengi wanategemea vyombo hivyo.

WATENDAJI MSHINDE KWENYE MIRADI


WATENDAJI katika halmashauri ya wilaya ya Mbeya wamekumbushwa kuwa ofisi zao ni kule miradi iliko na si katika majengo ya halmashauri yao.

Mkuu wa wilaya hiyo Norman Sigalla ameyasema hayo wakati akitoa salamu za serikali kwenye kikao cha kawaida cha baraza la madiwani ambacho miongoni mwa ajenda zake ilikuwa kumchagua naibu meya na kupitisha kamati mbalimbali.

“Haya majengo yapo kwaajili ya kuangalia ni wapi miradi inatekelezwa.Msikae huku mpaka wakulima waunguze mazao yao kwa matumizi mabaya ya mbolea.Nendeni huko mtoe mafunzo kwa vitendo wakulima wabadilike na waanze kunufaika na mikakati ya matumizi ya pembejeo bora”.

Sigalla amesisitiza ushirikiano baina ya watendaji na madiwani  akisema chuki inapaswa kuwa mwiko iwapo pande hizo zina nia ya dhati ya kuwatumikia wananchi wa halmashauri ya wilaya hiyo.

Amesisitiza watendaji kuzingatia maoni ya madiwani badala ya kuyapuuza kwakuwa wapo kuwawakilisha wananchi wa kata wanazoziongoza na miradi wanayoomba ndiyo inayohitajika kwa wananchi wao.

Hata hivyo alisema wapo baadhi ya madiwani walio na tabia ya kusema ya kwao na si wananchi na kusema diwani mzuri ni ni anayehakikisha mikutano inafanyika katika vijiji vyote vya kata yake kabla ya kuleta hoja za wananchi wake kwenye kikao cha baraza la madiwani.

Ameonya madiwani na wanasiasa kutohamasisha vitendo vinavyozusha migogoro akisema Mbeya ni muhimu kuliko vyama vya siasa hivyo ni vema wakajikita katika kuilinda amani ya wilaya yao badala ya kutekeleza matakwa ya siasa zilizo na mwelekeo wa kuhatarisha amani.

Mkuu huyo wa wilaya hakusita kuonya kuwa kwa yeyote atakayebainika kuhusika na uchochezi wa migogoro atakuwa wa kwanza kuchukuliwa hatua za kisheria pasipo kuangalia ni diwani ama ana wadhifa upi katika chama chake cha siasa.

Amesisitiza kutumia njia ya majadiliano zaidi pale inapobainika kuna tofauti badala ya kuanzisha makundi ya malumbano yasiyo na sababu za msingi.

Wednesday, July 25, 2012

TCRA YATOA UFAFANUZI WA SATELITE


MWINGILIANO wa masafa ya televisheni uliotokea hivi karibuni katika baadhi ya maeneo ya Jiji la Mbeya umeelezwa kusababishwa na masafa yaliyokuwa yakitumika kuchukuliwa na wamiliki wake halali walioyanunua.

Hayo yamebainishwa leo na Meneja wa mamlaka ya mawazsiliano nchini(TCRA) Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Deogratius Moyo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake.
 
Moyo amesema kuwa masafa hayo  hivi sasa yanatumika kutolea huduma za Interneti kwa makampuni yanayotoa huduma hiyo nchini.
Amesema kwa watumiaji  wa dishi ya Setilaiti wanatakiwa kufanya marekebisho ya madishi yao ili waweze kupata masafa sahihi yanayorusha matangazo kwenye masafa yaliyotengwa kwa ajili ya matangazo ya Televisheni.

Akifafanua zaidi, Meneja huyo amesema masafa ya sataelaiti katika C-Band huanzia 3.7GHZ hadi 4.2GHZ yametengwa kwa ajili ya intaneti barani Afrika huku masafa hayo katika C- Band huanzia 3.4GHZ hadi 3.6GHZ ni kwa ajili ya ukanda wa Afrika Mashariki.
 
Akizungumzia tatizo la masafa katika jiji la Mbeya, Moyo amesema kuwa kwa kuwa wananchi wengi walifunga kifaa cha kunasa mawimbi (NLB) kwenye uelekeo wa masafa ya intaneti ambayo wamiliki wake walikuwa hawajaanza kuyatumia, na kuwa baada ya wamiliki halali kuyachukua imesabaisha baadhi ya watu kukosa matangazo ya televisheni.

Meneja huyo amesema masafa hayo kwa hivi sasa yanatumiwa na kampuni ya simu ya Vodacom, hivyo watumiaji wengine hawana budi kuhama na kubadilisha kifaa cha kunasa matangazo kwa njia ya sataelaiti (LNB).

Amesisitiza wananchi kujiunga na mfumo wa digitali kwa kuwa ifikapo Desemba 31, mwaka huu mitambo ya kurushia matangazo kwa njia ya analojia itazimwa nchini huku akiusifia mfumo mpaya akisema ni salama, hauna madhara wala  gharama kubwa kwa mtumiaji.

POWERTILLER 40 HAZITUMIKI CHUNYA


MATREKTA madogo(Powertiller) 40 yaliyonunuliwa na halmasahauri ya wilaya ya Chunya na kusambazwa vijijini hayafanyi kazi.

Kwa mujibu wa mkuu wa wilaya hiyo Deodatus Kinawiro matrekta hayo yaliyoigarimu serikali zaidi ya shilingi milioni 217 hayajafanya kazi yoyote tangu yapelekwe vijijini ikiwa ni zaidi ya mwaka sasa umepita huku sababu za kutotumika zikiwa hazifahamiki.
 
Kinawiro aliyasema hayo katika kikao maalumu cha baraza la madiwani kilicholenga kujadili taarifa ya mdhibiti na mkaguzi wa hesabu za serikali(CAG) kilichokuwakikiongozwa na mkuu wa mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro.

Aliyasema hayo kufuatia mkuu wa mkoa kuhoji iwapo matrekta yanayotajwa katika moja ya hoja za CAG kwenye taarifa yake ya mwaka wa fedha 2010/2011 kuwa mpaka ukaguzi unafanyika matrekta hayakuonekana licha ya fedha kutumika na ndipo madiwani wakajibu kuwa yalinunuliwa na kusambazwa vijijini.

Hata hivyo mkuu wa wilaya aliwashangaa madiwani haoa kisema hawasemi ukweli juu ya matumizi ya matrekta hayo kwani hayafanyi shughuli iliyolengwa na serikali ya kuwapunguzia wakulima adha ya kulima kwa mkono.

Kinawiro alitolea mfano katika kata ya Ifumbo kuliko na mradi mkubwa waumwagiliaji akisema zilipelekwa Powertiller nne na tatu kati ya hizo zimeendelea kukaa bila matumizi na moja inatumiwa kwa shughuli za kubeba mchanga na mawe na si kulimia.

Alisema kama serikali ya wilaya tayari wamemuandikia barua mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ili aeleze ni kwa nini powertiller hizo hazijaanza kuwasaidia wakulima kama maelekezo ya serikali yanavyoeleza.

Alisema pia serikali kuu imepeleka fedha kwaajili yakununua powertiller nyingine kumi lakini amezuia ununuzi huokwakuwa 40 za kwanza hazijaonekana kufanya chochote.

“Tunalazimika kuhoji zile za awali hazifanyi kazi mpaka sasa kuna haja gani ya kununua nyingine 10.Tumeiuliza halmashauri na sasa tunasubiri majibu kutoka kwa mkurugenzi” alisema.