Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Saturday, July 28, 2012

ALBINO WAHIMIZWA KUSHIRIKI SENSA


WALEMAVU wa ngozi (Albino) wamesisitizwa kushiriki zoezi la sensa ya watu na makazi inayotarajiwa kufanyika agosti 26 mwaka huu na kudumu kwa muda wa siku saba.
Mmoja wa washiriki wa mafunzo ya wakufunzi watakaokwenda kufundisha makarani wa Sensa katika ngazi za tarafa za wilaya mkoani Mbeya Mwalimu Sydney Mwamlima ambaye pia ni mlemavu wa ngozi ameyasema hayo alipozungumza na waandishi wa habari muda mfupi baada ya mafunzo yao ya siku 12 kufungwa.

Mwalimu Mwamlima amesema kama ilivyo kwa shughuli nyingine takwimu zitakazopatikana kupitia sense ya watu na makazi zitasaidia serikali na wadau wengine katika kupanga mikakati ya kupambana na changamoto zinazowakabili walemavu hao.

Amesema kumekuwepo na changamoto nyingi zinazowakabili albino ikiwemo mauaji ya kinyama na kukatwa viungo kunakofanywa na baadhi ya watu kutokana na imani za kishirikina hivyo jamii hiyo inaishi kwa hofu kubwa.

Hata hivyo amesema ulinzi kwa jamii hiyo ni mdogo hali aliyosema huenda pia inasababishwa na kutowepo kwa takwimu zinazoonesha idadi yao ambazo zingeweza kusaidia katika kuweka mpango madhubuti ya kuwapa huduma muhimu ikiwemo ulinzi dhidi ya maadui.

Amewataka albino wenzakekutojificha wakati wa kuhesabiwa badala yake watoe ushirikiano wa kutosha kwa makarani watakaohusika na sense ya watu na makazi kwenye maeneo wanayoishi.

“Ni vema tukajitokeza kuhesabiwa kwakuwa sisi kama jamii yenye mahitaji maalumu pia takwimu zetu zinahitajika ili zisaidie wadau mbalimbali kupanga mikakati itakayosaidia kutatua changamoto zinazotukabili.Lakini pia sisi hatutengani na jamii nyingine hivyo ni vema hesabu yetu pia ikaungana na watu wengine ili kuiwezesha serikali kutambua idadi ya watu iliyo nao.” Alisisitiza mwalimu Mwamlima.

Naye afisa tawala wa wilaya ya Mbarali Moses Mashala ambaye pia ni muhitimu wa mafunzo hayo amesema hamasa zaidi inahitajika kwa wananchi hasa maeneo ya pembezoni ili watambue umuhimu wa kuhesabiwa.

Aliitaja wilaya ya Mbarali kuwa miongoni mwa maeneo yanayohitaji uhamasishaji wa hali ya juu kutokana na jamii inayoishi katika wilaya hiyo ambao wengi ni wafugaji wa makabila ya wasangu,wamasai na wasukuma ambao ni mara chache kuhudhuria vikao na mikutano ya kuhamasisha masuala ya msingi.

Kwa upande wake mshiriki mwingine Mary Swila mkazi wilayani Momba amependekeza vyombo vya habari kuwezeshwa zaidi ili visaidie katika kutoa elimu hususani katika maeneo ya pembezoni kama wilayani kwake ambako watu wengi wanategemea vyombo hivyo.

No comments:

Post a Comment