Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Saturday, July 28, 2012

WATENDAJI MSHINDE KWENYE MIRADI


WATENDAJI katika halmashauri ya wilaya ya Mbeya wamekumbushwa kuwa ofisi zao ni kule miradi iliko na si katika majengo ya halmashauri yao.

Mkuu wa wilaya hiyo Norman Sigalla ameyasema hayo wakati akitoa salamu za serikali kwenye kikao cha kawaida cha baraza la madiwani ambacho miongoni mwa ajenda zake ilikuwa kumchagua naibu meya na kupitisha kamati mbalimbali.

“Haya majengo yapo kwaajili ya kuangalia ni wapi miradi inatekelezwa.Msikae huku mpaka wakulima waunguze mazao yao kwa matumizi mabaya ya mbolea.Nendeni huko mtoe mafunzo kwa vitendo wakulima wabadilike na waanze kunufaika na mikakati ya matumizi ya pembejeo bora”.

Sigalla amesisitiza ushirikiano baina ya watendaji na madiwani  akisema chuki inapaswa kuwa mwiko iwapo pande hizo zina nia ya dhati ya kuwatumikia wananchi wa halmashauri ya wilaya hiyo.

Amesisitiza watendaji kuzingatia maoni ya madiwani badala ya kuyapuuza kwakuwa wapo kuwawakilisha wananchi wa kata wanazoziongoza na miradi wanayoomba ndiyo inayohitajika kwa wananchi wao.

Hata hivyo alisema wapo baadhi ya madiwani walio na tabia ya kusema ya kwao na si wananchi na kusema diwani mzuri ni ni anayehakikisha mikutano inafanyika katika vijiji vyote vya kata yake kabla ya kuleta hoja za wananchi wake kwenye kikao cha baraza la madiwani.

Ameonya madiwani na wanasiasa kutohamasisha vitendo vinavyozusha migogoro akisema Mbeya ni muhimu kuliko vyama vya siasa hivyo ni vema wakajikita katika kuilinda amani ya wilaya yao badala ya kutekeleza matakwa ya siasa zilizo na mwelekeo wa kuhatarisha amani.

Mkuu huyo wa wilaya hakusita kuonya kuwa kwa yeyote atakayebainika kuhusika na uchochezi wa migogoro atakuwa wa kwanza kuchukuliwa hatua za kisheria pasipo kuangalia ni diwani ama ana wadhifa upi katika chama chake cha siasa.

Amesisitiza kutumia njia ya majadiliano zaidi pale inapobainika kuna tofauti badala ya kuanzisha makundi ya malumbano yasiyo na sababu za msingi.

No comments:

Post a Comment