MKUU wa wilaya ya Rungwe Chrispin Meela amewaonya watu watakaotaka
kuvuruga mwenendo wa ukusanyaji wa maoni ya katiba mpya mara Tume
husika itakapofika akisema watachukuliwa hatua za kisheria.
Meela alitoa onyo hilo alipotoa salamu za serikali kwenye kikao cha
baraza la madiwani wa halmashauri ya wilaya hiyo kilichofanyika Julai
11 mwaka huu.
Alisema wapo watu wanaotajwa kuvuruga mwenendo wa ukusanyaji wa maoni
mahali ambako tume husika imepita na kusema hali hiyo haitavumiliwa
itakapoonekana wilayani Rungwe.
Aliwataja wanasiasa kuwa miongoni mwa waliobainika kuleta kasoro hizo
hususani kwa kuhudhuria zaidi ya mkutano mmoja na kutaka kuchangia
maoni kwenye mikutano hiyo.
Alisema kila mwananchi atakuwa huru kuchangia maoni yake katika kituo
kitakachopangwa karibu na makazi yake na si kuhudhuria na kutaka
kuchangia katika zaidi ya mkutano mmoja.
Alisema maoni yatakayotolewa pia yatakuwa ya mtu anayeyatoa na si
kushinikizwa na mtu mwingine kuwa aseme nini.
Mkuu huyo wa wilaya aliitumia fursa hiyo kuonya baadhi ya
wafanyabiashara wanaowabambikiza wakulima wachangie sehemu ya ushuru
wanaopaswa kulipa wao.
Alisema baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wakiwakata wakulima fedha
wanapolipa kutokana na mazao waliyonunua wakisema kiasi kinachokatwa
ni kwaajili ya ushuru wa mazao jambo alilosema ni kuwaibia wakulima.
Alisema anayepaswa kulipa ushuru ni mfanyabiashara na si mkulima hivyo
ni vema wakulima wakawafichua wafanyabiashara watakaobainika ili
wachukuliwe sheria.
Alisema pia serikali wilayani hapo inaandaa mchakato utakaowezesha
wafanyabiashara wanaoingia kununua mazao wanatambuliwa ili iwe rahisi
kujua njia wanazotumia kulipa kodi
No comments:
Post a Comment