Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Saturday, July 21, 2012

VURUGU LUPATINGATINGA TENA


VURUGU zilizoibuka Julai 18 mwaka huu na kudumu kwa siku mbili katika kijiji cha Lupa wilayani Chunya mkoani Mbeya zimesababisha uharibifu wa mali zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 30.
Uharibifu huo ulitokana na kuchomwa kwa gari yenye namba T 882 ANM Toyota Landcruiser yenye thamani ya shilingi milioni 20 na nyumba yenye thamani ya shilingi milioni 10 iliyoteketea pamoja na vitu vyote vilivyokuwa ndani vyote vikiwa ni mali ya Masagija Jilala(40) mkazi kijijini hapo.

Kwa mujibu wa kamanda wa polisi mkoani hapa Diwani Athumani wakazi wa kijiji hicho ndiyo walichoma mali hizo ikiwa ni njia ya kulipiza kisasi kutokana na baba wa Masagija aliyefahamika kwa jina la Jilala Kamonga(88) ambaye ni kiongozi wa askari wa jadi(Sungusungu) kuamuru askari hao kuwakamata watu wataatu waliotuhumiwa kuiba ng’ombe watatu.

Kamanda Athumani alisema mnamo julai 18 majira ya saa 3:30 asubuhi katika kijiji hicho watu watatu walituhumiwa kuiba ngo’mbe watatu mali ya Edward Helbert(32),Masagija Kamaga(40) na mwingine aliyefahamika kwa jina moja la Mohamed.

Aliwataja watuhumiwa wa wizi huo kuwa ni Kadoda Kayombo(40) na Msafiri Mgaya(38) wote wakazi wa kijiji cha Lupa na Makula Mfanyange(28) mkazi wa kijiji cha Ng’ung’ungu.

Alisema baada ya kutuhumiwa kundi la askari wa sungusungu waliwakamata watuhumiwa na kuwapeleka msituni walikoanza kuwatesa kwa kuwapiga.

Kamanda Athumani alisema baada ya wananchi kuona watuhumiwa waliokamatwa hawarejeshwi kijijini na hakuna taarifa za kuwapeleka polisi walijichukulia sheria Julai 19 saa 1:30 usiku kwa kuvamia nyumba ya mtoto wa Mtemi wa sungusungu na kuchoma nyumba na gari yake.

Hata hivyo alisema watuhumiwa wa wizi waliokuwa wamekamatwa walipatikana baadaye msituni wakiwa wametelekezwa na kufikishwa hospitali ya wilaya ambako walipata matibabu na kuruhusiwa.

Kufuatia hali hiyo kamanda huyo alisema jeshi la polisi linaendelea na uchunguzi wa tukio hilo ikiwa ni pamoja na kuwasaka sungusungu waliohusika pamoja na wananchi waliochoma moto gari na nyumba.

No comments:

Post a Comment