Tuesday, September 20, 2016
Ofisi ya Madini Chunya na mchango wake katika sekta ya Madini.
Na Joachim Nyambo.
OFISI ya Madini Chunya kwa sasa
inahudumia eneo lote la wilaya za Chunya mkoa wa Mbeya na Songwe mkoani
Songwe.Huduma ni pamoja na Utafiti,uchimbaji na biashara ya madini.
Kwa mujibu wa Kaimu Afisa Madini
Mkazi wa wilaya ya Chunya Ndege Bilagi,Ofisi ina jumla ya watumishi 12
wanaogawanyika katika kada za mhandisi wa migodi mmoja,mjiolojia mmoja,Fundi
sanifu mmoja,mhasibu mmoja,madereva watatu,walinzi watatu,mwangalizi wa ofisi
mmoja na katibu mhitasi mmoja.Watumishi wane kati ya hao ni wa mkataba.
Ofisi hii inafanya kazi za Idara ya
Madini iliyo chini ya wizara ya nishati na Madini,inatoa taarifa yake ofisi ya
madini Kanda iliyopo jijini Mbeya.Pia inatoa taarifa katika taasisi nyingine za
serikali ikiwa ni pamoja na ofisi ya mkuu wa wilaya juu ya utekelezaji wa
shughuli mbalimbali za ofisi.
Ofisi inashirikiana na Halmashauri
katika kutekeleza majukumu yake kwani shughuli nyingi za uchimbaji
zinaingiliana na matumizi mengine ya rasilimali kama maji,misitu na ardhi.
“Baadhi ya shughuli zinazosimamiwa
na ofisi ni pamoja na Kusimamia na kuratibu mfumo wa leseni wa Online Mining
Cadastre Transaction Portal(OMCTP) kwa watumiaji wa leseni ikiwemo
kuwasajiri,kuwafundisha wachimbaji au wateja namna ya kuomba na kuingiza maombi
ya leseni kwa kutumia akaunti zao za barua pepe”anasema Bilagi.
Shughuli nyingine ni Kusimamia
uchimbaji wa awali(mdogo) wa madini ikiwa ni pamoja na kutoa huduma za
ugani(Extension Service) kwa wachimbaji wadogo.Kukagua usalama wa maeneo ya
wachimbaji wadogo na wakubwa na Kutoa elimua ya uhifadhi wa mazingira kwa
wachimbaji wadogo,wa kati na wakubwa.
Nyingine ni kutoa elimu kuhusiana na
matumizi ya baruti na kusimamia au kuhakikisha kuwa sheria na matumizi ya
baruti vinatekelezwa kwa ufasaha.Kukusanya Maduhuli ya aina mbalimbali ya
serikali yatokanayo na shughuli mbalimbali za madini.
“Ofisi pia ainawajibika kukagua
shughuli za utafiti wa madini zinazofanywa na wenye leseni kubwa za utafiti wa
madini(prospecting licenses),kupokea taarifa za robo mwaka kutoka kwa watafiti
madini wenye leseni kubwa na kuzioanisha ili kubaini kama taarifa hizo
zinaendana na kazi iliyofanyika katika leseni husika”
“Kuna kusimamia shughuli za
uchimbaji mkubwa ili kubaini kama Sheria na kanuni zinafuatwa.Kufanya ukaguzi
wa shughuli zote za uchimbaji kwa lengo la kubaini ukiukwaji wa sheria,Kutoa
vibali vya kusafirisha madini na sampuli zenye madini nje na ndani ya nchi na
pia Kutoa vibali vya kuagiza Baruti,kukagua maghala ya kutunzia baruti”
“Kwa kifupi tunasimamia Sheria ya
Madini ya mwaka 2010,sheria ya Baruti ya mwaka 1963 pamoja na Sheria ya
Mazingira ya mwaka 2004” anasema Bilagi.
Uchimbaji mdogo wa madini
Bilagi anasema,Uchimbaji mdogo wa
madini unafanywa na watanzania pekee ambao lazima wawe na leseni za awali za
uchimbaji zijulikanazo kama Primary Mining Licenses(PMLs).Katika wilaya ya
Chunya uchimbaji huu unafanyika katika maeneo yaliyogawanywa kwenye kanda.
Kanda ya Makongolosi kuna maeneo ya
Mkola,Mapele,Gepu,Ujerumani,Chipoka na Kilombero wakati Kanda ya Matundani vipo
vituo vya Kasisi,Kasakalawe,Itumbi Jeshini,Jobu Iti,Makatang’ombe,Idundu na
Bwawani.
Kanda ya Chunya kuna maeneo ya
Sinjili,Mlima Yasini,Mapogolo,Kiwanja,Mbugani,Itumba,Godima,Simba
Reef,Simbachai,Safari
Mine,Saitunduma,Simbadume,Majengo,Isenyela,Chalangwa,Nyatula,Mlimanjiwa,Kasanga
Madini,Kasanga Market,Soweto na Mamusapu.
Maeneo mengine kwenye ukanda huu ni
Mapapai,Ifumbo,Chikula,Kisu Mine,Magamba,Makoma,Mawelo,Mnyolima,Mwankonyonto,Shoga,Legezamwendo,Ilepuka,Chokaa,Mapunga,Majengo,Ihamba,Tukuyu,Sangambi,Izumbi
na Kikavu.
Anasema wilaya za Chunya na Songwe
zina wachimbaji wadogo wenye leseni za PMLs zipatazo 729.
Utafutaji wa Madini
Anasema Shughuli za Utafutaji wa
madini zinafanyika kwenye leseni zinazojulikana kama Prospecting Licences(PL)
katika maeneo yote ya wilaya ya Chunya
ili kubaini uwezekano wa kupata mashapo makubwa ya madini.
Ukanda huu wa madini unajulikana kwa
jina la kijiolojia kama Lupa Gold Fields ambao una madini ya dhahabu na madini
mengine ya Metali yaani Shaba,fedha,galena,chuma na mengineyo.Nje ya ukanda wa
Lupa Goldfields kuna madini mengine kama rare earth
elements(Metals),Magadi(Soda ash),madini ya vito na mengineyo.Wilaya hizi mbili
zina jumla ya leseni za utafutaji madini 179.
“Kuna kituo cha Kufundishia
wachimbaji wadogo cha Matundasi ASM kilichoanzishwa na serikali mwakaa 2005 ili
kutoa elimu kwa vitendo kwa wachimbaji wadogo.Kituo hiki kipo eneo la Matundasi
ambapo mwaka 2008 kilibinafsishwa kwa mwekezaji kwa makubaliano na serikali ili
akiendeleze. Kwa sasa mradi huo unaendelea na shughuli za uchorongaji miamba
ili kubaini mashapo yatakayoweza kuanzisha mgodi darasa”anasema.
Uchimbaji Mkubwa
Uchimbaji mkubwa unafanyika katika
maeneo mbalimbali na kuna leseni zipatazo tano katika eneo linalisimamiwa na
Ofisi hii ya Madini ya Chunya.Kwa eneo la wilaya ya Chunya pekee kuna uchimbaji
mkubwa unafanyika eneo la kata ya Matundasi ambapo kampuni ya Sunshine Mining
Co Limited yenye leseni ya ucjenjuaji(processing licence) namba 00067/2013 na
imeomba Mining Licence kwa maeneo yake mawili.
“Kwa sasa kampuni hii imesimamisha shughuli zake ili kutengeneza
miundombinu ya bwawa la maji machafu(Tailing Storage Facility-TSF).Vilevile
tuna wachimbaji wengi wadogo ambao sasa mitaji yao na uchimbaji wao umekuwa
kutoka kwa wachimbaji wadogo hadi kufika kuwa wachimbaji wa kati.Mfano ni
Aidani Msigwa,Isack Msowoya na Elias Mwembe.”
Uzalishaji Madini na Ulipaji wa Maduhuli ya Serikali
Kwa mujibu wa sheria ya
madini,Wachimbaji wakubwa na wadogo wanapaswa kulipa kodi za serikali ambazo ni
Ada ya mwaka ya leseni,mrabaha wa asilimia nne kutokana na uzalishaji waa
madini,ada za kubeba baruti,ujenzi wa maghala ya kuhifadhia baruti.Hivyo serikali
kupata mapato kutokana na tozo hizo ambapo utaratibu ni kuwa fedha zinapaswa
kulipwa benki moja kwa moja.
Katika kipindi cha mwaka wa fedha
2010/2011 hadi 2015/2016 Jumla ya Shilingi 1,888,642,319.66 zilikusanywa na
Ofisi ya Madini wilayani Chunya ikiwa ni Mrabaha wa
asilimia 4 wa madini aina ya dhahabu yaliyochimbwa na wachimbaji wadogo wilayani
hapa katika kipindi hicho.
Bilagi anasema katika kipindi hicho
Jumla ya Gramu 821,113.16 za dhahabu zenye thamani ya jumla ya Shilingi
47,216,058,041.50 zilizalishwa katika migodi mbalimbali wilayani hapa hivyo
kuwezesha serikali kujipatia shilingi 1,888,642,319.66 ikiwa ni mrabaha wa asilimia 4.
Akifafanua zaidi,anasema katika
mwaka wa fedha 2010/2011 gramu 11,934.38 zenye thamani ya shilingi 668,325,550
zilizalishwa hivyo serikali ikajipatia mrabaha wa
shilingi 26,733,020.
Mwaka wa fedha 2011/2012 gramu
14,693.80 zilizalishwa zikiwa na thamani ya jumla ya shilingi 822,852,600 hivyo
serikali ikajipatia shilingi 32,914,104.
Mwaka 2012/2013 zilizalishwa gramu
11,957.93 zenye thamani ya shilingi 669,643,800 hivyo serikali ikapata shilingi
26,785,752 na mwaka wa fedha 2013/2014 zikazalishwa gramu 68,508.93 zenye
thamani ya shilingi 3,836,499,900 na serikali ikajipatia shilingi 153,459,996.
Anasema mwaka wa fedha 2014/2015
zilizalishwa gramu 405,587.81 zilizokuwa na thamani ya jumla ya shilingi
22,712,917,481 na serikali ikajipatia shilingi 908,516,699.24 na mwaka
2015/2016 gramu 308,430.31 zilizalishwa zikiwa na thamani ya shilingi
18,505,818,710.50 na hivyo serikali ikajipatia shilingi 740,232,748.42.
Utengaji wa Maeneo kwaajili ya wachimbaji wadogo
Akizungumzia Utengaji wa Maeneo ya Uchimbaji
mdogo,Bilagi anasema Wizara ya Nishati na Madini ilitoa eneo la Itumbi B lenye
ukubwa wa Kilometa za mraba 12.78 ambapo baada ya kufanyiwa michoro zaidi ya
viwanja 300 vilipatikana.
Anasema pia kwa sasa Wizara imetenga
maeneo ya Mbugani na Chalangwa na mpango wa kuyagawa maeneo hayo utafanyika
mara baada ya Wakala wa Jiolojia Tanzania(GST) atakapofanya kazi ya Utafutaji
wa awali ili kubaini uwepo wa mashapo ya madini.
Changamoto zinazoikabili Ofisi
Kwa mujibu wa Bilagi Ofisi ya
Madini Chunya inakabiliwa na changamoto nyingi ambazo kimsingi zinakwamisha
utendajikazi.Changamoto hizi ni pamoja na Ukosefu wa rasilimali fedha za
kuendesha ofisi.Hii imesababisha kusimama kwa shughuli nyingi za nje ya
ofisi(field activities) kama ukaguzi kwa wachimbaji,watafutaji madini,kutoa
semina katika vijiji na pia kudhibiti wachimbaji haramu.
Umiliki na matumizi holela ya Baruti
ni changamoto nyingine inayohatarisha maisha ya wachimbaji wadogo wa
madini,familia zao na majirani wilayani Chunya.Bilagi anasema baadhi ya
wachimbaji wamekuwa wakitunza baruti majumbani mwao,madukani na baadhi husafiri nazo kwenye gari zao.
“Uhifadhi huu holela ni hatari kwa
maisha ya wachimbaji hao,familia na majirani zao kwakuwa inaweza kusababisha
mlipuko na kuwadhuru watu wanaokuwa jirani”.
Anasema changamoto nyingine iliyopo
ni baadhi ya viongozi na watendaji wa serikali za vijiji kuingilia shughuli za
ofisi ya madini hasa pale wanapotoa vibali kwa wachimbaji kinyume cha sheria.Baadhi
yao wamekuwa wakaidi hata wanapoelimishwa na badala yake wamekuwa wakichochea
migomo kwa wananchi ili wasikubali kutii sheria ya madini ya mwaka 2010.
“Tuna changamoto pia ya baadhi ya
wanakijiji kujimilikisha maeneo ya kuchimb kwa kisingizio kuwa madini yapo
katika mashamba yao.Vile vile hali hii imesababisha baadhi ya wachimbaji
wanaomiliki leseni kisheria kushindwa kuchimba maeneo yao kwa kuhofia kufanyiwa
vurugu na wenyeji”
“Bado pia uchimbaji wa kuhama hama
unaendelea.Hii inasababishwa na wachimbaji wengi kutokuwa na mitaji ya kutosha
ya kufanya utafiti wa kugundua kama maeneo wanayoombea leseni yana mashapo ya
madini ya kutosha ili wachimbe” alisema Bilagi.
Kuwepo kwa Utitiri wa kodi na tozo
nyingi kwa wachimbaji wadogo nalo linatajwa kama changamoto kubwa.Baadhi ya
taasisi zinatoza kodi kubwa zinazoleta manung’uniko kutoka kwa wadau wa
shughuli za madini.Mfano watu wanaosaga mawe wanatakiwa kulipa TRA shilingi
700,000 kwa mwaka,wakilipe kijiji kuanzia kiasi cha shilingi 15,000 hadi 20,000
kwa mwezi na wanatakiwa walipe ushuru halmashauri ya wilaya.
Wachenjuaji wanalalamikia kodi ya
zimamoto ambapo hadi baadhi yao waliwahi kuwekwa mahabusu wakiamriwa kulipa
shilingi 5,000,000 kwa mwaka kama ada ya zimamoto huku wachimbaji wakiwa
hawapati huduma yoyote kutoka jeshi hilo.Kero kubwa ni namna taasisi husika
inavyoidai kwa njia ya shuruti kabla ya kuwaelimisha.
Bilagi anasema katika kutafuta
ufumbuzi wa baadhi ya changamoto,serikali kupitia ofisi ya madini wilaya
imeendelea kutoa Elimu kuhusu sheria ya Madini ya mwaka 2010 ili wananchi waweze
kutambua kuwa unapomiliki ardhi hauna ruhusa ya kumiliki madini yaliyopo bila
kufuata sheria.
Anasema pia Elimu inaendelea
kutolewa kwa wananchi na wachimbaji juu ya namna bora ya kumiliki na kutumia baruti
kwa mujibu wa Sheria ya Baruti ya mwaka 1963
Afisa huyo anasema Serikali ya awamu
ya Tano imedhamiria kuinua hali ya wachimbaji wadogo ili wasiwe wa kuhama hama
hivyo imeiwezesha wakala wa Jiolojia Tanzani(GST) ili wafanye utafutaji wa
awali wa mashapo yenye madini katyika maeneo mbalimbali nchini na Chunya ikiwa
ni miongoni mwa maeneo yaliyopewa kipaumbele.
“Serikali ina mpango wa kujenga
kituo kingine cha kutoa elimu kwa wachimbaji wadogo katika kata ya Mbugani ili
wawe na weledi wa uchimbaji wenye tija.Tunaendelea kutoa huduma ya kuandikisha
wananchi katika mfumo wa leseni wa OMCTP ili kila mchimbaji aweze kuomba leseni
bila ya kuwa na ulazima wa kufika ofisi ya madini”
Anasema kuhusu utitiri wa kodi Ofisi
ya madini Chunya ilikwisha wasilisha kwa Kamishna wa Madini.
Mkuu wa mkoa wa Mbeya Amos Makalla
alipotembelea shughuli za madini na kukutana na wadau wa Sekta hiyo aliahidi
kuendelea kupigania haki za wachimbaji wa madini ili kupunguza adha
zinazoikabili sekta hiyo wilayani hapa.
Monday, September 19, 2016
ELISABENE,SHULE ILIYOANZISHWA KUTOKANA NA MISUKOSUKO YA KIFAMILIA KIELIMU
Na Joachim Nyambo.
“Yapo mambo mengi yaliyonisukuma kuanzisha shule” Ni
sentensi aliyoanza nayo Anivene Lusubilo nilipozungumza naye.Huyu ni mmoja wa
wakurugenzi wa Shule ya Awali na Msingi ya mchepuo wa kingereza ya Elisabene
iliyopo mjini Tunduma wilayani Momba mkoani Songwe.Mkurugenzi mwenza ni mumewe
Frank Shitindi.
Ipo historia ndefu kwa familia ya wanandoa hawa hata
kufikia hatua ya kuwa na taasisi ya kutoa elimu ambayo sasa imekuwa manufaa kwa
jamii pia inayowazunguka na kwingineko nchini nchini.Ni familia yenye watoto
wane wote wakiwa ni mabinti.
“Msukumo wa kwanza nilianza kuupata kutokana na mimi
mwenyewe kupata elimu kwa kuungaunga sana.Hii ilitokana na wazazi wetu
kutotambua sana umuhimu wa elimu”
“Suala la pili ninaye binti yangu ambaye mara baada
ya kumaliza darasa la saba na kupata matokeo mabaya nilihangaika sana kupata
shule ya sekondari ya kumpeleka.Nilimpeleka shule tano binafsi lakini kila
alipofanya usaili alionekana kushindwa.Nilichokibaini ni kuwa alishindwa
kutokana na kuwa na uwezo mdogo wa lugha ya kingereza.Iliniumiza sana,nikawaza
halii kama hiyo ikoje kwa jamii inayonizunguka!” alisema Anivene ambaye ni
mtaalamu wa Kilimo katika halmashauri ya mji wa Tunduma.
“Watoto wote waliofaulu kwenye usaili uliofanyika
kwenye shule nilizompeleka mwanangu nilibainia walitokea katiak shule
binafsi.Nikaona walimu katika shule hizi wanajituma kutokana na kutetea ajira
zao hivyo mwanafunzi atapewa elimu inayostahili.Katika shule za serikali wapo
walimu wanaobweteka na kuona hana cha kupoteza mtoto anapokuwa na maendeleo
mabaya kitaaluma”
Anasema hapo alianza kufikiria kupeleka watoto wake
wote kwenye shule za michepuo ya Kingereza ili wasikumbwe na adha iliyomkuta
dada yao.Alimshawishi mumewe na walianza kuwekeza kidogo kidogo fedha kutoka
katika sehemu ya mishahara yao ya kila mwezi.
“Niligundua
gharama haikuwa kubwa sana kumsomesha mtoto katika shule hizi.Nilimshawishi
mume wangu kila mmoja wetu atenge shilingi elfu ishirini katika mshahara wake
wa kila mwezi.Tukajikuta tunaweza.Yule aliyekuwa darasa la nne na mwezie wa
darasa la kwanza tukawapeleka wote English Medium katika shule moja iliyopo
hapa mkoani kwetu lakini wilayani Mbozi.”
Anasema kuwapeleka watoto katika shule hiyo ya
mchepuo wa kingereza kukampa fundisho jingine ambalo lilizidi kumpanua mawazo
na kuzidisha nia ya kutafuta ufumbuzi.Mazingira aliyokutana nayo yakaonekana
kutomridhisha kama mzazi.
“Kwakweli pamoja na watoto kuendelea kusoma pale
sikuweza kuwa na amani kwakuwa kila tulipokwenda kuwasalimia watoto
hatukuridhishwa sana na mazingira tuliyokutana nayo.Masuala ya lishe,malazi na
pia mazingiara ya shule kwa ujumla.Tukaona kuna kila dalili za watoto
kuambukizana magonjwa kwa urahisi.Hapo tukaamua kuwahamishia katika shule moja
iliyopo jijini Mbeya.”
Wakati haya yakifanyika suala la uchungu wa mzazi
kuishi mbali na watoto wake nalo likajitokeza.Anivene akajikuta anakuwa mpweke
kwa watoto wake kuishi mbali nae.Akahisi watoto pia hawana imani kutokana na
kuishi kwao mbali na wapendwa wazazi wao.Akahisi kuna mambo muhimu wanayakosa.
“Hakuna siku niliyoumia kama nilipokuwa namwacha
mtoto wangu wa mwisho anakwenda kuanza darasa la awali.Kilikuwa kitoto kidogo
mno chenye miaka sita.Kilipoanza kulia nikajikuta na mimi nabubujikwa na
machozi.Nilikosa raha hata baada ya kuwa nimemwacha shuleni.Nilijua uangalizi
ni mzuri lakini nikawaza namba amekuwa akifurahi kila tuamkapo asubuhi.Nikaona
furaha yake sasa itakuwa imepotea na huenda hata masomo ikawa shida kwake.nilibeba
uchungu wa wanawake wote wa eneo hili”.
Wakati huo wote alikuwa akijaribu kutafakari ni
kwanini watu wenye uwezo kwenye maeneo ya jirani hawajataka kuanzisha shule
kama hizo wanazozifuata mbali ili watoto waweze kusoma jirani na makwao?Mji wa
Tunduma una wakazi walio na vipato vizuri kutokana na wengi wao kuwa wafanyabiashara
wakubwa.Lakini hawakutaka kuwekeza katika suala la elimu.Wote wakawa wanapeleka
watoto mbali nao.
“Iliniuma sana lakini ikanibini kuja na wazo
jipya.Ili uweze kuanzisha shule yakupasa uwe na vigezo gani.Hapo ndipo
nilipoanza mchakato wa kufuatilia vigezo vinavyohitajika mpaka pale
niliporuhusiwa na serikali”
Anasema hapo ndipo alipoanza kujenga majengo kwenye
eneo lake lililopo katikati ya mji wa Tunduma ambako kwa sasa yapo madarasa ya
shule ya awali pekee.Mwaka 2012 baada ya kukamilisha majengo hayo nikaanza
kuwaza napataje walimu wa kuanza nao.Mtaji umeishia katika kujenga majengo na
kuboresha mazingira.
“Nilihitaji muda wa kujipanga zaidi mpaka kufikia
kuanza kuajiri na kupokea wanafunzi.Madhari niliyokuwa nimeweka yanayovutia
watoto kwa kuwepo na bembea siku moja yakaniponza.Siku hiyo watoto wawili wa
rafiki yangu waliokuwa wakisoma katika shule moja hapa mjini waligoma kwenda
shuleni kwao.Walimlazimisha mama yake awalete kwenye majengo yetu na wakasema
hawatokwenda shuleni kwao iwapo mama yao hatokubali ombi lao.”
“Mama yao alinipigia simu kuniomba awapeleke kwenye
majengo yetu nikamwambia haiwezekani sisi hatujaanza kufanya kazi hivyo
hatuwezi kuruhusu.Badaye alipoona wanamsumbua sana akanipigia tena simua
akanambia kwakuwa pale kuna walinzi anawapeleka hivyo hivyo ili wakashinde huko
wao wafurahi”
“Wakati akinambia hayo alikuwa tayari njiani
kuelekea huko.Sikuwa na namna zaidi ya kumkubalia.Nilimpigia mlinzi
akawafungulia geti na kuwaruhusu kuingia na mama yao akawaacha hapo.Mpaka nakwenda
niliwakuta wanaendelea kucheza wala hata hawakujali kuwa walikuwa peke yao”anasema.
Anasema hapo akawa na mtihani mpya.Ili mlazimu
atumie pesa yake ya mfukoni kuwanunulia chipsi kwenye kibanda kilichopo jirani
kwaajili ya chakula cha mchana.Baadaye mama yao aliwapitia watoto hao na kurudi
nao nyumbani.Kesho yake hali ilikuwa hivyo hivyo,watoto waligoma kwenda shuleni
kwao ikabidi waletwe shuleni hapo.
“Nikawa na kibarua kigumu.Watoto wa watu wanasinda
kwenye majengo yangu,hakuna mtu wa kuwasimamia,nikaona nina wakati
mgumu.Ilibidi nikutane na mzazi wao ili tulijadili jambo hili kwa pamoja.Ajabu
hakuwa na hofu kama yangu!Akanambia wewe unasubiri nini kutafuta walimu?akasema
tafuta mwalimu aanze kuwafundisha watoto mimi nitakutafutia wanafunzi wengine
kama unashindwa kuwatafuta”
“Nikaona mbona huyu simwelewi!Lakini nikaona huenda
huu ndiyo mwanzo wenyewe.Akanitafutia mwalimu mmoja anaitwa Sarafina.Sikuwa na
kwa kumweka ikabidi niishi nae nyumbani kwangu.Rafiki yangu akashawishi
wafanyabiashara wakaniletea watoto wengine wawili.Hapo nikawa na wanafunzi
wane.Kwakuwa usajiri wa shule tulikuwa
tumepata tayari hatukuwa na mashaka.”
Anasema baadaye waliopata mwalimu mwingine raia wa
Kenya.Lakini hakuweza kudumu shuleni hapo kwakuwa baadaye ilibainika hakuwa ametimiza
masharti ya kufanya kazi nchini hivyo aliondoka.Walilazimika kuendelea
kudunduliza walimu.
“Unajua tatizo kubwa tulilonalo hapa nchini ni
kupata walimu walio na uwezo.Si kwamba walimu hawapo!wapo wengi tu lakini uwezo
ni tatizo.Na hii ndiyo inasababisha shule zetu kuwa na ushindani mkubwa wa
kuwapata walimu wenye kuiwezesha taasisi yako kufanya vizuri”
Anasema kupenda kwake kujifunza kulimfanya azidi
kupanua wigo wa uelewa kila mara aliposafiri.Alipenda kutembelea shule
mbalimbali zinazotoa elimu sawa na ya shuleni kwake.Na kila jambo jipya
alilojifunza aliangalia namna ya kuliongeza kwenye taasisi yake.
“Kutokana na ugumu wa kupata walimu kuna wakati
ilinilazimu kwenda Dar es salaam na kukaa huko kwa majuma mawili nikiwatafuta
wanaoweza kuja kunisaidia.Hapo ndipo nilipokutana na mwalimu David Buyogela
ambaye sasa ndiye Mkuu wa shule.Nakumbuka ilikuwa mwaka 2013.Wakati huo pia
mpaka nafanya mazungumzo na mwalimu huyu nilikuwa naumwa na kabla sijarudi
ilibidi nifanyiwe upasuaji”
Kwakuwa mtazao wa familia hii ulikuwa ni kuwa na
shule ya awali na Msingi zilizokamilika,waliamua kutumia eneo walilokuwa nalo
nje ya mji kidogo litumike kwaajili ya kujenga shule ya msingi.Hapo ujenzi
ulianza na baada ya kuziona taasisi za kifedha zikakubali kutukopesha fedha.
Anivene anasema kujua namna ya kutawala imekuwa
chachu ya mafaniko kwenye taasisi yao kwani hadi sasa walimu na wanafunzi
wamezidi kuongezeka.Wapo wanaohamia wakitokea katika shule nyingine na pia wale
wanaoanza awali kila mwanzo wa mwaka wa masomo.
Mkuu wa shule mwalimu Buyogela anasema hivi sasa
shule ina jumla ya wanafunzi 255 kwa maana ya kuanzia darasa la awali hadi
darasa la tatu.Darasa la awali wapo 114
wasichana wakiwa 58 na wavulana 56,darasa la kwanza wako 71 wavulani 37
na wasichana 34.Darasa la pili waapo 54,wasichana 31 na wavulana 23 na darasa
la tatu wako 16 wasichana 11 na wavulana watano.
“Wapo watoto wanaohamia kutoka shule nyingine.Hawa
tunawasaili na kuona uwezo wao iwapo unaridhisha anaendelea na darasa alilokuwa
huko alikotoka na iwapo tutaona kiwango chake hakiridhishi tunaongeza na mzazi
au mlezi kumrejesha darasa moja.Lengo ni kumjengea uwezo kitaaluma aweze kwenda
sambamba na wenzie darasani” anasema Buyogela.
“Kama watumishi tumekuwa na jambo la kujivunia
kutokana na mahusiano mazuri baina yetu na mwajiri.Baadhi ya waajiri hawapedi
kupokea maoni ya wafanyakazi wao.Kwa hapa hali ni tofauti,tunasikilizwa na
tunajiona sehemu ya taasisi.”
Baadhi ya wanafunzi shuleni hapa Tecla Almasi,Moses
Ndaga na Jesca Korogwe wote wa darasa la tatu,wanasema mazingira ya utoaji
elimu yanayokwenda sambamba na kupata chakula yanawawezesha kupata fursa nzuri
ya kuwaelewa walimu wao.
Tecla na
Moses wanasema walihamia shuleni hapa wakitokea shule tofauti lakini tofauti na
walikotoka hapa wameongeza uwezo kitaaluma.Wanasema huenda mazingira ya walimu
kuwajali na uwepo wa miundombinu rafiki ya kufundishiwa imekuwa chachu ya
mafanikio yao tofauti na awali.
Uwepo wa uwekezaji shule ya Elisabene umekuwa chachu
ya maendeleo kwa watu mbalimbali.Zipo ajira zilizozalishwa kama za
walimu,madereva,wapishi,walinzi,watu wa usafi na utunzaji bustani,ujenzi wa
majengo,ufyatuaji tofali na nyingine nyingi.
“Wananchi waishio jirani na shule pia tunawapa maji
kutoka katika kisima kirefu tulichochimba hapa shuleni.Tunashiriki pia katika
shughuli za kijamii kwa kuchangia michango mbalimbali.Tunaamini jamii
inayotuzunguka ni sehemu yetu” anasema mkuu wa shule.
Pamoja na mafanikio yaliyofikiwa bado kuna
changamoto zinazoikabili shule hii.Miongoni mwa changamoto hizo ni pamoja na
mtoto kuletwa akiwa amechelewa kuanza shule,mzazi kutaka mtoto aingie darasa la
juu japo hana uwezo akiona kumrudisha darasa atapata hasara.Pia kutokuwepo kwa
hostel kunasababisha wanafunzi kukosa muda wa kutosha kupumzika akiwa katika
mazingira ya shule.
“Kama watumishi tunataraji utawala unafanyia kazi
suala la Usafiri wa watumishi,kujenga nyumba za wafanyakazi,Kujenga
hosteli,kupata fursa ya kujiendeleza kielimu,kushiriki semina za mara kwa mara
ili kujijengea uzoefu na pia kutuunganisha na taasisi za kifedha ili kupata
mikopo na pia mifuko ya kijamii”anasema Buyogela.
Mkurugenzi wa shule anasema changamoto za kiutawala
ni pamoja na wazazi kutolipa ada kwa wakati licha ya kuwa wazazi wengi wanao
uwezo mzuri kiuchumi,upatikanaji wa walimu,kutofikiwa kwa miundombinu ya maji
na maji katika eneo la shule ya msingi hivyo kulazimu kutumika kwa jenereta na
kisima cha kuchimbwa.Taasisi za kifedha kutoza riba kubwa kwenye mikopo.
“Tuna changamoto kubwa ya mtazamo hasi wa serikali
juu ya fedha binafsi,inaamini kuwa zinapata faida kubwa na hapo ndipo
tunapolundikiwa mzigo wa kodi lukuki zikiwemo za majengo,TRA,fedha za
ukaguzi,kulipia majengo.Hapa tunaona kama hakuna mahusiano mazuri baina ya
serikali na shule binafsi”
“Lakini kuna suala la wazazi kutowajibika na watoto
wao.Wapo ambao hawajawahi kufika hapa shuleni tangu watoto wao waanze kusoma
hapa.Hawaulizii maendeleo ya watoto wao na wala hawawaandai watoto wanapokuja
shule.Mtoto anakuja ukimuona tu utajua huyu anaumwa lakini unapompigia mzazi
anakuwa hajui lolote na amemruhusu aje shule siku hiyo.Mtoto mwingine utakuta
amekuja na nguo chafu ni kama hakutokea kwa mzazi.Hii yote ni kutokana na
wazazi kutowajali watoto” anasema Anivene.
Mkurugenzi huyu anasema matarajio ya taasisi hii ni
kujenga hosteli ili watoto waweze kukaa shuleni japo ni kwa wale
watakaopenda.Japo hii ni changamoto kwake kwani awali alipenda mtoto aje kusoma
na jioni aungane na familia yake.
Kuanzisha shule ya sekondari kutategemea mwenendo
mzuri wa mafanikio ya shule ya msingi.Japo ni muhimu kwakuwa itasaidia watoto
wanaomalisha shuleni hapo kuendelea na masomo ya sekondari wakiwa katika
mazingira waliyoyazoea tofauti na kwenda shule nyingine.
Mtazamo wa Serikali ya mkoa wa Songwe ni kuona
uwekezaji katika Nyanja mbalimbali ikiwemo sekta ya Elimu unaimarishwa.Hii
itasaidia jamii ya wakazi mkoani hapa kujikwamua na kuondokana na maadui
Ujinga,Maradhi na Umasikini pale watakapokuwa na elimu ya kutosha.
“Tunataka kuwaondoa wakazi wa mkoa wa Songwe kwenye
Unyonge.Wana fursa nyingi za uzalishaji mali lakini bado ni wanyonge na ili
kuwaondoa kwenye hali hii lazima tuwape elimu”alisema mkuu wa mkoa wa
SongweLuteni mstaafu Chiku Galawa alipozungumza na wanachama wa Chama cha
Waandishi wa Habari za Utalii na Uwekezaji Tanzania(TAJATI).
Kwa upande wake kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru
kitaifa,George Mbijima,alipokimbiza mwenge shuleni hapa alipongeza waasisi wa
shule ya Elisabene akisema jamii inapaswa kujikita katika uwekezaji wa
kujikomboa kutoka kwenye adui Ujinga.
Subscribe to:
Posts (Atom)