WAFANYABIASHARA mkoani Mbeya wamehimizwa kutumia
fursa ya uwepo wa kiwanda cha bia cha TBL mkoani kwao kwa kujihusisha na
biashara zenye mahusiano na kiwanda hicho ili waweze kunufaika na uwepo wake.
Miongoni mwa fursa zilizopo ni pamoja na kuanzisha
viwanda kwaajili ya kusaga unga wa mahindi utumikao katika kutengenezea bia.
Meneja wa kiwanda cha TBL Mbeya Waziri Jemedari alitoa
hamasa hiyo alipozungumza na wanahabari mkoani hapa kwenye shindano la kuonja
na kutambua ladha ya bia lililofanyika kiwandani na kuwashirikisha wanahabari
kutoka vyombo mbalimbali.
Jemedari alisema bado wafannya biashara na wakulima
mkoani Mbeya hawajaitumia vyema fursa ya uwepo wa kiwanda hicho hatua
inayopelekea wenzao kutoka maeneo ya mbali kunufaika na fursa hiyo.
Alisema licha ya mkoa wa Mbeya kuwa miongoni mwa
mikoa inayozalisha kwa wingi mahindi,bado kiwanda hicho kinalazimika kuagiza
unga kutoka Arusha,Iringa,Kibaigwa na Dar es salaam.
“Wafanyabiashara wa Mbeya bado wamejikita katika
biashara nyingine ikiwemo ya kununua nafaka kutoka kwa wakulima na kuziuza tena
pasipo kuziongezea thamani.Hii inatulazimu kuagiza unga wa mahindi wa dona
kutoka mbali wakati hapa mahindi yanalimwa kwa wingi.”
“Nadhani hawajatambua uwepo wa kiwanda hiki
unavyoweza kuwanufaisha.Hatuwezi kufungua viwanda vya kusaga unga wa dona
kwakuwa tutakuwa tunawanytima wengine fursa.Sisi tunatengeneza bia,tunahitaji
wadau wengine wa kutuzalishia malighafi za kulisha kiwanda chetu” alisisitiza.
Alisema kwa sasa mahitaji ya unga wa mahindi wa dona
kiwandani hapo ni mkubwa ambapo jumla ya tani 30 hutumika kwa kila juma moja
hivyo ni fursa nzuri kwa watakaopenda kuwekeza kwenye uzalishaji wa malighafi
hiyo.
Alisema TBL iko tayari kukutana na mfanyabiashara
yeyote atakayeonesha nia ya kuwekeza katika biashara hiyo na itahakikisha
inampa mwongozo juu ya namna gani malighafi inayohitajika na kiwanda
inavyopaswa kutengenezwa.
Aliitaja fursa ya kilimo cha Shayiri kuwa faida
nyingine ambayo wakazi wa Mbeya hawajawekeza ipasavyo kwani hadi sasa kwa
mkoani hapa ni wakulima wa wilaya ya Mbozi pekee wanaozalisha huku kiwanda
kikilazimika kununua bidhaa hiyo kutoka maeneo mengine ikiwepo Sumbawanga
mkoani Rukwa.
Alisema licha yak ampuni kutoa fursa ya kuwawezesha
wakulima katika shughuli mbalimbali za uzalishaji wa zao hilo,bado mwitikio wa
wakulima mkoani hapa ni mdogo mno katika kilimo cha zao la Shayiri wakati soko
ni la uhakika.
Katika shindano la kuonja bia,mtangazaji wa Mbeya FM
David Nyembe anayekabidhiwa katoni ya bia aina ya Kilimanjaro Twist pichani aliibuka mshindi akifuatiwa na mwakilishi wa ITV mkoani hapa
Emmanuel Lengwa aliyeshika nafasi ya pili.
No comments:
Post a Comment