Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Monday, September 14, 2015

UKIRITIMBA WAKWAMISHA HALMASHAURI RUNGWE

KUTOFANYA kazi kwa umoja kwa watendaji katika halmashauri ya wilaya ya Rungwe kumetajwa kuwa chanzo cha kudorola kwa utendaji kazi ndani ya halmashauri hiyo.

Mkuu wa mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro alisema jana kuwa taarifa alizonazo ni kuwa watendaji ndani ya halmashauri hiyo hawana ushirikiano hata kidogo na badala yake kila mmoja anatekeleza majukumu yake kivyake.

Hali hiyo ilijidhihirisha wazi pale watendaji walipotakiwa kujibu maswali yaliyohojiwa na mkuuu wa mkoa yaliyotokana na hoja za mkaguzi na ndipo kila afisa akaonekana kuwa na majibu yake na kuleta mkinzano ndani ya kikao.

“Inaonekana hamfanyi kazi kama timu.Ninazo habari kuwa hakuna umoja kati yenu.Kila mmoja anafanya mambo yake ajuavyo yeye.” Alisema Kandoro kwenye kikao cha kupitia taarifa ya Mdhibiti na mkaguzi wa hesabu za serikali(CAG) katika mwaka wa fedha 2013/2014.

Kandoro alisema hali hiyo ndiyo inayochangia kwa kiasi kikubwa kukwama kwa shughuli za kimaendeleo na kuzalisha hoja nyingi za kiukaguzi zisizo za msingi ndani ya halmashauri hiyo.

Aliwataka watendaji wa halmashauri hiyo kutambua kuwa kufanya kazi kama timu ndiyo silaha pekee inayoweza kumwezesha kila mmoja wao kuonekana anawajibika katika nafasi yake na hivyo maendeleo ya wananchi kupatikana kwa urahisi.

Alisema anahitaji kuona wanafanya kazi kama timu kuanzia ngazi ya mkurugenzi mtendaji,menejimenti,watendaji na mpaka kwenye kata na vijiji huku wakitambua kuwa kilichowakutanisha ni kuwatumikia wananchi wa Rungwe.

Akizungumzia suala la udhibiti wa mapato ya ndani,Kandoro alisema bado inaonekana kuwepo kwa mianya ya upotevu wa fedha hivyo si kiasi chote kinachokusanywa na halmashauri kinakwenda sehemu sahihi na kuitaka ofisi ya katibu tawala mkoa kulifanyia kazi suala hilo.

Mkuu huyo wa mkoa pia aliagiza kutafutwa kwa ufumbuzi wa haraka juu ya malalamiko yaliyofikishwa kwake na watumishi wa halmashauri hiyo wakiwemo wa idara ya afya wanaolalamikia kukatwa mishahara yao pasipo sababu za msingi.

Alisema hali hiyo inakwamisha utendaji kazi wa watumishi na menejimenti kubaki ikitoa visingizio visivyo vya msingi pale inapobainika wananchi kutopata huduma kikamilifu kwenye idara husika.

No comments:

Post a Comment