JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI
JESHI LA POLISI TANZANIA.
Ofisi ya Kamanda wa Polisi,
Mkoa wa
Mbeya,
Namba ya simu 2502572
S. L. P. 260,
Fax - +255252503734
MBEYA.
E-mail:- rpc.mbeya@tpf.go.tz
TAARIFA YA JESHI LA POLISI MKOA WA MBEYA KWA VYOMBO VYA HABARI
“PRESS RELEASE” TAREHE 04.01.2017.
Jeshi la Polisi mkoa wa Mbeya limeendelea kufanya
misako, operesheni na doria zenye tija katika maeneo mbalimbali ili kudhibiti
uhalifu na wahalifu na limekuwa likishirikiana na wananchi na wadau wengine
katika jitihada hizo za kukabiliana na uhalifu na wahalifu na kupata mafanikio
makubwa ikiwa ni pamoja na kupungua kwa matukio makubwa ya uhalifu. Mafanikio
yaliyopatikana katika Misako ni kama ifuatavyo:-
KUKAMATA MTUHUMIWA KWA KOSA LA KUFUKUA
KABURI.
Mnamo tarehe 04.01.2017 majira ya saa
01:00 usiku huko katika Kijiji cha Mumba kilichopo Kata ya Ilembo, Tarafa
ya Isangati, Wilaya ya Kipolisi Mbalizi, Mkoa wa Mbeya, Mtu mmoja aliyefahamika
kwa jina la JONAS JOHN [28] mkazi wa
Chapakazi alikamatwa na askari Polisi akiwa na wenzake wawili wakifukua kaburi la
marehemu SISTER OSISARA aliyekuwa
mlemavu wa ngozi (ALBINO) kwa lengo la kuchukua viungo vyake.
Inadaiwa
kuwa marehemu alifariki dunia mwaka 2010 kwa ugonjwa wa homa na kuzikwa katika
makaburi ya Kijiji cha Mumba. Mtuhumiwa alikutwa na majembe na makoleo ambayo
walikuwa wakiyatumia kufukuria kaburi hilo. Baada ya mahojiano mtuhumwa huyo
aliwataja washirika wenzake wawili ambao walikimbia baada ya kuwaona askari.
Msako mkali wakuwatafuta watuhumiwa unaendelea.
Mnamo tarehe 03.01.2017 majira ya saa
21:30 usiku huko Mtaa wa Makongolosi, Kata ya Makongolosi, Tarafa ya
Kiwanja, Wilaya ya Chunya, Mkoa wa Mbeya, mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la KELVIN KUBANDA [24] mkazi wa Kahama alikamatwa
akiwa na bhangi kete 10 sawa na uzito
wa gramu 55.
Mtuhumiwa
alikamatwa akiwa katika kijiwe cha kuvutia Bhangi. Upelelezi unaendelea.
WITO:
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Naibu Kamishna wa
Polisi DHAHIRI A. KIDAVASHARI anatoa
wito kwa jamii kuacha tamaa mali/fedha kupitia njia zisizo halali kwani Jeshi
la Polisi halitaruhusu wala kufumbia macho vitendo kama hivyo na badala yake
wajishughulishe na kazi halali kwa lengo la kujipatia kipato halali kuendesha
maisha yao. Aidha Kamanda KIDAVASHARI anatoa
wito kwa vijana na jamii kwa ujumla kuachana na matumizi ya dawa za kulevya
kwani ni kinyume cha sheria na ni hatari kwa afya ya mtumiaji. Pia anaendelea
kutoa wito kwa wakazi wa Mbeya kutoa taarifa za mtu/watu au kikundi cha watu
wanaojihusisha na vitendo vya uhalifu kwa hatua zaidi za kisheria.
Imesainiwa
na:
[DHAHIRI A.
KIDAVASHARI - DCP]
KAMANDA
WA POLISI MKOA WA MBEYA.
No comments:
Post a Comment