ZAIDI ya wanafunzi 60 wa kidato cha
nne katika shule ya sekondari ya Seminari ya Kidugala, inayomilikiwa na Kanisa
la Kiinjili la Kilutheli Tanzania (KKKT), wamefukuzwa shule kwa madai ya
kutolipa ada na michango mbalimbali.
Miongoni mwa michango ambayo
wanafunzi hao wanadaiwa ni pamoja na mchango wa kununulia basi, mchango wa
kambi wakati wa likizo ya mwezi wa sita, na mingineyo mingi.
Lyamba Lya Mfipa imeshuhudia
wanafunzi wakihangaika kuwasiliana na wazazi wao, baada ya kushushwa Njombe
mjini toka katika kijiji cha Kidugala, iliko shule hiyo ili watumiwe nauli.
“Tunahangaika kuwatafuta wazazi wetu
walio mbali na Njombe ili watutumie nauli turudi nyumbani kwa sababu tumelipa
ada kidogo, sio milioni 1.7 wanayoitaka walimu,mimi nimelipa Sh laki nane
lakini nimefukuzwa,”alisema mmoja wa wanafunzi hao.
wazazi wa wanafunzi hao waliiomba serikali kuingilia kati tatizo la walimu wa shule hiyo kuwafukuza wanafunzi, na kuwatelekeza mijini jambo ambalo ni hatari.
“Unapomfukuza mtoto bila kuwasiliana
na mzazi unataka afanye nini, tunasikitishwa na jambo hili,” alisema Anitha
Mgeni, mkazi wa mtaa wa Mgendela, Njombe mjini baada ya kuwapokea watoto
watatu, akiwahifadhi nyumbani kwake ili wawasiliane na wazazi wao.
Mzazi huyo alidai kuwa shule hiyo
ilijengwa na waumini wa KKKT kwa lengo la kuwasaidia watoto wa watu maskini,
lakini kwa sasa imekuwa ikitoza ada kubwa kuliko matarajio ya waumini hao.
Mwalimu Mkuu wa shule ya sekondari
ya Kidugala, Jackson Ngilangwa alikiri wanafunzi wengi kudaiwa ada, na kwamba
hakuwepo shuleni wakati wanafunzi hao wanafukuzwa.
Akizungumza kwa njia ya simu,
Ngilangwa alisema michango na ada ambazo wanafunzi hao wanatakiwa kulipa ni ile
ya msingi.
“Mimi nipo kwenye semina sipo
shuleni, ngoja niwasiliane na makamu mkuu wa shule kuona kwa nini amewafukuza
wanafunzi hao,”alisema.
No comments:
Post a Comment