Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Tuesday, March 10, 2015

ALBINO ALIYEKATWA KIGANJA AHAMISHIWA RUFAA MBEYA,WAKUU WA MIKOA YA MBEYA NA RUKWA WAMTEMBELEA KUMFARIJI



Mkuu wa mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro na mkuu wa mkoa wa Rukwa Mhandisi Stella Manyanya wakimwangalia mtoto Baraka Cosmas(6) mwenye ulemavu wa ngozi(albino) aliyelazwa katika hospitali ya Rufaa kanda ya Mbeya baada ya kukatwa kiganja cha mkono wa kulia na watu wasiofahamika walipomtembelea jana.



 Mkuu wa mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro na mkuu wa mkoa wa Rukwa Mhandisi Stella Manyanya wakisali pamoja na viongozi wa Chama Cha watu wenye ulemavu wa Ngozi(albino) katika wadi ya watoto walipofika kumjulia hali mtoto Baraka Cosmas.
 Mama wa mtoto Baraka, Priscar Shaban(28)akielezea namna alivyovamiwa nyumbani kwake na kisha mwanaye huyo kukatwa kiganja




                           HABARI KAMILI
WAKUU wa mikoa ya Mbeya na Rukwa,Abbas Kandoro na Stella Manyanya jana walimtembelea mtoto Baraka Cosmas(6) mwenye ulemavu wa ngozi(albino) aliyelazwa katika hospitali ya Rufaa kanda ya Mbeya baada ya kukatwa kiganja cha mkono wa kulia na watu wasiofahamika.

Mtoto huo mkazi katika kijiji cha Ikonda kata ya Chitepa wilayani Sumbawanga mkoani Rukwa alihamishiwa katika hospitali ya Rufaa Mbeya baada ya kukatwa kiganja chake akitokea kituo cha Afya cha Kamsamba wilayani Momba.

Kwa mujibu wa mama wa mtoto huyo Prisca Shaban(28) tukio hilo lilitokea juzi majira ya saa saba usiku ambapo alipokuwa anarudi ndani akitokea nje kujisaidia alivamiwa na mtu ambaye hakumfahamu na kisha akamsukumia ndani kabla ya kumpiga kichwani kwa rungu na kisha kupoteza fahamu.

Mama huyo alisema akiwa amepoteza fahamu mtu aliyekuwa amemvamia ndipo alipata nafasi ya kuingia ndani na kutekeleza adhma yake ya kumkata kiganja mmoja wa watoto watatu wenye ualbino katika familia hiyo na kuondoka nacho.

Alisema wakati hayo yakitokea mumewe aliyemtaja kwa jina la Cosmas Lusambo alikuwa amekwenda kulala nyumbani kwa mke mdogo kwani ilikuwa zamu ya kwenda kulala huko kwa usiku huo lakini baada ya kusikia mayowe ya kuomba msaada alikwenda kuungana na familia yake na kumpeleka mtoto kituo cha afya cha Kamsamba kwani ndicho kilichopo jirani na kijiji chao.

Akizungumza bada ya kumtembelea mtoto Baraka katika wodi ya watoto kwenye hospitali ya rufaa kanda ya Mbeya,Mkuu wa mkoa wa Rukwa Mhandisi Manyanya alioneshwa kusikitishwa na tukio hilo na kuahidi kulifanyia kazi ili wahusika wapatikane na kuchukuliwa hatua.

“Ni tukio ambalo kwakweli linasikitisha mno.Nchi yetu inazidi kuendeleza vitendo vya aibu kwa kuwafanyia ukatili wa kinyama albino kwa ujinga wa watu wachache wanaowadanganya watu kuwa viungo vyao ni bahati ya kuleta utajiri” alisema

Mhandisi Manyanya ambaye pia aliongoza sara fupi ya kuwaombea albino hospitalini hapo alionesha pia kusikitishwa na mwenendo wa mashitaka ya watu waliofanya ukatili dhidi ya albino akisema mahakama zimekuwa na milolongo mirefu inayokatisha tama wadau wa kupinga ukatili huo.

Alitolea mfano kwa tukio lililotokea  mwaka juzi ambapo mkazi wa kijiji cha Miangalua wilayani Sumbawanga Mary Chambanenge alikatwa mkono na baadaye wahusika walikamatwa lakini hadi leo hukumu haijatolewa.

Alihoji kwa nini mahakama iendelee kutoa visingizio vya kutokuwepo kwa ushahidi wa kutosha ilikhali wahusika walikwenda kuonesha mahali walikokuwa wameufukia mkono uliokatwa.

Mkuu huyo wa mkoa alishauri pia kuangaliwa upya kwa sheria inayohusu masuala ya hukumu za kifo akisema ikibidi inapaswa kubadilishwa ili iweze kutoa haki kwa watu wanaofanya ukatili dhidi ya wenzao.

Alisema sheria ya sasa kumtaka rais pekee kuwa mtu wa mwisho kutoa uamuzi kunyongwa kwa mtu aliyehukumiwa inakosa nguvu ya kutekelezwa kutokana na majukumu mengi aliyonayo na kushauri kuwa ni vyema vyombo vya sheria vipewe mamlaka ya mwisho ya kutekeleza adhabu hiyo.

Kwa upande wake Kandoro alisisitiza jamii kuendelea kushirikia katika ulinzi wa albino badala ya kuviachia vyombo vya sheria pekee huku pia akivitaka vyombo vya habari kuendelea kutoa elimu badala ya kuishia kuripoti  matukio yanapotokea.

Aliwataka pia wakazi mkoani Mbeya kutobweteka kwakuwa matukio kama hayo hayajatokea,badala yake wachukue tahadhari na kuongeza ushirikiano wa ulinzi na pale wanapokuwa na shaka juu ya uwepo wa watu flani kwenye maeneo yao watoe taarifa.

No comments:

Post a Comment