Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Saturday, March 7, 2015

BODABODA MBEYA WAPAZA SAUTI,WADAI KUONEWA NA MAMLAKA

 
 
 KATIBU wa Bodaboda mkoa wa Mbeya, MSUMBA MDESA, akitoa tamko kwa niaba ya waendesha Boda boda mkoa wa Mbeya.
 
 
 
                      HABARI KAMILI
 
WAKATI zoezi la kubadili namba za pikipiki kutoka T kwenda MC likitarajiwa kufika kikomo Machi 31, Mwaka huu, Madereva na wamiliki Mkoa wa Mbeya wametangaza mgomo wa kuendelea na zoezi hilo kwa madai kuwa wanatozwa gharama kubwa tofauti na ambazo zilitangazwa na Serikali.
 
Wakizungumza wakati wakitoa tamko kwa vyombo vya habari katika mkutano uliofanyika jana kwenye ukumbi wa Coffee Garden uliopo jijini Mbeya na kuhudhuriwa na viongozi wa Bodaboda kutoka Wilaya nane za Mkoa wa Mbeya walisema hawatakuwa tayari kuendelea na zoezi hilo hadi serikali itakapolitafutia ufumbuzi.
 
Akisoma tamko hilo, Mwenyekiti wa Umoja wa Bodaboda Mbeya, Vicent Mwashoma, alisema Serikali ilitangaza kuanza kubadili namba za pikipiki na bajaji ili kuzitofautisha na magari kwa gharama ya shilingi 10,000 na kutoa miaezi sita ya kufanya zoezi hilo ikiwa ni kuanzia mwezi Oktoba mwaka jana hadi Machi Mwaka huu.
 
Mwashoma alisema lakini wakati zoezi hilo likiendelea wakaanza kukutana na vikwazo kutoka Mamlaka ya Mapato(TRA) na kujikuta gharama zinakuwa kubwa tofauti na ile iliyotangazwa na Serikali ambapo mtu mmoja hulipishwa hadi shilingi 550,000 na kima cha chini kufikia 120,000.
 
Alisema kutokana na kuongezeka kwa gharama hizo kinyume na tangazo la Serikali kupitia kwa Waziri wa Fedha aliyotangaza bungeni wakaona ni vema kuomba ufafanuzi kutoka kwenye uongozi wa Mamlaka ya Mapato (TRA) Mkoa wa Mbeya katika mkutano uliofanyika Februari 26, mwaka huu.
 
Alisema katika Mkutano huo Meneja wa TRA Mkoa wa Mbeya aliwafafanulia kuwa gharama hizo zinatokana na malipo ya usajili kuwa 10,000 kama ilivyopangwa lakini mwenye pikipiki anapaswa kulipia kibaocha kubandikia namba shilingi 19,000, ada ya zima moto shilingi 10,000 na kodi ya kubadili jina la umiliki(Transfer tax) shilingi 50,000.
 
Mwenyekiti huyo aliongeza kuwa Wanachama wa boda boda Mbeya wako tayari kubadili namba za pikipiki zao kwa gharama ya shilingi 10,000 na si vinginevyo kutokana na kuwa na mlundikano wa ushuru anaopaswa kulipia kwa mwaka.
 
Alifafanua kuwa kwa Mwaka pikipiki moja kwa mwaka hulipiwa kati ya Shilingi 154000 hadi 204000 ambazo zinatokana na ushuru wa maegesho shilingi 72,000, Leseni ya Sumatra shilingi 22000,Ada ya zimamoto shilingi 10000 na Bima kati ya Shilingi 50,000 hadi 100,000.
 
Baadhi ya Wanachama wa Bodaboda waliohudhuria Mkutano huo wakiwa na mabango mbali mbali walisema Serikali ilikuwa na mpango mzuri wa kuongeza ajira kwa vijana  kwa kuruhusu uendeshaji wa boda boda lakini jambo hilo linaonekana kuanza kuvurugwa na kupelekea vijana wengi kuachana na biashara hiyo.
 
Madereva hao ambao majina yao hayakupatikana haraka walisema awali kabla ya kuanza kuendesha bodaboda vijana wengi ndiyo walikuwa wakijihusisha na upigaji wa nondo na uhalifu mkoani Mbeya hivyo kitendo cha kuanza kuwanyanyasa tena kinaweza kurudisha hali hiyo kama ilivyokuwa awali.

No comments:

Post a Comment