Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Saturday, August 22, 2015

MBUNGE AHAMA VYAMA VITATU KWA WIKI MOJA

KATIKA kuonesha kinachopiganiwa  si kuwatumikia wananchi bali maslahi binafsi,aliyekuwa mbunge wa Mbarali mkoani Mbeya kupitia Chama Cha Mapinduzi(CCM) Modestus Kilufi amejikuta anakuwa mwanachama wa vyama vitatu tofauti katika kipindi cha wiki moja akitafuta nafasi ya kutetea nafasi ya ubunge.

Safari ya kuhama kwa Kilufi ilianzia katika viwanja vya Ruanda Nzovwe jijini Mbeya ambapo mbunge huyo aliyemaliza muda wake aliutumia mkutano wa mgombea wa urais kupitia Chadema Edward Lowasa kutangaza kuhama rasmi CCM na kuhamia chama hicho baada ya kushindwa katika kura za maoni.

Hata hivyo makazi ya Kilufi ndani ya Chadema yakashindikana kuwa ya kudumu kwani pamoja na ushawishi wote alioufanya kwa uongozi ndani ya chama hicho katika ngazi za Taifa mkoa na wilaya alijikuta anagonga mwamba baada ya wafuasi wa chama hicho kumzuia kuingia ofisi ya msimamizi wa uchaguzi alipokwenda kuchukua fomu.

Taarifa kutoka Mbarali zinaeleza kuwa juzi kunako majira ya jioni(Agosti 20) wanachama wa Chadema walimzuia Kilufi kuingia kwenye ofisi za msimamizi kwakuwa walitaka nafasi hiyo ibakie kwa mgombea Liberatus Mwang’ombe ambaye tayari alikuwa amekwishachukua fomu baada ya kushinda kwenye kura za maoni ndani ya chama ambako Kilufi hakushiriki.

Baada ya kushawishiwa na kundi la wafuasi wake jana(Agosti 21) Kilufi aliiona Chadema si pahala sahihi tena na akajikuta anaangukia mikononi mwa chama cha ACT Wazalendo na majira ya saa nane mchana alikwenda kuchukua fomu ya kugombea kupitia chama hicho.

Akiwasiliana kwa njia ya simu na mwandishi wa habari hizi,msimamizi wa uchaguzi jimbo la Mbarali Adam Mgoi alithibitisha Kilufi kuwa miongoni mwa wagombea nane waliochukua fomu kugombea ubunge na kubainisha kuwa amechukua kupitia chama cha ACT Wazalendo.

Akizungumzia kuhama kwa mwanachama aliyedumu naye kwa takribani siku sita,mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Mbeya Josef Mwachembe China alisema anamuona Kilufi kama msaliti anayeendeshwa na msukumo wa watu wachache.

China alisema Kilufi ni miongoni mwa wanasiasa wasio na msimamo na wasio wazalendo kwa taifa lao na ndiyo sababu anapigania maslahi yake binafsi badala ya maslahi ya watanzania wanyonge.

Mwenyekiti huyo ambaye juzi alionekana kutwa nzima wakiwa na Kilufi katika mitaa mbalimbali ya jiji la Mbeya wakifanya mikakati ya mapinduzi ya mgombea wa ubunge Mbarali kupitia Chadema alikana uongozi kununuliwa na mbunge huyo ili ushinikize kumkabidhi nafasi ya kupeperusha bendera ya chama kwenye uchaguzi.

Hata hivyo China alikiri kuwa maagizo ya chama kumpokea Kilufi yalitokea ngazi ya juu yaani makao na kamwe haikuwa ridhaa ya wanachadema wilaya wala mkoa na ndiyo sababu hata uongozi wa Chadema ngazi ya kanda haukuwa na taarifa.

Hata hivyo ujio ndani ya ACT ulionekana kuleta mkanganyiko kwa uongozi ngazi ya wilaya kwani ulipopigiwa simu ulionekana kugawanyika ambapo Mwenyekiti Anzuruni Rashid Anzuruni alisema anachojua ni kuwa mtu aliyechukua fomu kupitia chama hicho ni James Kamanga na Kilufi hamtambui huku katibu wake Erasto Sanga alithibitisha kumpokea Kilufi na kutengua uteuzi wa mgombea wa kwanza.


No comments:

Post a Comment