Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Friday, March 18, 2016

Sasyaka sekondari mkombozi anayechelewa kutua Mbeya vijijini

Na Joachim Nyambo.

NI miaka mitatu sasa imepita tangu wakazi wa kata ya Masoko wilayani Mbeya walipochukua uamuzi wa kujenga shule ya sekondari.Lengo la wakazi hawa ilikuwa kutekeleza adhma ya serikali ya kila kata kuwa walau na shule moja ya sekondari.

Sekondari ya kata ya Masoko ijulikanayo kama Shule ya sekondari ya Sasyaka ilianza kujengwa mwaka 2013 lakini mpaka leo haijaanza kutumika.Kutoanza kufanya kazi kwa shule hii kunasababisha wanafunzi wanaofaulu katika shule za msingi zilizopo kwenye kata ya Masoko kwenda kuanza masomo ya sekondari kwenye shule za sekondari za kata za Shisyete na Ilembo.

Hii huwalazimu wanafunzi hao kwenda kuishi mbali na wazazi wao katika vyumba vya kupanga au kulazimika kutembea umbari mrefu wa zaidi ya kilometa 20 kwa siku kwenda na kurudi shuleni.

Mbunge wa jimbo la Mbeya vijijini Oran Njeza anasema kilio kikubwa cha wakazi wa kata ya Masoko ni kukosekana kwa shule ya sekondari.

Anasema kutokana na kukosekana kwa sekondari,wanafunzi wanaofaulu kujiunga na kidato cha kwanza wamekuwa wakilazimika kupangiwa shule zilizopo kwenye kata nyingine ikiwemo Ilembo hatua ambayo huwalazimu kutembeza zaidi ya kilometa 10 kuzifikia shule hiyo hivyo kwa siku wanalazimika kutembea zaidi ya kilometa 20 kwaajili ya kwenda na kurudi.

“Watoto wanawakati mgumu sana katika kata hii.Wanalazimika kutembea zaidi ya kilometa 20 kwa siku.Hii inawalazimu kutumia muda mwingi kutembea na muda mchache mno darasanai.” Anasema Njeza.

Anasema hali ni mbaya zaidi katika kipindi cha mvua nyingi kwakuwa wanafunzi hufika shuleni wakiwa wamenyeshewa na mvua na na vivyo hivyo wakati wa kurudi makwao na hivyo kushindwa kushiriki vipindi darasani ipasavyo.

Wakazi wa kata hii wanasema wamechoshwa na watotoa wao kwenda kusoma mbali na kata yao.Wamechoshwa na athari ambazo zimekuwa zikiwakumba watoto hao na familia zao kwa ujumla.Familia zilizo na watoto wa kike ndizo huathiriwa zaidi.

Fidelia Mwasenga ni mmoja wa wakazi wa kijiji cha Masoko kilichopo kwenye kata hiyo,Anasema Kukosekana kwa sekondari kwenye kata yao kunasababisha uduni wa elimu.Ndoto zao ilikuwa kuanza kunufaika mapema na sekondari wanayoijenga.Sasa siku zinazidi kupita pasipo matunda tarajiwa kuonekana.

“Sasa shule hii mimi inanikera kwakuwa najiuliza ni kwa nini inachelewa kufunguliwa?Na hii tunaumia kutokana na Mazingira ambayo watoto wanasoma.Ni mabaya sana,watoto wanapata mimba humo njiani,Wengine hawaendi shule inavyostahili kwakuwa wanarubuniwa njiani.”

“Tumelia kwa muda mrefu.Imefikia wakati mpaka wazazi wanakata tama ya kupeleka watoto wao shule kwakuwa kila wanapojaribu kuwapeleka hawafikii malengo ya familia kwakuwa wanaishia njiani.Tunaomba serikali itusikilize ifungue shule yetu” anaomba Fidelia.

Mkazi mwingine Donati Mwalinda anasema walioathirika si watoto peke yao,wazazi pia wameathirika sana kwakuwa hawaoni matunda ya michango wanayochangia katika elimu.

“Kwa mfano kipindi hiki cha mvua,mtoto analowa njia nzima mpaka anafika shuleni.Akifika darasani amelowa hata mahesabu hawezi kufanya kwakuwa akili haifanyi kazi.Atalazimika kulowa tena wakati wa kurudi nyumbani mpaka anafika.Taayari kwa familia ni tatizo kwani kwa kunyeshewa na mvua tayari anaweza kupata magonjwa na kuilazimu familia kugharamia matibabu.”

“Tulijenga madarasa manne kwa wakati mmoja mwaka huo huo 2013.Kazi nyingi tumefanya mapaka majengo ya shule hii kufikia hapa unapoyaona.Kusomba tofali,kuchimba na kusomba mchanga kwa kichwa kutoka mtoni zote tumefanya.Tukaambiwa tujenge kwanza jengo la utawala.Lakini matokeo yake tumejenga mpaka jengo la utawala hawataki kufungua shule yetu” anasema mkazi mwingine Obeid Mwashibanda.


Kaimu Ofisa Elimu Sekondari wialayani hapa Abihudi Fungamtama,anasema kilichocheleweshwa kufunguliwa kwa shule hiyo ni kutokamilika kwa vigezo vinavyotakiwa.

“Mwenye mamlaka ya kusajiri shule ni Kamishna wa Elimu na Upo waraka maalumu uliotolewa unaoeleza kuwa ili shule ifunguliwe lazima ikidhi vigezo ambavyo tumekuwa tukiwaelekeza wakazi wa kata hii kuvitimiza”anasema Fungamtama.

“Moja unatakiwa kuwa na vyumba vya madarasa angalau vya kutosha wanafunzi wa miaka miwili kwa maana ya kidato cha kwanza na cha pili kwa mikondo miwilimiwili hivyo kunatakiwa kuwepo na madarasa angalau manne.Lakini pia Miundombinu kwa maana ya Nyumba za walimu,maji na eneo ambalo kwa kijijini ni hekta tatu.”

“Kwa shule hii kwa upande wa eneo inalo la kutosha.Tatizo kubwa ni kwamba hakuna nyumba za walimu na pia maji hayaklo jirani na shule.Pia hakuna samani kwa maana ya meza na viti.Jengo la utawala halijakamilika na pia hakuna vyoo”

Afisa huyu anasema kutokamilika kwa vigezo hivyo kwa kipindi cha nyuma kulitokana na kutojitoa kwa wananchi katika michango  mbalimbali ya ujenzi kama ilivyohitajika.Uongozi wa kata hiyo ulihamasisha wananchi kutochangia ujenzi huo ukisema serikali ina jukumu la kutekeleza jambo hilo tofauti na uongozi uliopo hivi sasa ambao umeonesha nia ya kuhamasisha wananchi kushiriki kwenye mikakati ya kujiletea maendeleo.

“Kwa kasi ninayoiona hivi sasa nina amini mwakani shule hii inaweza ikafunguliwa.Na sisi kama halmashauri kama ilivyokuwa huko nyuma tutaendelea kushiriki kwa karibu kushauri ili ikamilike kwa wakati ili angalau mwaka kesho shule iweze kupata usajiri” anasema afisa huyo.

Lakini tama ya mbunge wa jimbo hili ni kuona shule hii inafunguliwa haraka na watoto kuanza masomo shuleni hapo.Nia ni kuwaondolea adha wanafunzi huku pia akisema atahakikisha ujenzi wa Hosteli shuleni hapo unafanyika kwa haraka ili wanafunzi wa kike waishi jirani na shule yao kuepuka vishawishi vya wanaume wa mitaani.

“Nilianza kuja shuleni hapa hata kabla sijawa mbunge.Nikiwa Kamanda wa vijana wa Chama Cha Mapinduzi(UVCCM) nilifika mara kadhaa hapa hivyo natambua haja ya wakazi wa kata hii juu ya sekondari.Nitahakikisha ninafanya kila linalowezekana kukamilisha jambo hili kwa wakati”anasisitiza Njeza.

Nia ya mbunge huyu imejidhihirisha hivi karibuni pale alipoandaa harambee ya kuchangia sekondari hii ya Masoko ili kukamilisha ujenzi wake.Katika harambe hiyo iliyofanyika kwenye eneo la shule husika Njeza alifanikiwa kukusanya zaidi ya shilingi milioni 30.

Miongoni mwa fedha zilizokusanywa katikaa harambee hiyo ni pamoja na shilingi milioni 16 zilizotolewa na mbunge Njeza huku halmashauri ya wilaya ikiahidi kuchangia shilingi milioni 6.2.

Kwa mujibu wa Diwani wa kata ya Masoko Tumaini Mzumbwe kiasi cha shilingi milioni 71 kinahitajika ili kukamilisha ujenzi wa sekondari hiyo.

Akizungumzia harambee hiyo,mbunge Njeza aliyeambatana na wafanyabiashara rafiki zake kutoka mji mdogo wa Mbalizi wilayani hapa ambao pia kila mmoja wao alichangia kwa kadiri alivyoweza,alisema huo ni mwanzo na iwapo kuna jambo lolote atahitajika kuchangia hatosita.

“Lakini haya yote yatawezekana iwapo tutashirikiana kila mmoja kwa namna anavyoweza.Tumekwishawambia wananchi kuwa tusitarajie maendeleo kwa kutegemea nguvu ya jirani.Ni lazima tushiriki kujiletea maendeleo na ndiyo sababu hata bajeti ijato ya serikali kuu inalenga kujitegemea zaidi badala ya kubaki ombaomba”anasema Njeza.

Mwenyekiti wa halmashauri ya Mbeya Mwalingo Kisemba anasema ni kata mbili pekee zimebakia kwenye halmashauri yake hazika shule za sekondari.Ipo kata ya Masoko ambayo ujenzi wa sekondari ya Sasyaka unaendelea na kata ya Inyala ambako ujenzi wa sekondari ya Iyelanyala unaendelea pia.

“Kwa kutimiza ujenzi wa sekondari katika kata nyingine zote tunaamini tumepunguza deni kwa kiasi kikubwa hivyo kutokana na ushiriki wa wananchi kwa sasa tutakamilisha na hizi mbili kwa kipindi kifupi kijacho.Uwepo wetu tu hapa leo unaonesha nia yetu katika kutekeleza jambo hili mapema” alisema Kisemba aliyehudhuria pia harambee hiyo.

Mwandishi wa Makala haya anapatikana kwa namba 0756 40 95 97 Email nyambojoachim@gmail.com

No comments:

Post a Comment