Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Tuesday, March 1, 2016

YAJUE MAGONJWA YASIYOPEWA KIPAUMBELE TANZANIA



Na Joachim Nyambo.

MAGONJWA ya Matende na Mabusha(Ngirimaji),Minyoo ya Tumbo,Kichocho,Trakoma na Usubi ni miongoni mwa magonjwa yanayoiathiri jamii na kuidhoofisha.Inakadiriwa kuwa watu bilioni moja duniani kote tayari wameathiriwa.Zaidi ya watu bilioni mbili wako hatarini kupata magonjwa hayo.

Nchini Tanzania tafiti mbalimbali zinaonesha kuwa maambukizi ya magonjwa haya hupatikana karibu maeneo mengi.Licha ya uwepo wake ndani ya jamii yalikuwa hayapewi kipaumbele kwenye mikakati ya kupambana na maradhi.Jamii masikini zinatajwa kuathirika zaidi na magonjwa haya.

Afisa Mradi wa Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbelea kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto,Dk.Edward Kirumbi anasema magonjwa mengine yaliyopo kwenye kundi hili ni pamoja na Kichaa cha mbwa,Homa ya Papasi,Malale na Tauni.

Dk.Kirumbi anasema magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele yapo kwenye jamii zetu.Kwa muda mrefu yalikuwa hayapewi umuhimu stahili  na wadau wa huduma za afya kama ilivyo kwa magonjwa mengine kama ilivyo kwa Malaria,Ukimwi na mengineyo.Hayakupewa umuhimu kutokana na athari zake katika jamii.

“Kila mtu yuko katika hatari ya kupata maambukizi ya magonjwa haya endapo hatazingatia ushauri wa kitaalamu” anasema Dk Kirumbi.

Nini uambukizi wa magonjwa haya.

Dk Kirumbi anasema Usubi husababishwa na minyoo iitwayo Onchocerca Volvulus.Minyoo hii huenezwa nzi wadogo weusi wanaokaa kandokando ya mito iendayo kasi.Ugonjwa huu husababisha ngozi kuwasha au ngozi kuwa na mabaka mabaka mithili ya mamba au mjusi.

Matende na Mabusha(Ngirimaji) husababishwa na minyoo aina ya Wucheria Bancrofti inayosababishwa na Mbu.Anasema minyoo hii huishi kwenye mfumo wa maji ya damu.Ni ugonjwa unaosababisha kuvimba kwa miguu,mikono na sehemu za siri.

Kichocho Husababishwa na minyoo aina ya Shistosoma.Konokono anaeneza ugonjwa huu kwa kutoa vimelea kwenye maji yaliyotuwama na binadamu huambukizwa kwa kugusa maji hayo..Kichocho husababisha damu kutoka kwenye mkojo na choo.Pasipo tiba ya haraka baadaye kichocho kinaweza kusababisha Saratani ya tumbo,kibofu cha mkojo na ini.

Minyoo ya tumbo ni minyoo iliyopo katika aina tatu.Minyoo mviringo,Minyoo mjeledi na Minyoo Safura.Minyoo hii huishi ndani ya tumbo.Isipotibiwa mapema husababisha mwili kuwa dhaifu,upungufu wa damu,utumbo kujifunga na hata kifaa.Pia inaweza kumfanya mtoto kushindwa kuhudhuria shule au kuelewa vizuri masomo.

Trakoma Husababishwa na bacteria aina ya Chlamydia Trachomatis wanaosambazwa na nzi na pia kwa njia ya kugusana baina ya mtu na mtu aiwapo mmoja wao ana maambukizi.Trakoma isipotibiwa mapema husababisha upofu.

Malae husababishwa na vimelea aina ya Protozoa anayeitwa Trypanasoma.Huenezwa na Mbung’o.Ugonjwa huu husababisha udhoofu wa viungo vya mwili,kuuma mwili,kichwa kuuma,kuvimba tezi za shingo,kuchanganyikiwa,kulala mara kwa mara, hasa mchana na kukosa usingizi usiku.

Tauni ni ugonjwa unaosababishwa na bacteria aitwaye Yersinia Pestis.Bakteria hawa husambazwa na viroboto vya panya.Dalili za ugonjwa huu ni homa kali,maumivu ya mitoki(tezi) na mwili kuchoka.

Kichaa cha Mbwa,Ugonjwa huu husababishwa na virusi.Binadamu anaambukizwa baada ya kung’atwa na Mbwa au wanyama wengine wa jamii hiyo kama Mbweha na paka walio na ugonjwa huo.Pia binadamu anaweza pia kuambukizwa kwa kugusa mate ya mnyama mwenye ugonjwa huu.Dalili za Kichaa cha Mbwa ni homa,kichwa kuuma,mwili kuchoka,kushtuka,kuchanganyikiwa,kupoteza fahamu,kuogopa maji,upepo na wakati mwingine kushindwa kutembea.

Homa ya Papasi Husababishwa na bacteria aina ya Borrelia.Bakteria hawa huenezwa na Papasi.Dalili za ugonjwa huu ni homa kali,kichwa kuuma,mwili kuchoka na pia kutapika.

“Njia za kujikinga na magonjwa haya ni pamoja na Kutumia dawa za kutibu na kudhibiti magonjwa haya ambazo hutolewa kila mwaka katika jamii iliyoathirika.Kuzingatia usafi wa uso na mwili kwa ujumla ni jambo muhimu” anasema Dk Kirumbi

“Jamii inapaswa kuzingatia usafi wa mazingira kwa ujumla na pia kutokuoga,kutokuogelea wala kutotembea kwenye maji yasiyo safi na yaliyotuama kama vile mabwawa na mifereji.Tunapaswa kujikinga na kuumwa na nzi,Mbung’o,mbu na wadudu wengine wasambazao magonjwa haya.Matunda na Mbogamboga zioshwe vizuri na maji safi na salama kabla ya kuliwa.Lakini pale tunapokuwa tumepata maambukizi tayari ni muhimu kutibiwa haraka.”

Anasema utoaji wa chanjo kwa wanyama kama mbwa ni muhimu sana.Hii ni kwa manufaa ya jamii yote kwakuwa mbwa aliyechanjwa si rahisi kuwa na virusi vya ugonjwa wa kichaa vinavyoweza kumpata mtu yeyote iwapo mnyama huyo atamng’ata.

Nini mikakati ya Udhibiti na kutokomeza magonjwa haya.

Afisa mradi huyo anasema magonjwa ya Usubi,Matende na Mabusha(Ngirimaji),Trakoma Vikope,Kichocho na Minyoo ya tumbo hudhibitiwa moja kwa moja na Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbelea kwa njia ya kugawa dawa za kuzuia na kukinga maambukizi ya magonjwa haya.Dwa hutolewa kila mwaka mara moja kwa jamii katika mikoa na wilaya zilizoathirika.

“Magonjwa mengine yakiwemo,Malale,Kichaa cha Mbwa,Tauni,Homa ya Dengu,Homa ya Papasi,Kifua kikuu na Ukoma hushughulikiwa na mpango huu kwa kushirikiana na wadau mbalimbali” anasema.

Praziquantel ni dawa inayotibu na kukinga Kichocho cha Tumbo na Kichocho cha Kibofu cha mkojo,Zithromax ya vidonge na maji inatibu na kukinga Trakoma.Albendazole na Mectizan zinatibu na kukinga Matende,Usubi na Minyoo ya tumbo.

Manufaa ya dawa hizi zikitumika kwa usahihi ni pamoja na Kupunguzamaambukizi kutoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mwingine,kuua vimelea vya magonjwa haya,kukinga upungufu wa damu,kukinga,kupunguza maumivu na athari zinazosababishwa na magonjwa haya,kuboresha nguvu kazi katika jamii,kuwezesha watoto kukua vizuri kimwili na kiakili na pia kuongeza mahudhurio ya watoto shuleni na uweza wa kuelewa masomo.

Kila mwananchi anayestahili anatakiwa kumeza dawa za kutibu na kuzuia magonjwa haya mara moja kila mwaka.Itawezesha vimelea vilivyo ndani ya mwili kufa na maambukizi hayataendelea.Kutokana na ukweli huu kila mwananchi anapaswa kujitokeza kupata dawa za kutibu magonjwa haya katika siku maalumu zinazopangwa na kutangazwa katika jamii.

Hivi karibuni katika warsha ya Uraghibishi na Uhamasishaji juu ya magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele iliyofanyika mkoani Mbeya,Mkuu wa mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro alisema haya  ni magonjwa ambayo yanaathiri jamii  ya watu hususan jamii yenye kipato cha chini, wananchi wake wanaishi katika maeneo duni, maeneo ambayo  hata upatikanaji wa  huduma za afya ni  mgumu.Kiwango cha maambukizi ya magonjwa haya katika jamii ni kati ya asilimia 1 hadi asilimia 87.6 kitaifa.

“Pamoja na athari nyingine,Magonjwa haya pia husababisha usumbufu mkubwa kwa waathirika wake na  yanaongeza matumizi ya rasilimali chache tulizonazo katika kuyakabili kwa gharama kubwa mno. Pamoja na athari zote hizo, waathirika wa magonjwa haya  wakabiliwa na unyapaa katika jamii.”

“Ombi langu kwenu Wakurugenzi wa Halmashauri, ni kwamba muhakikishe Mpango huu unaingizwa katika Mpango Kabambe wa Halmashauri na kutengewa fedha za kutosha, ili tusiwe tegemezi kwa wahisani tu.”

“Lakini, vilevile Wakurugenzi na maafisa wote mnaohusika na mchakato wa kuzitoa fedha hizi wilayani mpunguze ukiritimba ili fedha itoke kwa wakati na kuwezesha shuguli kufanyika kwa wakati uliopangwa.”

“Rai yangu kwa Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri na viongozi wa ngazi zote  ni kwamba msimamie kikamilifu zoezi la umezeshaji dawa kwa kinga –tiba ya magonjwa haya, ili Mkoa wetu mwaka huu na miaka ijayo uweze kupata “coverage” nzuri ya umezaji dawa.”

“Pia ni muhimu kwa wananchi wote kumeza dawa hizi za Kinga-tiba kama wanavyoelekezwa na wataalam wakati wa Kampeni husika. Dawa hizi zimethibitishwa na Shirika la Afya Duniani pamoja na Mamlaka ya Chakula na Dawa nchini kuwa ni salama na hazina Madhara yeyote.”alisisitiza Kandoro.

Muandaaji wa Makala haya anapatikana kwa namba 0756 40 95 97, Email nyambojoachim@gmail.com

No comments:

Post a Comment