Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Monday, May 9, 2016

ZAHANATI YAFUNGWA MIEZI MITATU KWA MUUGUZI KWENDA LIKIZO YA UZAZI

UHABA wa wataalamu wa Afya wilayani Mbozi mkoani Songwe umesababisha wakazi wa kijiji cha Itepula kata ya Igamba wilayani hapa kukosa huduma za matibabu kwa miezi mitatu sasa kufuatia Muuguzi katika Zahanati ya kijiji chao kwenda likizo ya Uzazi.

Wakazi wa kijiji cha Itepula walibainisha hayo kwenye mkutano wa Hadhara uliofanyika kijijini hapo ukiwakutanisha na madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Mbozi walioongozwa na mwenyekiti wao Eliki Ambakisye.

Mmoja wa wakazi hao Sikudhani Mkondya alisema suala la kufungwa kwa Zahanati kutokana na kukosekana muuguzi limekuwa kero kwao kwasababu miezi mitatu imepita sasa na wanalazimika kutembea umbali mrefu kufuata huduma za matibabu katika vijiji vingine.

Mkondya pia alisema kufuatia kukosekana kwa mtaalamu kijijini hapo baadhi ya wakazi wanalazimika kutumia dawa pasipo ushauri wa kitabibu hivyo kubaki wakimeza dawa kwa kukisia hata kama hawajui ugonjwa unaowasumbua.

Alisema hali imekuwa mbaya zaidi kwakuwa hata wanapokwenda katika zahanati iliyopo kijiji cha jirani cha Igamba wanafukuzwa na wataalamu wa zahanati hiyo wakiwataka warudi kutpata matibabu katika zahanati ya kijiji chao

“Inatulazimu kwenda kununua dawa katika maduka yaliyopo pasipo kujua tunaumwa nini kwani hakuna vipimo.Tunaamini tunahatarisha maisha yetu kwa kutumia dawa pasipo kujua magonjwa yanayotusumbua ,lakini tutafanya nini nasi hatuna njia mbadala.”alisema Mkondya.

Afisa mtendaji wa kijiji cha Itepula, Timothy Msukwa alikiri zahanati ya kijiji hicho kufungwa tangu January mwaka huu hivyo wananchi kuhangaika kupata matibabu kwani walizoea kupata huduma jirani.

Msukwa alisema chanzo cha kufungwa kwa zahanati hiyo ni baada ya muuguzi aliyekuwa anatoa huduma katika zahanati hiyo kwenda likizo lakini akabainisha kuwa tayari wamempata muuguzi mwingine ambaye tayari ameripoti lakini hajaanza kufanya kazi.

Kwaupande wake mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Mbozi Elick Ambakisye aliagiza zahanati kufunguliwa mara moja huku akimtaka muuguzi aliyepangiwa kituo hicho kufika mara moja na kuanza kazi ili kutoa hudumia wananchi.

Mwenyekiti huyo alisema ipo haja kwa serikali kutafuta uwezekano wa kuongeza wataalamu ili kuendana na dhana ya wanyonge kupata matibabu  jirani kwakuwa walijitoa kujenga zahanati hiyo kwa lengo la kujinasua na adha ya kusafiri umbali mrefu kufuata matibabu.

No comments:

Post a Comment