WANAFUNZI 1,302 hawajaanza masomo ya kidato cha kwanza wilayani hapa kufuatia uhaba wa vyumba vya madarasa unaozikabili shule za kata walizopangiwa.
Hali hiyo inatokana na wananchi katika kata hizo kugoma kuchangia ujenzi wa vyumba hivyo huku sababu ikitajwa kuwa ni baadhi ya viongozi wa vijiji na kata kutafuna michango wanayokusanya huku vyumba vinavyohitajika kwa sasa vikiwa ni 32.
Hali hiyo imewekwa bayana na mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Mbarali Keneth Ndingo katika kikao cha baraza la madiwani kilichofanyika katika ukumbi wa maji uliopo mjini Rujewa.
Ndingo alisema kuwa upungufu huo wa madarasa ni changamoto kubwa kwa wilaya na kutoa wito kwa kila kiongozi kuhakikisha anawajibika kutokana na nafasi yake kuhimiza ujenzi wa vyumba hivyo ili watoto waanze masomo.
Alisema hakuna budi kuweka mikakati madhubuti ili wanafunzi waliobaki waweze kuanza masomo na kwamba moja ya mkakati mkubwa ni kuhamasisha uchangiaji kwa wananchi licha kukatishwa tamaa na viongozi wa vijiji na kata.
Alikiri wananchi wamekuwa wagumu kuchangia kutokana na kukata tama hali inayotokana na baadhi ya viongozi wa vijiji na kata kufuja michango inayotolewa na wananchi ili iweze kusaidia shughuli za maendeleo katika maeneo yao.
Hata hivyo mwenyekiti huyo hakuweka bayana ni maafisa watendaji na viongozi wa vijiji wangapi waliobainika kutafuna fedha za wananchi na pia ni hatua zipi za kishweria zilizochukuliwa dhidi yao wala kiasi cha fedha kilichobainika kutafunwa.
No comments:
Post a Comment