Tuesday, January 22, 2013
MUME AJINYONGA BAADA YA KUMNYONGA MKE
WATU wane wamefariki dunia mkoani Mbeya katika matukio matatu tofauti
likiwemo la mume kujinyonga kwa kamba ya manira muda mfupi baada ya
kumnyonga shingo hadi kumuua mkewe kutokana na wivu wa mapenzi.
Kamanda wa polisi mkoani Mbeya Diwan Athuman aliwataja marehemu katika
tukio hilo kuwa ni Richard Mwakalukwa(23) na mkewe Agnes Kalinga(18)
wote wakazi katika kitongoji cha Mkeje kijiji cha Mwalisi kata ya
Ngana wilayani Kyela.
Kamanda Athuman alisema tukio hilo lilitokea Januari 21 mwaka huu
majira ya saa 9:00 alasiri ambapo wakiwa chumbani kwao mume
alimnyonga shingo mkewe mpaka kuivunja na baada ya kuona amemuua
akachukua kamba ya manira na kujinyonga katika mti wa mkorosho nje ya
nyumba yao.
Alitaja chanzo cha mauaji hayo kuwa ni wivu wa mapenzi kwani mume
Mwakalukwa kwa muda mrefu alikuwa akimtuhumu mkewe kutokuwa mwaminifu
katika ndoa yao kutokana na kuwa na mahusiano ya kimapenzi na wanaume
wengine.
Katika tukio jingine lililotokea Januari 21 majira ya saa 12:30 jioni
katika kijiji cha Hanseketwa wilayani Mbozi barabara ya Mbeya/Tunduma
Gari lenye namba T 451 BRK Toyota Coasta lililokuwa likiendeshwa na
Willy Songelamaarufu kama Muasisi(46) liligonga pikipiki yenye namba T
201 CCT aina ya T-Better na kusababisha kifo cha dereva wa pikipiki
hiyo Tito Nyondo(20) mkazi wa Tunduma.
Ajali hiyo pia alimsaababishia majeraha mwanafunzi wa shule ya
sekondari Msika Baraka Nyondo(19) ambaye amelazwa katika hospitali ya
wilaya ya Mbozi iliyopo katika mji mdogo wa Vwawa.
Kamanda Athumani alisema tukio la tatu ni la kifo cha mwanafunzi wa
darasa la kwanza katika shule ya Mwanyanje Halaika Bushiri(7)
kilichosababishwa na ajali ya moto iliyotokea nyumbani kwao Uyole
jijini Mbeya.
Alisema tukio hilo lilitokea januari 21 majira ya 7:45 za mchana
wakati mtoto huyo alikuwa amelala kwenye kochi lililokuwa kwenye
korido ulipoanzia moto lakini baadaye ukazimwa.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment