Tuesday, January 15, 2013
WAWILI WAZIKWA HAI
WATU wawili wakazi wa kijiji cha Ivuna wilayani Momba wamezikwa wakiwa
hai baada ya wakazi wenzao kuwatuhumu kuwa ni wachawili.
Kamanda wa polisi mkoani Mbeya Diwani Athumani alisema jana kuwa tukio
hilo lilitokea siku ya jumapili iliyopita ambapo aliwataja waliozikwa
kuwa ni Mizinara Matela na Ernest Molela wote wakazi kijijini hapo.
Kamanda Athumani alisema wakazi hao walikuwa wakituhumiwa na
wanakijiji wenzao kuwa walihusika na kifo cha ndugu yao aliyemtaja
kwa jina la Nongwa Molela aliyekufa baada ya kuugua kwa muda mrefu.
Alisema baada ya maziko ya Nongwa ndipo wakazi wa kijiji wakiwemo
ndugu wa marehemu walianza kuwanyooshea vidole watu hao wawili
wakisema ndiyo waliomuu na kuchukua uamuzi wa kuanza kuwapiga.
Alifafanua kuwa kabla ya kuwazika wakiwa hai kundi la wanandugu hao
waliwapiga wawili hao kwa marungu na mawe na kabla ya kuwaua
wakawatupia kwenye kaburi moja na kuwafukia humo.
Baada ya kuwazika wakiwa hai,kundi la wanandugu hao lilikwenda
nyumbani kwa Ernest na kuiteketeza nyumba yake kwa moto.
Mpaka anazungumza na mwandishi wa habari hizi shughuli ya kufukua
miili ya watu hao ilikuwa ikiendelea kwa lengo la kufanyiwa uchunguzi
ambapo alifafanua kuwa baada ya uchunguzi huo kila mwili utazikwa
kwenye kaburi lake.
Aidha kamanda huyo alisema mpaka sasa watu wawili wanashikiliwa ambapo
inasadikiwa kuwa ndiyo waliongoza kundi lililotenda ukatili huo lakini
hakuwataja kutokana na sababu alizosema ni za kiusalama.
Hii si mara ya Kwanza kwa matukio ya watu kuzikwa wakiwa hai kwa
tuhuma za uchawi mkoani Mbeya kwani mwaka jana pia matukio hayo
yalikuwa yakielewa kufanyika kwa usiri mkubwa lakini ilikuja kubainika
siku ambayo Chifu Merere wa kabila la Wasangu aliponusurika kuzikwa
akiwa hai na wakazi wa kijiji cha Ruiwa wilayani Mbarali.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment