Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Thursday, November 6, 2014

KFW YAWAFUMBUA WANAUME MBEYA,SASA WAHAMASIKA KUWASINDIKIZA WAKE ZAO WAJAWAZITO KLINIKI



 Meneja wa NHIF mkoani Mbeya Dk.Mohamed Kilolile akiwasilisha moja ya mada kwa watoa huduma wa KFW wakati wa semina iliyofanyika katika ukumbi wa Mtenda jijini Mbeya










MRADI wa Afya ya Mama na Mtoto(KFW) unaoendeshwa na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya(NHIF) kwa ufadhili wa benki ya maendeleo ya watu wa Ujerumani umewezesha wanaume kushiriki shughuli za uzazi kwa kuwasindikiza wake zao kliniki wanapokuwa wajawazito.

Hayo yamebainishwa na watoa huduma wa KFW walipohudhuria semina ya siku mbili ya mafunzo ya kuwajengea uwezo iliyofanyika jijini Mbeya.

Watoa huduma hao wanasema tofauti na awali hivi sasa kumekuwa na mwamko mkubwa wa wanaume kuongozana na wake zao kwenda kliniki  wanapokuwa wajawazito na kupata elimu kwa pamoja juu ya njia sahihi zinazotakiwa katika kumhudumia mama mjamzito.

“Kwa sasa wanaume wanashiriki kwa kiasi kikubwa ikilinganishwa na awali.Wanapenda kuongozana na wake zao ili wapate elimu kwa pamoja.Tunaamini kupitia elimu tunayoitoa upitia KFW wamebadilika na wametambua kuwa wanawajibu pia wa kuhudhuria kliniki ili kupata tarifa sahihi za ujauzito wa wake zao” anasema mmoja wa watoa huduma hao Elizabeth Mwamlima kutoka zahanati ya kijiji cha Utulo wilayani Mbarali

Mwamlima amesema kwa ushiriki huo wa wanaume hivi sasa familia zimekuwa zikijipanga mapema wakati wa ujauzito ili kuhakikisha mwanamke husika anapata huduma stahiki ikiwemo kupelekwa katika hospitali waliyoshauriwa na wataalamu mara wakati wa kujifungua unapowadia.

Amesema hali hiyo inawaepusha wanawake wajawazito kuepuka hatari ambazo zilikuwa zikiwakumba awali na kuhatarisha maisha yao na watoto wachanga wakati wa kujifungua na baada.

Kwa upande wake katibu wa Afya mkoa wa Mbeya Juliana Mawala amesema mradi wa KFW ambao kwa hapa nchini unaendeshwa katika mikoa miwili ya Mbeya na Tanga umeleta manufaa makubwa katika utatuzi wa changamoto za Afya za wajawazito na watoto wachanga.

Mawala amesema ni imani ya wadau wa afya kuwa ushiriki wa jamii katika utatuzi wa changamoto zinazowakabili wajawazito na watoto utakuwa endelevu hata baada ya ukomo wa KFW kwakuwa tayari wananchi wamepata uelewa juu ya umuhimu wa kuchangia na kuwekeza katika masuala ya afya.

No comments:

Post a Comment