Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Monday, November 10, 2014

WANAFUNZI 48 WATAPELIWA MILIONI 26 NA CHUO FEKI,KIKO JIJINI MBEYA.WAACHWA NJIA PANDA HAWANA CHAKULA WANA NAULI KURUDI MAKWAO

UONGOZI wa chuo cha kilimo cha Nice Dream kilichopo katika mtaa wa Mapelele kata ya Ilemi Jijini Mbeya umetokomea kusikojulikana na kuwaacha wanafunzi 48 wakiwa hawajui la kufanya wakiwa wametozwa jumla ya shilingi milioni 26 walizotoa kwaajili ya ada ya masomo chuoni hapo.

Kutokana na kukimbiwa na uongozi wa chuo na wanafunzi kubaki peke yao chuoni hapo,wanafunzi wamejikuta katika wakati mgumu kwani sasa licha ya kutojua nini hatma ya maisha yao sula la kukosekana kwa chakula ni changamoto nyingine inayowaweka kwenye mazingira magumu zaidi.

 Wakati Lyamba Lya Mfipa ikifika chuoni hapo jana,wapo baadhi ya wanafunzi walioonekana kuzirai na kupoteza fahamu kwa zaidi ya saa mbili kwa kukosa chakula kabla ya kuokolewa na wakazi wa maeneo ya jirani na Chuo walioamua kuchangia fedha na kuanza kuwapikia wanafunzi hao.

Baadhi ya wananchi pia walionekana chuoni hapo wakiangua vilio kwa kuwahurumia wanafunzi na wazazi wao kwa hasara kubwa waliyoipata baada ya kutapeliwa na uongozi wa chuo hicho ulioanza kupokea wanafunzi na kuwatoza ada ingali ukijua chuo hakijasajiriwa.

Joanes Renatus, mwanafunzi kutoka mkoa wa Kagera amesema alipokea barua na fomu ya kutaarifiwa kujiunga na Chuo hicho baada ya matokea ya kidato cha nne mwaka jana ikiambatanishwa na gharama za michango yenye jumla ya shilingi 860,000.


Joanes amesema barua hiyo ilikuwa ikisisitiza mwanafunzi anaporipoti kufika na karo ya mhula wa kwanza ambayo ni shilingi 550,000 jambo ambalo lilitekelezwa na wazazi na kufanikiwa kufika Chuoni Septemba mwaka huu.


Amesema kuwa jambo la kushangaza ni kuona tangu afike chuoni hapo hali aliyoikuta imekuwa tofauti na matarajio yake ambapo baada ya yeye na wanafunzi wenzie kutafuta usajili wa chuo kutokana na muonekano wa majengo na upungufu wa Walimu waligundua kuwa chuo hicho hakina usajili kutoka Nacte.


Wanafunzi wengine Annaf Habibu (Kagera), Mtani Ndelekule(Mara) na Joviness Selestine kutoka Karagwe wamefafanua zaidi wakisema baada ya kuripoti chuoni hapo hawakukuta wananfunzi wengine jambo walilouliza na kujibiwa kuwa wako kwenye mafunzo ya vitendo lakini kadri muda ulivyozidi ikabainika kuwa wao walikuwa wanafunzi wa kwanza.

Wanafunzi hao 48 ambao asilimia kubwa wanatoka mikoa ya kanda ya Ziwa wamesema hadi sasa hawajui hatima ya maisha yao kutokana na baadhi yao wazazi kuuza mifugo na mashamba ili kuwagharamia nauli na ada na ndipo wakaweza kufika chuoni hapo.

Wamesema hivi sasa maisha yao yako hatarini kutokana na kutokuwa na chakula jambo linalowalazimu majirani na baadhi ya wazazi kuwachangia kitu chochote ili mradi wapate mlo wa siku.


Wameiomba Serikali kuingilia kati sakata hilo na ikiwezekana iwatafutie chuo kingine ili waweze kuendelea na masomo ili waweze kutimiza adhma yao na kuwaridhisha wazazi kwa kuwa wakirudishwa makwao wengi wao hawatapokelewa wala kuaminiwa tena.


Kwa upande wake diwani wa Kata ya Ilemi(Chadema) Furaha Mwandalima baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa wanachuo hao na kufika Chuoni hapo na kujionea hali halisi alionesha kushangazwa kuona kuna chuo mahali hapo akisema hakuwahi kukisikia katika maisha yake.


Mwandalima alisema taarifa za kuwepo kwa Chuo hicho alizipata baada ya kupata malalamiko kutoka kwa Ubalozi na wanafunzi wenyewe hivyo aliamua kuchukua hatua za haraka za kumtafuta Mstahiki Meya ambaye alimshauri kutoa taarifa kwa Mkuu wa Wilaya ya Mbeya ili kupata mustakabali wa suala hilo.


Diwani huyo alisema muafaka uliofikiwa ni kutolewa kwa agizo la kuorodheshwa kwa majina ya wanafunzi na mahali wanakotoka ili kuwarudisha makwao na Chuo kifungwe kutokana na Chuo hicho kutosajiliwa rasmi na kwamba kilikuwa kinaendeshwa kijanja na wanachuo hao wamelipa malipo ya awali zaidi ya shilingi laki tano na kufikia zaidi ya shilingi Milioni 26 zilizotapeliwa na uongozi wa Chuo.


Balozi wa mtaa wa Mapelele jijini hapa Geophrey Mwalupindi na mkazi mwenzake Fanuel Kisanga walipoulizwa kama wamewahi kusikia kuwepo kwa Chuo hicho walionesha kushangaa na kudai kuwa awali kilikuwa ni kituo cha kufundishia masomo ya ziada(Tution) na masomo ya awali(chekechea) lakini kuhusu Chuo wamesikia baada ya kutokea utapeli.


Kati ya wanafunzi waliotapeliwa,43 wanatokea Mkoa wa Kagera,wawili mkoani Mara,wawili wilayani Kyela mkoani Mbeya na mmoja akitokea Dar es Salaam.


Juhudi za kuupata uongozi wa Chuo hicho haukufanikiwa kupitia namba za simu za Mkononi walizoandika kwenye bango la chuo ambazao ni 0765659079 na 0684423849 kwani hazikupatikana hewani.


Uchunguzi pia uliofanywa na  mwandishi wetu umebaini kuwa malipo ya karo chuoni hapo yalikuwa yakipokelewa kwa ujanjaujanja na mtu aliyefahamika kama Samwel Daud ambaye ni mmiliki wa chuo hicho na njia anazotumia kukusanyia ada kutoka kwa wanafunzi ambao hupeleka kwa katibu mukhtasi wake na kutoa stakabadhi isiyokuwa na namba za usajili wa chuo wala namba za TRA( tin number).

Njia nyingine ambayo wanafunzi waliambiwa walipie ada zao ni kupitia njia ya Mpesa ambapo mzazi alilazimika kutuma kwa wakala mwenye namba 98369 tofauti na kupokelewa kwa njia ya Benki au simu ya uongozi.

Kama vile haitoshi,mmiliki wa Chuo hicho alitumia mbinu zaidi ili kuwaaminisha wanafunzi na wazazi kuwa Chuo hicho kimesajiliwa baada ya kuchora kibao kikionesha Chuo hicho kilifunguliwa rasmi na waziri kuu wa Mstaafu, Frederick Sumaye.

No comments:

Post a Comment