Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Tuesday, May 16, 2017

JELA MIAKA 30 KWA KUJARIBU KUMBAKA KIKONGWE

MAHAKAMA ya wilaya ya Nkasi mkoani Rukwa imemuhukumu kutumikia kifungo cha miaka 30 jela, Jovin Bukambo (30) mkazi wa kitongoji cha Nkomolo wilayani Nkasi kwa kosa la kujaribu kumbaka Bibi kizee Maria Tenganamba (60).

Akisoma hukumu hiyo jana, Hakimu mkazi wa mahakama hiyo Ramadhani Rugemalila alisema mahakama hiyo imeridhishwa na ushahidi pamoja na maelezo ya upande wa mashitaka pasipo kuacha shaka yoyote  na kumtia hatiani mtuhumiwa huyo ndipo alipotoa hukumu hiyo ya miaka 30 jela kwa kuzingatia kifungu Na,132 cha kanuni ya adhabu sura ya 16 kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka wa 2002.

Awali mwendesha mashitaka wa polisi Hamimu Gwelo aliieleza mahakama hiyo kuwa mtuhumiwa huyo alitenda kosa hilo Oktoba 16 mwaka jana nyumbani kwa Bibi huyo maeneo ya Nkomolo wilayani Nkasi majira ya saa 11 jioni ambapo mtuhumiwa alimvamia bibi huyo na kutaka kumbaka.

Alisema akiwa katika jaribio hilo kabla ya kufanikiwa kutekeleza kosa hilo Bibi huyo alipiga kelele na kuokolewa na baadhi ya vijana waliokuwa karibu na eneo hilo ndipo walipofanikiwa kumkamata kijana huyo akiwa uchi na kumfikisha Polisi.

Upande wa mashitaka uliwakilishwa na mashahidi watatu ambao walitoa ushahidi ambao haukuwa na mashaka wakati mtuhumiwa alijitetea mwenyewe.ambapo aliiomba Mahakama impunguzie adhabu kutokana na kwamba amekaa muda mrefu Mahabusu na anategemewa katika familia yao.

Upande wa jamhuri uliiomba mahakama hiyo kutoa adhabu kali kwa mtuhumiwa ili iwe fundisho kwa watu wengine, ndipo mahakama hiyo iliamua kutoa adhabu ya miaka 30 jela ikizingatia ombi la jamhuri kwa nia ya kukomesha vitendo hivyo.

Na Israel  Mwaisaka
Nkasi

No comments:

Post a Comment