Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Friday, November 6, 2015

Amawawa mkombozi wa uchumi wa mkulima Rukwa anayechechemea.

 Na Joachim Nyambo

ASILIMIA kubwa ya kilimo kinachoendeshwa mkoani Rukwa nchini Tanzania ni kile cha kizamani na kisichokuwa na tija kubwa katika kumwinua mkulima na mfugaji kiuchumi.Wakulima wengi mkoani hapa bado wanalima kilimo cha kutegemea mazao ya muda mrefu hususani mahindi,maharage,ulezi,mtama na karanga.

Kilimo cha mazao haya kimekuwa na changamoto nyingine kwakuwa hutumia mizezi mingi tangu kupandwa kwa zao husika hadi kukomaa na kufikia mavuno.Kwa zao kama mahindi mkulima hulazimika kutumia kati ya miezi mine mpaka mitano kuvuna.Kipindi hiki ni kirefu mna na huathiri mapato ya mkulima.

Ufugaji pia unaofanyika mkoani hapa si ule wa kisasa.Wafugaji wengi wanafuga ng’ombe,mbuzi,kuku,bata na nguruwe kwa kutumia mazoea.Hawafugi kibiashara hatua ambayo ingewainua haraka kiuchumi iwapo wangebadilishwa.

Kilimo hiki kisicho na tija ndicho kilipelekea wadau wachache kukaa na kuibuka na wazo la kuanzisha Asasi ya Maendeleo ya Kilimo na Wafugaji(Amawawa).Mwaka 2009 ndipo kilipoundwa chombo hiki.

Lengo la kuanzishwa kwa Amawawa ni kuwawezesha wakulima na wafugaji wadogo kuwa na nguvu ya pamoja.Waweze kuwa na sauti ya pamoja ya kutetea na kutatua changamoto zinazowakabili ambazo kwa muda mrefu zimekuwa zikikwamisha jitihada zao za kupiga hatua kimaendeleo kupitia shughuli zao za kiuchumi.

Kutokana na unyeti wa jambo husika,kupitia asasi hii waanzilishi wake wakaona jambo la kwanza na muhimu kufanikisha lengo la kuanzisha kwake ni kuwa na kituo cha kutoa elimu ya kilimo na ufugaji wa kisasa kwa vitendo na si kuishia kuzungumza kama wanavyofanya wadau wengi wa kilimo.Wengi wamekuwa wakiishia kupiga porojo majukwaani na utekelezaji wao kuishia kwenye makabrasha na vipeperushi.

Katibu wa Amawawa Petro Milambo anasema walengwa wakuu wa kituo hiki ni vijana.Hao ndio wanaopaswa kunufaika kwa kiasi kikubwa na uwepo wa kituo hicho kilichopo nje kidogo ya manispaa ya Sumbawanga.Kwa kupata mafunzo ya kilimo na ufugaji wa kisasa wataweza kuona umuhimu wa kujiajiri kupitia shughuli hizo.

Milambo anasema vijana wengi wamekuwa wakivikimbia vijiji vyao na kwenda mijini wakiamini huko kuna unafuu mkubwa wa upatikanaji wa ajira.Lakini matokeo yake huko mijini wemekuwa wakijikuta wanaingia kwenye makundi ya vijana yenye kujihusisha na matukio mbalimbali ya uhalifu.

“Vijana wengi wamekuwa na imani potofu kuwa mijini pekee ndiko wanakoweza kupata mafanikio ya haraka.Lakini hii yote ni kutokana na kilimo kuonekana hakiwaletei tija vijijini kwao.Huko mijini matokeo yake imekuwa ni kujiunga na vikundi vinavofanya mambo maovu kama wizi na matumizi ya dawa za kulevya”

“Lakini wanakimbia kilimo kwakuwa hawaoni kama kinaweza kuwaajiri.Tunapowapa elimu tunawahamasisha kulima na kufuga kwa njia za kisasa ni dhahiri wataweza kujiajiri wakiwa vijijini kwao.Kamwe hawatatamani kwenda mijini kwakuwa tayari wamekwishaona mifano ya wenzao waliokwenda huko na hawakupata mafanikio.Badala yake walirudi wakiwa wameharibikiwa baadhi yao wakiwa wagongwa baada ya kuambukizwa virusi vya ukimwi” alisema Milambo.


AMilambo anasema kwa vijana kunufaika na ajira za kilimo na ufugaji wa kisasa wakiwa vijijini kwao kunawezesha hata wenzao waliokimbia kurudi na kuungana nao ili kwa pamoja waweze kuunganisha nguvu kwenye shughuli hizo.Kwa sasa  vijana wengi wanakimbilia mjini na kuiacha sekta ya kilimo bila nguvu kazi kwani wazee wao ndio wanaobaki wakijihusisha na shughuli hiyo.

“Kwa hapa kituoni vijana ambao wanakuwa wakija kupata mafunzo hapa kwa vitendo wanaweza kujifunza mambo mbalimbali.Wakiwa hapa wanajifunza kilimo cha matunda na mboga mboga kama unavyojua mkoa wa Rukwa hamasa ya kilimo cha matunda bado ni ndogo ikilinganishwa na mikoa jirani kama Mbeya.Lakini kilimo cha matunda kina manufaa makubwa mno.Tukidhamiria kwa dhati kujikita katika kilimo hiki vijana wanaweza kujikuta wanapata mafanikio kwa muda mfupi sana na umaskini unaowasumbua kwa sasa ukabaki katika historia.Matunda kama mapera na matunda jiwe yanastawi sana mkoani hapa lakini hayalimwi kwa malengo”

“Lakini pia kilimo cha mboga mboga kinachofanyika mkoani hapa ni cha kizamani.Wakulima hawalimi kwa matarajio makubwa na kuona kama kinaweza kuwasaidia kunyanyuka kimaendeleo na jamii ikabaki inashangaa.Tunatambua kuna tatizo la miundombinu hasa ya kilimo cha umwagiliaji lakini tunaamini serikali nayo ina wajibu wa kujipanga kuwasaidia vijana hasa inapoona wadau wengine tunatekeleza kwa upande wetu” anasema 

Katibu huyo wa Amawawa anasema katika msimu wa 2014-2015 Kitruo hicho kilianza kutekeleza adhama ya kilimo cha matunda.Anasema anasema shamba darasa lenye ukubwa wa ekari moja lililimwa na kufanikiwa kuvuna kiasi cha tani 2.5 za matunda aina ya tikiti maji.

“Tikitimaji ni kilimo kinachotumia miezi mitatu tu.Hivyo tulikuwa na misimu kadhaa ya kilimo hiki licha ya kuwa katika msimu huo tulikumbwa na changamoto ya uhaba wa maji kwakuwa kutokana na mvua kuwa kidogo msimu wa kiangazi ulikuwa mkubwa na hivyo kukawa na ukame”

Milambo anasema kupitia shamba darasa la kilimo cha tikiti chuoni hapo wapo wakulima hususani vijana waliopata fursa ya kujifunza kilimo hicho  waliporudi makwao waliweza kutumia teknolojia hiyo na wanaendelea kunufaika nayo.

“Unaweza usiamini lakini wanaojifanyia kazi elimu waliyoipata hapa wananufaika kwa kiasi kikubwa licha ya uwepo wa changamoto ya upungufu wa maji.Mpaka leo wapo ambao uchumi wao umeonesha kukua kwani wameweza kununua mifugo kama Ngombe,Mbuzi na wapo pia waliojenga nyumba za kisasa na kuezeka bati badala ya nyasi kama ilivyokuwa awali.”

“Takribani vijana 35 kutoka manispaa ya Sumbawanga na pia Sumbawanga vijijini walifika kituoni hapa kupata elimu ya kilimo cha matikiti maji kwa kipindi hicho.Kilimno hiki kimeonekana kuwa na manufaa kwao kwakuwa soko lake si la kusuasua kama ilivyo kwa mazao kama mahindi.Matikiti yanapokomaa kazi yako ni kutafuta mteja tena wa jumla na akija shambani unavuna na kukabidhiana naye papo hapo”

Amawawa pia inalenga kufundisha vijana ufugaji wa kisasa wa Sungura,nguruwe,kuku,mbuzi na ndezi.Uongozi wa kituo unaamini hiyo yote ni miradi yenye kuweza kumwingizia kipato kijana mmoja mmoja au wakiwa katika kikundi.Kijana ama kikundi kikilima mchicha wakati huo huo kikawa na ng’ombe wa maziwa au mbuzi na pia mifugo mingine midogomidogo hatoweza kukosa fedha.

Ufugaji wa nyuki na samaki ni mafunzo mengine yanayotolewa kituoni hapo kwa vijana.Ufugaji huu unawezesha kwa kiasi kikubwa utunzaji wa mazingira ambayo kwa kiasi kikubwa yameharibiwa na kilimo cha mfumo wa kizamani.Miti na misitu mingi imefyekwa ili kupata mashamba ya kulima.Lakini pia upo uchomaji moto wa mapori kwaajili ya baadhi ya watu kutafuta wanyama wadogo wa porini kwaajili ya kitoweo.

Kwa kufuga samaki na nyuki kwa njia za kisasa vitoweo vitapatikana kwa urahisi na vijana watajiingizia vipato kwa kuuza samaki,asali na pi nta kutokana na mazao hayo kuwa na soko zuri.Hii pia itasaidia kutunzwa kwa mazingira kwa kutochomwa moto misitu na kufyekwa hovyo miti.


“Yapo mambo mengi mazuri ambayo vijana wakiwa hapa watajifunza.Na tunataka wakitoka hapa waone kuwa awali walikuwa wakicheza mijiji na waweze kujipanga kuanza maisha upya wakitaraji neema kwa wakati mfupi.Lini hatutoishia kutoa elimu kwa vijana watakaofika kituoni hapa pekee.Tunataka pia wakulima wawe wanapanga ziara za kimafunzo na kuja hapa kujifunza wakaondoka”

Mwenyekiti wa Amawawa Oscar Msangi anasema pamoja na mipango hiyo mizuri ya kituo,changamoto zinaonekana kuwa nyingi zaidi ya uwezo wa kuzikabili.Ukosefu wa rasirimali fedha umekuwa kikazo kikubwa.

“Shughuli zetu zote zinahitaji fedha.Tulitegemea zaidi nguvu ya wafadhili mbalimbali ili kumudu gharama za uendeshaji wa kituo hiki.Tunahitaji vijana wanaokuja kujifunza wakae hapa kituoni na si watoke mbali.Tumejitahidi kujenga majengo kwaajili ya mabweni kwa kuchanga fedha zetu za mifukoni.”

“Tunao uhitaji wa samani kama vitanda,meza na viti.Tunahitaji pia magodoro kwaajili ya kulalia vijana wawapo kituoni hapa wakijifunza.Tatizo fedha hatuna.Tunajaribu kushirikisha wadau wengine bado hatujakata tama tunaamini siku moja tutafanikisha lengo la kuinua uchumi wa mkulima ” anasisitiza Msangi.

Mwenyekiti huyo anasema changamoto nyingine ni hali ya ukame.Hii imeleta ugumu katika suala zima la ufugaji wa samaki katika mabwawa.Anasema kutokana na ukame sehemu kubwa ya mabwawa kituoni hapo yamekauka na kusababisha samaki wengi kufa.Hasara inayokadiriwa kuwa zaidi ya shilingi 5000,000 za kitanzania imepatikana kutokana na kukauka kwa mabwawa hayo.

Kwa mujibu wa mamlaka ya hali ya hewa nchini,msimu wa kilimo mwa mwaka 2015/2016 unatarajiwa kuwa na mvua nyingi.Kwa Amawawa hii ni neema inayotarajiwa.Kituo hiki kinaamini kuwa kwa uwepo wa mvua nyingi msimu huu mabwawa yatajaa maji na ufugaji wa samaki utarejea katika hali ya kawaida.Wanaamini pia vyanzo vingi vya maji hususani mbuga zitakuwa na maji ya kutosha kwaajili ya kilimo cha mboga mboga na matunda.Hii itawezesha kituo kuwa na mashamba darasa endelevu na pia wakulima wanapojifunza kwenda kufanya vizuri kwenye mashamba yao.

“Jana tu hapa Sumbawanga imenyesha mvua kubwa sana.Kwetu sisi tunapata matumaini kwakuwa tunahitaji maji mengi kufanya shughuli kituoni kwetu na pia kwenye mashamba ya wakulima tunaowafundisha.Pasipo maji ya kutosha hatuwezi kufanikiwa kitu.Ndiyo sababu tunahimiza pia suala la utunzaji wa mazingira.” Anasema Msangi.

Tunahitaji pia fedha kwaajili ya kufanikisha mradi wa maji ya mserereko.Yapo umbali wa takribani mita 600 kutoka kituoni hapa.Kituo kinataraji kutega na kuyavuta kwaajili ya matumizi ya kilimo.
 
Msangi anasema changamoto ya rasilimali fedha pia inatokana na kupungua kwa asilimia kubwa kwa waanzilishi wa asasi hii.Kati ya waasisi 30 ni 15 pekee waliosalia hivyo kusababisha nguvu ya utafutaji ufadhili kupungua Anasema wengi wa waasisi wamekimbia majukumu ya kuchangishwa kila kunapokucha.

No comments:

Post a Comment