Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Friday, November 13, 2015

Kandoro ataja chanzo cha migogoro ya wakulima,wafugaji

Mkuu wa mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro akisisitiza suala la utunzaji mazingira wakati wa kufungua warsha

Naibu katibu mkuu wizara ya Maji mhandisi Ngosi Mwihava akitoa taarifa ya mradi wa tathmini ya maji.


 MKUU wa mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro amesema kupungua kwa maji ardhini ni miongoni mwa mambo yanayochangia kwa kiasi kikubwa migogoro ya ardhi baina ya wakulima na wafugaji.

Kandoro aliyasema hayo alipofungua warsha ya siku mbili ya kujadili  taarifa ya Mpango wa pamoja wa usimamizi na uendelezaji wa rasilimali za maji katika bonde la maji la Ziwa Rukwa inayofanyika jijini Mbeya ikihudhuriwa na wadau mbalimbali kutoka mikoa ya Mbeya,Rukwa na Katavi.

Mkuu huyo wa mkoa alisema mara nyingi wakulima na wafugaji wamekuwa wakigombania maeneo yaliyo na maji ya kutosha kwaajili ya kulishia mifugo au kilimo.

“Haukuti watu wakipigana kwaajili ya jangwa,labda kama kuna mafuta.Wanapigana kwakuwa kila mmoja anataka eneo lililo na unyevu linalotesha nyasi.Sasa kadiri maji yanavyopungua ndivyo na migogoro hapa nchini kati ya wakulima na wafugaji inaongezeka” alisema.

Alisisitiza halmashauri kuhakikisha zinakuwa na sheria ndogo zitakazowezesha kudhibiti uharibifu wa mazingira na kuyafanya yawe endelevu kwa manufaa ya kizazi kilichopo na kijacho.

Kandoro pia alisisitiza ushiriki wa wananchi kwenye mipango mbalimbali ya utunzaji mazingira akisema wao ndiyo wahusika wakubwa katika athari zozote zitokanazo na uharibifu unaoendelea kufanyika.

Alisema ni jambo la msingi kila mwananchi mahali alipo atambue umuhimu wa utunzaji mazingira sambamba na kushiriki katika mikakati inayowekwa na wadau wa masuala hayo.

Kwa upande wake Naibu katibu mkuu wizara ya Maji mhandisi Ngosi Mwihava alisema serikali imejipanga kuhakikisha tahtimini juu ya uwepo wa maji katika mabonde ya maji zinafanyika ili kuwa na uhakika wa kiasi hali cha maji kilichopo sambamba na matumizi sahihi.

PICHA KWA HISANI YA KENETH NGELESI

No comments:

Post a Comment