MGOMBEA anaewania nafasi ya
kugombea ubunge wa Iringa mjini kwa tiketi ya CCM, Mwanahabari Frank Kibiki
ameahidi kushirikiana na wadau wa soka kupandisha daraja timu ya soka ya Lipuli
ya mjini Iringa iwapo atapewa ridhaa ya kupeperusha bendera ya CCM katika uchaguzi
mkuu ujao.
Akizungumza wakati wa kampeni za
kujinadi zilizofanyika katika eneo la Kihesa kilolo, mjini Iringa Kibiki
alisema michezo ni fursa ambayo inaweza kuinua uchumi wa mkoa wa Iringa endapo
itapatiwa kipaumbele.
Alisema ikiwa atapewa ridhaa ya kuwa mbunge,
atakaa chini na wadau wa soka wa manispaa ya Iringa na kuweka mikakati
madhubuti ili kuhakikisha wananchi Lipuli inapanda daraja.
“Ndugu zangu, Lipuli ikipanda daraja uchumi wa
Iringa mjini utakuwa kwa sababu vijana watapata ajira kwa sababu kwenye uwanja
wetu wa samora, zitachezwa timu za kimataifa,” alisema Kibiki.
Aidha alisema kuwa ataimarisha timu
nyingine za mjini Iringa ili ziweze kupanda madaraja sambamba na kuinua sekta
ya sanaa hasa muziki.
Katika hatua nyingine, Kibiki
aliwashauri vijana kujiunga kwenye vikundi vya ujasiriamali na kutumia fursa
zilizopo kwenye maeneo yao ili waweze kujiajiri na hivyo kujikwamua na hali
ngumu ya maisha.
Kibiki alisema, umoja ni nguvu na
ikiwa vijana watajiunga kwenye vikundi hivyo vya kiujasiriamali itakuwa rahisi
kufanikiwa kiuchumi.
Alisema maeneo mengi ambayo vijana
wameungana wameweza kukopeshwa, na wanaendesha shughuli zao za kiuchumi bila
wasi wasi, jambo hilo linawezekana.
No comments:
Post a Comment