Friday, June 28, 2013
MTOTO APOTEA KATIKA MAZINGIRA TATANISHI,HISIA ZA KUUAWA ZATANDA KWA JAMII
JINAMIZI la kuibwa kwa watoto limezidi kuukabili mkoa wa Mbeya baada
ya mtoto Victor Ngisa(4) wa kitongoji cha Barabarani kata ya Lugelele
wilayani Mbarali kupotea katika mazingira ya kutatanisha.
Kwa mujibu wa mama mzazi wa mtoto huyo Grace Muhuzi hadi leo ni siku
saba zimepita tangu kupotea kwa mwanaye na juhudi za
kumtafuta zinaonekana kutokuwa na mafaninikio.
Akizungumza na Lyamba Lya Mfipa kwa njia ya simu Grace alisema mwanaye
alitoweka katika mazingira ya kutatanisha tangu juni 22 majira ya saa
tatu asubuhi alipokuwa akicheza na watoto wenzake.
Mama huyo alisema alimwacha mwanaye nyumbani kwa mama yake mdogo
kwakuwa yeye alikwenda msitu uliopo jirani kwaajili ya kufuata kuni
kwa matumizi ya nyumbani lakini aliporudi hakuweza kukutana tena na
mwanaye huyo hadi leo hii.
Alisema baada ya kurudi alikutana na mtoto mkubwa kati ya watatu
waliokuwa wakicheza na mwanaye na alipomuuliza akasema wenzake
walikwenda kuchuma ubuyu katika vichaka vilivyopo jirani na nyumbani
kwao lakini alipojaribu kuwafuata huko akakutana na mtoto mwingine na
kuambiwa mtoto Victor alilala kabla hajatokea mtu mmoja aliyevaa koti
refu jeusi kuwatisha na wao kukimbia.
Alisema baada ya watoto hao kukimbia kwa kutishwa na baadaye kubaini
walimuacha mwenzao walirejea kwaajili ya kumfuata lakini hawakumkuta
tena hivyo wakawa na imani alichukuliwa na mtu huyo wa jinsia ya kiume
aliyewatisha.
Grace alisema alilazimika kuwafahamisha majirani na jitihada za
kumtafuta mtoto huyo zikaanza mara moja na ndipo walipoanza kukutana
na taarifa tofauti tofauti kwa kuambiwa na baadhi ya watu kuwa
walimuona mtu mmoja akiwa na mtoto mdogo katika maeneo na nyakati
tofauti
“Kwa siku ya kwanza tulitafuta mpaka usiku bila mafanikio wala taarifa
yoyote.Siku ya pili tukiendelea kutafuta tukakutana na watu wakasema
walimuona wakiwa wanaelekea machimboni.Siku ya tatu tukakutana na watu
wengine wakasema walimuona msukuma mmoja akiwa na mtoto akimnunulia
chakula maeneo ya Madibira.Naumia sana kutomuona mwanangu hadi leo”
alisema Grace.
Mama huyo alisema si tukio la kwanza kutokea wilayani hapo kwani
watoto na hata watu wazima wamekuwa wakipotea katika mazingira ya
kutatanisha na miili yao kuokotwa baada ya siku kadhaa ikiwa
imeharibika vichakani.
Kwa upande wake mwenyekiti wa kitongoji cha Barabarani Ramadhan
Mkatilwa alisema alipokea taarifa ya kupotea kwa mtoto Victor Juni 22
mwaka huu majira ya saa 12 jioni na kulazimika kupiga mbiu kukusanya
wakazi wa eneo hilo na jitihada za kumtafuta zikaanza.
Alisema katika siku zote za kumtafuta mtoto huyo wametumia njia
mbalimbali ikiwemo wamiliki wqa pikipiki kusafiri umbali mrefu kutoa
taarifa kwa vijiji jirani lakini hakuna mafanikio yoyote.
Mwenyekiti huyo alikiri kuwa si mara ya pili kwa tukio la kuibwa kwa
mtoto kutokea eneo hilo kwani Mei 2012 mtoto mmoja aliibwa lakini
kwakuwa mama yake alibaini mapema akapiga yowe na watu walipokusanyika
mtu aliyemuiba akamtelekeza porini na kukimbilia kusikojulikana.
Kamanda wa polisi mkoani hapa Diwani Athuman awali alisema hana
taarifa za kupotea kwa mtoto huyo na kuomba mawasiliano ya wazazi wa
mtoto na ndipo alipoamuru mkuu wa kituo cha polisi wilayani Mbarali
kufika eneo husika na kupewa taarifa halisi.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment