Monday, July 1, 2013
WATATU WAUAWA KIKATILI MBEYA
WATU watatu wamefariki dunia katika matukio tofauti yaliyotokea Juni 30
mwaka huu mkoani Mbeya,yakiwemo mawili ya watu kuuawa na watu wasiojulikana.
Mmoja wa waliouawa ni mkazi wa kijiji cha Iyendwa wilayani Momba Geofray
Simpungwe(45) aliyekutwa porini ametundikwa mtini kwa kamba mithiri ya mtu
aliyejinyonga huku mwili wake ukiwa na majeraha ya kupigwa.
Kaimu kamanda wa polisi mkoani hapa Barakael Masaki amesema mwili wa
Simpungwe umekutwa majira ya saa 11 jioni umbali wa kilometa mbili kutoka
eneo la makazi huku ikidaiwa kuwa marehemu alikuwa akituhumiwa kwa uchawi
kijijini hapo.
Masaki amesema tukio la pili ni la mauaji ya mkazi wa kijiji cha Nsongwi
Mandanji aliyefahamika kwa jina la Ame Dundai(25) aliyekutwa majira ya saa
12 asubuhi kijijini hapo akiwa ameuawa kwa kuchomwa moto kwa kutumia
gurudumu la gari huku ikidaiwa kuwa ni mwizi.
Tukio la tatu ni ajali ya gari aina ya Noah isiyoifahamika namba wala
dereva wake iliyoacha njia na kumgonga mtembea kwa miguu Helena Ukupama(68)
mkazi wa Garijembe wilayani Mbeya na kusababisha kifo chake papo hapo
majira ya saa 1:30 usiku kijijini hapo.
Kaimu Kamanda huyo amesema jeshi hilo linaendelea na uchunguzi wa matukio
yote matatu,sambamba na kuwasaka waliosababisha vifo hivyo ili hatua za
kisheria zichukuliwe dhidi yao.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment