Wednesday, December 18, 2013
MWANAFUNZI WA DARASA LA PILI AFA MAJI AKIOGELEA MTO CHUNYA
MVUA zinazoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali mkoani hapa zimeendelea kuleta maafa kwa kuwezesha mito kujaa maji na kusababisha vifo vya watoto wanaoogelea.
Ikiwa ni siku chache tu zimepita tangu mtoto mmoja aripotiwe kufa maji huko wilayani Mbarali alipokuwa akiogelea mtoni na wenzake,jeshi la polisi mkoani hapa limesema mtoto mwingine amekufa maji wilayani Chunya.
Kaimu kamanda wa polisi mkoani Mbeya Barakael Masaki amesema leo kuwa aliyekufa maji ni mwanafunzi wa darasa la pili katika shule ya msingi Chokaa wilayani Chunya aliyemtaja kwa jina la Ezekia Azigeti(10).
Kamanda Masaki amesema mwanafunzi huyo alipoteza maisha Desemba 16 mwaka huu majira ya saa 10:00 jioni baada ya kuzidiwa na maji alipokuwa akiogelea katika mto Chunya.
Aidha kaimu kamanda huyo ametoa wito kwa wazazi na walezi wa watoto mkoani Mbeya kuwa makini na watoto wao katika kipindi hiki ambacho mvua zinaendelea kunyesha kwa kuwakanya kwenda kuoga katika mito,mabawa au madimbwi ya maji.
Amewataka pia wakazi kuhakikisha wanachukua tahadhari kwa kufukia au kufunika na kuziba mashimo na visima vilivyo wazi ili kuepusha vifo vya watoto vitokanavyo na maji.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment