BARAZA la madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Mbozi Mkoani Mbeya limekataa mapendekezo ya bajeti ya mwaka wa fedha 2012/2013 yaliyokuwa yameandaliwa na wataalamu wa halmashauri hiyo.
Kukataliwa kwa bajeti hiyo kumetokana na madiwani kutoridhika na makisio ya ukusanyaji mapato ambapo madiwani wamesema kiasi cha shilingi bilioni 2 na milioni 20 kilichokuwa kimepangwa ni kadirio dogo ikilinganishwa na vyanzo vya mapato vilivyopo.
Katika kikao cha baraza hilo baadhi ya madiwani wamependekeza makadirio ya makusanyo yafikie bilioni 3 hasa kutokana na matarajio makubwa yaliyopo kwenye mavuno ya zao la kahawa mwaka huu.
Madiwani hao Barton Sinyanga,Gaudance Simfukwe na Eva Mlonganile wamesema halmashauri inao uwezo mkubwa wa kukusanya fedha nyingi iwapo nguvu ya kudhibiti uvujaji wa mapato itaimarika.
Baada ya mvutano wa muda mrefu baina ya upande wa madiwani ukiongozwa na mwenyekiti wao Elick Ambakisye na upande wa wataalamu ukiongozwa na mkurugenzi wa halmashauri Levison Chilewa baraza hilo limefikia uamuzi wa kuongeza makadirio ya makusanyo hadi kufikia bilioni 2.5.
No comments:
Post a Comment