Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Saturday, June 23, 2012

HAMASA YAKWAMISHA CHF MBEYA


HAMASA ndogo juu ya mfuko wa  afya ya jamii(CHF) imetajwa kuwa sababu kubwa ya wakazi mkoani Mbeya kutotambua umuhimu wa mfuko huo hivyo hawajiungi.

Hali hiyo imebainika katika semina elekezi kwa waratibu na waandishi wa habari mkoani Mbeya kuhusu Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) iliyofanyika katika ukumbi wa hospitali ya mkoa.

Meneja wa NHIF kanda ya nyanda za juu kusini Selestin Muganga alisema hamasa bado hali inayosababisha wananchi kutojiunga na CHF kutokana na kukosa elimu juu ya mfuko huo.

Muganga alizitupia lawama halmashauri kwa kutolipa kipaumbele suala la utoaji elimu hiyo kupitia kwa waratibu wa mfuko huo na kusema viongozi wengi wa halmashauri hiyo wanazingatia miradi inayokuwa na maslahi ya moja kwa moja kwao na si ile inayolenga kuinufaisha halmashauri kama huo.

Alihimiza kuwepo kwa hali ya ushindani kwa kila wilaya juu ya mafanikio ya mfuko huo akisema hali hiyo itachochea kwa kiasi kikubwa halmashauri zilizolala kuona zimebaki nyuma hivyo kuona aibu na muiga mfano wa wenzao wanaofanya vizuri.

Awali akifungua semina hiyo ya siku moja mganga mkuu wa mkoa wa Mbeya Seif Mhina alihimiza hamasa ya CHF kutolewa katika msimu wa mavuno kama sasa wakati ambao wananchi wengi hususani wakulima wanakuwa na kipato kizuri madala ya masika.

Dokta Mhina alisema wananchi wanatumia fedha nyingi kugharamia matibabu ya wana familia jambo linaloashiria kuwa elimu juu ya CHF haijawafikia hivyo hawatambui kuwepo kwa uwezekano wa wanakaya kupata matibabu kwa shilingi 10,000 tu kwa mwaka mzima.

“Mkielimisha hakuna mtu atakayebisha.Tatizo ni elimu bado haijawafikia Wananchi wanatumia pesa nyingi sana kwa matibabu ya kawaida tu.Tukiwahamasisha kuwa kaya zao zinaweza kutibiwa kwa shilingi 10,000 kwa mwaka mzima wataridhia tu” alisema

Alisema kujiunga kwa wingi kwa wananchi mkoani hapa kunaweza kusaidia pia kupunguza kwa kiasi kikubwa changamoto zinazoikabili huduma ya afya katika zahanati,vituo vya afya na hospitali zilizopo.

Aliutaja mkoa huo kuwa na kaya zipatazo laki sita ambazo zikijiunga zote na CHF zitawezesha kupatikana kwa shilingi bilioni sita na bima ya afya kupitia mpango wa Tele kwa tele ikichangia bilioni sita mkoa utakuwa na jumla ya shilingi bilioni 12 ukiachilia mbali fedha zitakazotoka serikalini ambazo ni za OC shilingi bilioni 2 na za kapu(Busket Fund) bilioni tano.

Alisema fedha hizo zinatosha kabisa kutatua changamoto zote zilizopo ikiwa ni pamoja na ununuzi wa dawa kwa matumizi ya mwaka mzima,ununuzi wa vifaatiba na ujenzi na ukarabati wa majengo mbalimbali.

Kwa mujibu wa takwimu kutoka NHIF kwa mkoani Mbeya zipo kaya 612,216 na kati ya hizo 17,988 sawa na asilimia 2.94 ndizo zilizojiunga na CHF ambapo wilaya ya Kyela iliyo na kaya 39,542 inaongoza kwa kuwa na kaya 4,447 zilizosajiriwa na Ileje iliyo na kaya 32,153 ni ya mwisho kwa kuwa na kaya 97 pekee zilizosajiriwa.

No comments:

Post a Comment