Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Tuesday, June 26, 2012

KIAMA CHA MADAKTARI WALIOGOMA MBEYA

SERIKALI mkoani Mbeya imetishia kukatisha mikataba ya madaktari watakaoendeleza mgomo mpaka siku ya kesho(Juni 27) ikiwa ni siku tano mfululizo hawajaingia kazini.

Kaimu mkuu wa mkoa wa Mbeya Dk.Norman Fegi ameyasema hayo leo (Juni 26) katika kikao chake na waandishi wa habari ikiwa ni siku ya nne mfululizo tangu baadhi ya madaktari katika hospitali ya Rufaa kuanza mgomo.

Dk.Fegi amesema tangu kuanza kwa mgomo huo serikali ya mkoa kupitia mkuu wa mkoa ambaye kisheria ndiye mwenyekiti wa bodi ya hospitali inayoingia mkataba na madaktari wa mafunzo imeshawaandikia barua za kuwaita ili wafanye mazungumzo lakini jana(Juni 25) hawakufika.

Amesema baada ya kutofika huko mkoa ukawaandikia tena barua kwa kila mmoja wao kujibui ni kwa nini asiwajibishwe na kusisitiza kuwa iwapo mpaka siku ya tano hawatafika kazini mkoa utavunja mkataba na kuwarudisha kwa muajiri yaani wizara husika.

Amesema kwa sasa wamelazimika kuchukua baadhi ya madaktari kutoka vituo vya afya vilivyopo jijini Mbeya na ndiyo wanaendelea kutoa huduma hususani katika kitengo cha upasuaji cha hospitali ya Rufaa ambacho ndicho kimeathiriwa zaidi.

Kwa upande wake mkurugenzi wa hospitali ya mkoa Dk.Eliuter Samky alisema madaktari waliogoma ni 45 waliopo katika mafunzo na 19 waliosajiriwa lakini wameajiriwa hivi karibuni lakini madaktari bingwa 19 wanaendelea na kazi kama kawaida.

Samky amesema wateja wote waliofika hospitalini hapo tangu kuanza kwa mgomo wameathirika kwa namna moja ama nyingine ikiwa ni kwakupata huduma isiyo katika kiwango ama muda wa kawaida au kisaikolojia.

Amesema tangu kuanza kwa mgomo huo haijatokea kifo lakini wagonjwa 250 wamefikishwa na kulazwa wakati wagonjwa wan je jumamosi walifika 53,jumapili 42 na jumatatu 283.

Amesema siku ya jumapili pia ilitokea ajali ya gari na majeruhi 16 wakafikishwa hospitalini hapo na wote walipata huduma japo si kwa kiwango kilichozoeleka siku zote.

Naye mganga mkuu wa mkoa dokta Seif Mhina alisema mgomo wa madaktari katika hospitali ya rufaa imeongeza msongamano wa wagonjwa katika hospitali ya mkoa hususani akina mama wajawazito waliokwenda kujifungua katika hospitali hiyo kitengo cha wazazi Meta na kukosa huduma ndipo wakaamua kukimbilia hapo.

Mhina amesema wajawazito wanaojifungua katika hospitali ya mkoa wameongezeka kutoka wawili hadi watano kwa siku na kufikia zaidi ya kumi huku wanaopata huduma ya upasuaji wakiongezeka kutoka mmoja kwa siku hadi kati ya watano na kumi.

No comments:

Post a Comment